Thursday, November 5, 2015

KWA CHAMA CHA MAPINDUZI (CCM), UCHAGUZI HUU UWE FUNDISHO LA MWISHO


Ushindi wa Chama cha Mapinduzi katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015 unabaki na utaendelea kubaki kuwa funzo kubwa tofauti na chaguzi zilizopita. Tanzania ilirejesha mfumo wa demokrasia ya vyama vingi mwaka 1992 baada ya kuufuta miaka ya sitini mwanzoni. Mfumo wa vyama vingi ulirejeshwa baada ya serikali kuwahoji wananchi kupitia Tume ya Jaji Nyalali ambaye pamoja na mambo mengine alihoji wananchi kama Tanzania ilikuwa tayari kuingia katika siasa za vyama vingi.

Katika hali ambayo ilishangaza wengi miongoni mwa wasomi na wananchi wa daraja la kati na juu, wananchi kwa zaidi ya asilimia 80 walipendekeza mfumo wa chama kimoja uendelee. Kipindi kile busara na hasa ya viongozi wa Chama cha Mapinduzi (CCM) akiwemo Mwalimu Nyerere walionelea ni vema tukaingia katika mfumo wa vyama vingi. Msingi wa busara na hekima hii ilitokana na ukweli kwamba katika maoni ya wale wananchi wengi waliopendekeza mfumo wa vyama vingi uendelee walitoa mapendekezo makubwa ambayo iwapo yangefanyiwa kazi ipasavyo tusingeweza kuwa tena na mfumo wa chama kimoja.

Wengi ya wana CCM kipindi kile hawakuonesha kufurahishwa na hatua ile kwasababu tayari kulikuwa na hali ya mazoea, kwa maneno mengine chama ndio kilikuwa kila kitu. Chama kilikuwa katika kipindi chote hadi mwaka 1992 kimeshika hatamu au “party supremacy”, kimsingi Serikali ilipata maelekezo kutoka katika chama na halkadharika Bunge nalo lilipata msukumo mkubwa kutoka katika chama. Mfano mzuri wa Chama kushika hatamu ulijidhihirisha wakati wa vuguvugu la G55 yaliyopelekea Bunge kupitisha azimio la kuundwa kwa serikali ya Tanganyika.

Baafa ya mjadala mzito wa ndani ilikubalika kwamba sera ya Chama cha Mapinduzi ni Serikali Mbili na ni uamuzi uliopitishwa na chama tena kwa turufu ya wanachama wenyewe. Ukiachilia mbali kwamba uamuzi ule wa Bunge ulighubikwa na mihemko ambayo haikuwa imetaarifiwa sawasawa na uhalisia. Baada ya vuta-nikuvute uamuzi wa chama ulitamalaki na maisha yakaendelea.

Mwaka 1995 ndio ilikuwa Uchaguzi Mkuu wa kwanza katika mfumo wa demokrasia ya vyama vingi. Uchaguzi wa mwaka 1995 ulikuwa na changamoto na mhemko mkubwa kama huu wa miaka 20 baadaye yaani mwaka 2015. Ikumbukwe mwaka 1995 Naibu Waziri Mkuu aliondoka CCM akahamia chama cha upinzani kipindi hicho. Kampeni zilichagizwa na mihemko na mashamsham kama ya mwaka huu. Kipindi hiki naona watu wanajitambua zaidi kwamba baada ya mkutano gari ya Mhe. Lowassa iliachwa itembee yenyewe kuelekea nyumbani kwake baada ya mkutano. Mwaka 1995 gari ya Mhe. Agostino Lyatonga Mrema haikuachwa iwashwe na kutembea yenyewe, bali ilisukumwa mpaka nyumbani kwake.

Ikumbukwe pia mwaka 1995 mgombea wa CCM, Mzee Mkapa hakuwa almaarufu katika CCM, na yeye ni kama alifichuliwa kutoka kwenye kona iliyofichika ya jukwaa kubwa na pana la CCM. Kipindi kile walikuwapo magwiji katika chama cha mapinduzi ambao kwa rafu nyingi walitamani wapewe dhamana ya kupeperusha bendera ya CCM katika uchaguzi mkuu wa kwanza katika demokrasia ya vyama vingi. Kwa sauti moja CCM ilikataa hadaa na kwa kiasi msukumo wa Mwalimu Nyerere.

Mwalimu Nyerere alizunguka huku na huko akimuuza Mhe. Mkapa kwa watanzania, na nikiri kwamba heshima waliyokuwa nayo kwake ilikuwa mtaji wa kura zilizompa Mhe. Benjamin Mkapa dhamana ya kuwa Rais wa Jamhuri yetu. Kwa upande mwingine CCM ambayo tayari Mwalimu alikuwa ameshaikosoa sana kipindi kirefu cha miaka ya 90 mwanzoni kwa kupungukiwa uadilifu, lakini kwa tiketi ya ndugu Benjamin Mkapa aliyekuwa tunu ing’aayo na iliyouzwa na Mwalimu mwenyewe chama kikaponea hapo na kuvuka na ushindi.

Mheshimiwa Mkapa alifanya vizuri sana awamu yake ya kwanza ambayo iliwezesha ushindi wake katika awamu ya pili kwa maana ya uchaguzi wa mwaka 2000.

Mwaka 2005, kilichoipa CCM ushindi ilikuwa kampeni nzuri ya kisayansi na iliyochagizwa na tiketi ya ujana kama sehemu ya mabadiliko ya kirika ndani ya Chama cha Mapinduzi lakini pia hilo likiwa ni sehemu ya kiu ya watanzania kipindi kile. Wengi mtakubaliana name kwamba “ari mpya, kasi mpya na nguvu mpya” yalikuwa maneno yaliyoongeza hamasa ya ushiriki wa vijana katika kuleta mabadiliko katika CCM. Leo sio kusudio langu kujadili namna mchakato wa kumpata mgombea wa CCM mwaka 2005 lakini kusudio langu ni kuonesha katika kila uchaguzi namna ambavyo CCM imeweza kupenya ukiachilia upinzani mkali kutoka vyama vyenye mawazo mbadala nchini.

Ipo ile desturi ya Chama cha Mapinduzi kwamba akipewa mtu nafasi ya Madaraka ya Urais kwa awamu ya kwanza (miaka mitano) basi apewe pia na awamu ya pili ili akamilishe kazi aliyopewa na kutimiza miaka 10. Kwa sehemu imeonekana kuwa desturi ambayo mpaka mwaka 2010 wananchi wa kawaida walionesha kukubaliana nayo. Hili linaonekana kupotea kipindi hiki na kadri muda unavyoendelea hasa ukizingatia wapiga kura wengi kipindi hiki na mwaka 2020 watakuwa ni vijana chini ya miaka 40 ambao wengi wao wamepata elimu ya msingi mpaka kidato cha nne.

Nikiongea na wengi ya vijana hawa utawasikia wakisema “tunampa miaka mitano akiboroga toa tupa kule na tunaweka mwingine”. Huenda ile busara ya kumwachia mtu amalize na kipindi cha pili inaweza isiendelee katika chaguzi zinazofuata. Hili ni funzo kubwa la kwanza kwa CCM kwamba ile dhana kwamba wananchi watatoa dhamana kwa awamu ya pili ili kutimiza miaka 10, kwa kipindi hiki na chaguzi zinazofuata kama hatutafanya kazi ambazo zitaonekana miongoni mwa watanzania basi tujiandae kisaikolojia kushindwa.

Uchaguzi wa Mwaka 2015, kama ule wa Mwaka 1995 zinashabihiana kwa ukaribu sana. Tofauti na mwaka ule ilikuwa Naibu Waziri Mkuu Mhe. Mrema aliyehamia upinzani, mwaka 2015 ni Mawaziri Wakuu wawili, Mhe. Lowassa na Mhe. Sumaye. Mgombea wa CCM ni kama alivyokuwa Mkapa mwaka 1995, ameonekana si mjuvi wa siasa za ndani za chama hadi kufikia baadhi ya makada wa CCM kumtamka hadharani kwamba hajui siasa. Ukiacha beza beza za baadhi ya wana CCM kama ilivyokuwa kwa Mkapa, kipindi hiki aliyekuwa nuru inayong’aa na inayouzika kwa wapiga kura wa kipindi hiki si mwingine bali ni Dkt. Magufuli.

Kipindi hiki Mwalimu hayuko lakini viongozi wote wakubwa wastaafu na hasa wale ambao watanzania wanawaona wana akisi haiba ya Mwalimu Nyerere, nawazungumzia Mzee Joseph Sinde Warioba, Dkt. Salim Ahmed Salim na hata Mama Maria Nyerere wameonesha kumuunga mkono Dkt. Magufuli moja kwa moja.

Mchezo ambao CCM ilifanya ikiwemo kuwaruhusu baadhi ya makada wake waliokuwa wanautafuta urais wa kimungu chini ya Katiba ya mwaka 1977 wakavuruga mchakato wa Katiba Mpya ambao wananchi wenyewe walitoa maoni yao. Kura za CCM kipindi hiki zimepunguzwa kama sehemu ya adhabu ya kupuuza maoni ya wananchi katika mchakato wa Katiba. Nakiri kusema asingekuwa Dkt. Magufuli, CCM ilikuwa haiuziki tena. Nakiri kusema hii ndio tiketi ya mwisho. Iwapo CCM haitaamka na kuwajibika mchana na usiku hakika 2020 itatukuta nje ya Bunge na nje ya Ikulu.

Itaendelea 

Thursday, October 8, 2015

TUTOKE KWENYE “PANGO LA PLATO,” TANZANIA YA VIWANDA INAWEZEKANA



Katika gazeti la RAI  Toleo Na. 1217 la Alhamisi ya Octoba 1-7, 2015, kulikuwa na makala ya Ndugu Kennedy Masiana  yenye kichwa cha habari “Dk. Magufuli Tanzania ya Viwanda haiwezekani.” Katika makala hiyo mwandishi amefanya juhudi kubwa kuonyesha kuwa juhudi zozote za kujenga viwanda kwa Tanzania ni ndoto kwa kuwa gharama za kujenga viwanda hivyo ni kubwa kwa nchi kama Tanzania kumudu. Mwandishi anasema Rais wa Tanzania hana haja ya kujishughulisha na ndoto za kujenga viwanda kwa kuwa ni jambo lisilowezekana.  

Kwa maneno yake  mwandishi anasema, “Watanzania  wa sasa wanamtaka Rais ajaye, awe ni yule atakayeshughulika na hali zao za mashambani, hospitalini, miundombinu bora ya barabara itakayowawezesha kusafirisha mazao yao kwenda kwenye masoko.” ... “awahakikishie huduma nzuri za kijamii kama huduma ya maji safi na salama ya kunywa, elimu bora, umeme wa uhakika, lakini pia aguswe na hali yao ya umaskini wa kipato ili waweze kujikomboa kiuchumi.”

Kimantinki na kimaana maelezo ya mwandishi hapo juu yana matatizo makubwa ya aina kubwa tatu: Kwanza, maelezo haya yanaonyesha kukata tamaa na kukubali hali tuliyo nayo kuwa ndivyo ilivyo na haiwezi kubadilika. Kwa sasa serikali imekuwa ikijitahidi kufanya hayo aliyosema mwandishi.  Inaeleweka duniani kote kuwa maendeleo ya kweli yanakuja tu kwa kuwa na viwanda na kwamba sekta zingine zote zitaweza kustawi tu ikiwa tu zimefungamana na viwanda. Mfano, uzoefu wa nchi zote ambazo zimeendelea kiuchumi unaonyesha kuwa  mapinduzi ya kilimo yaliwezekana kwa kufungamana kwa sekta ya kilimo na ukuaji wa viwanda vya kuzalishaji pembejeo na kusindika mazao.

Vivyo hivyo, sekta ya huduma za elimu isiyofungamana na viwanda badala ya kuwa chanzo cha ustawi na maendeleo ya nchi inaweza kuwa chanzo cha matatizo. Kwa mfano, Tanzania sasa inazalisha wasomi wengi kila mwaka, hata hivyo kutokana na kukosekana kwa  viwanda, wasomi wetu hubaki mitaani wakiwa hawana ajira na matokeo yake baadhi yao hushawishika kujiingiza katika vitendo viovu kama vile ukahaba, ujambazi na uhalifu wa aina mbalimbali kama njia ya kujipatia kipato. Lakini tulipokuwa na viwanda katika miaka ya sabini na themanini wahitimu wetu walikuwa wanachagua kazi maana zilikuwepo za kutosha.

Hata sasa tatizo la ajira si kubwa katika nchi kama  China na Korea ambapo kuna uwekezeji wa kutosha kwenye viwanda.

Tatizo la pili la makala ni kuegemea kwenye falsafa za feki na zilizoshindwa za uchumi mamboleo. Msingi mkubwa wa falsafa hiyo ni kuwa dola haipaswi kujishughulisha na masuala ya kiuchumi kama vile viwanda. Kuingizwa kwa falsafa hii kupitia ushawishi na masharti ya wafadhili wakiongozwa na Benki ya Dunia na Shirika la Fedha Duniani (IMF)  katika miaka ya tisini ndiyo sababu kubwa iliyosababisha viwanda tulivyokuwa navyo hapa nchini kubinafsishwa kwa visingizio mbalimbali ikiwemo kutoendeshwa kwa ufanisi. Hata hivyo, baada ya kubinafsishwa viwanda vingi  kwa matumaini kuwa vingeendeshwa kwa faida na ufanisi, viwanda vingi vilikufa na kuiacha  Tanzania  bila viwanda. Hapo ndipo u-feki wa falsafa hiyo inayojinasibu kuwa sekta binafsi pekee ndiyo injini ya uchumi ilipoonekana wazi. U-feki huo ulijidhihirisha zaidi wakati wa msukosuko wa uchumi wa dunia ulioanzia Marekani mwaka 2008.

Marekani ambayo ndio kuhani mkuu wa falsafa hiyo ya kiuchumi iliamua kuachana nayo na dola kuingilia uchumi ili kuokoa makampuni makubwa yenye maslahi kwa nchi hiyo. Kwa nyongeza, hakuna nchi hata moja duniani zikiwemo zilizoendelea huko nyuma kama uingereza na ujerumani na zile zilizoendelea siku za karibuni kama China, Korea ya Kusini na Taiwani ambayo zilifanikiwa bila dola kujiingiza katika uwekezaji.  Kwa bahati mbaya, falsafa hii feki bado inafunga fikra za watu kama wale wafungwa kwenye hadithi ya pango la Plato. Katika pango hilo wafungwa walinyimwa fursa ya kuona mwanga wa jua.

Walizoea kuona vivuli vya mwanga wa jua ukipiga ukutani kupitia kwenye mlango wa pango, na kwao vivuli hivyo ndiyo ulikuwa mwanga halisi. Siku walipotolewa nje wakaonyeshwa mwanga walikataa kuwa huo siyo mwanga kwa maana kwao vile vivuli walivyozoea kuviona ndiyo mwanga wenyewe. Inabidi tufungue fikra zetu tuangalia hali halisi ya mwenendo wa kiuchumi duniani na tutaona kuwa Tanzania ya viwanda inawezekana.

Tatu, mwandishi anaonekana kutokujua chanzo halisi cha matatizo ya kiuchumi yanayoikabili Tanzania kwa sasa. Matatizo hayo ni pamoja na  ukosefu wa ajira, utegemezi wa misaada kwa bajeti yetu, umaskini uliotopea, kudorora kwa huduma za jamii kutokana na kukosekana kwa fedha za kuboresha miundombinu ya kugharamia ubora wa utoaji huduma. Chanzo kikubwa cha matatizo hayo ni kuwa na uchumi usiotosheleza mahitaji.

Hivyo, kama tutakubali maoni ya mwandishi kama yalivyonukuliwa kwenye aya ya kwanza, Tanzania itakuwa imekubali kuwa kwenye “vicious cycle of poverty” yaani  mduara wa umaskini. Kwa maana tutaendelea kuwa kwenye kilimo kisicho na tija, tutaendelea kukopa nje na kuongeza deni la Taifa ili tutoe huduma za jamii. Tutazalisha wasomi ambao wataishia mitaani na kuwa chanzo cha maovu katika jamii. Mwisho wa yote Tanzania si tu kuwa itaendelea kuwa nchi maskini na tegemezi.

Tanzania ya Viwanda anayoinadi Dk. Magufuli Inawezekana.

Hakika ujenzi wa viwanda ndiyo namna pekee ya kujikwamua kutoka katika matatizo yetu ya kiuchumi na kuhakikisha ustawi wa Tanzania ya leo na ya vizazi vijavyo. Bahati nzuri Dk. Magufuli ameeleza ni namna gani atatekeleza azma yake ya kuleta mapinduzi ya viwanda Tanzania ikiwa tutampa ridhaa ya kuwa Rais wetu.

Kwanza, serikali inaweza ikajenga viwanda vya aina mbalimbali nchini kwa kuweka sera nzuri zinazovutia wawekezaji watakojenga viwanda katika maeneo ya kimkakati na kipaumbele kwa nchi.  Bahati nzuri hapa Tanzania tunayo mifano hai kupitia  kujengwa kwa kiwanda cha Dangote (Dangote Industries Limited Tanzania [DIL]),  moja ya viwanda vikubwa vya kuzalisha sementi barani Afrika,  mkoani Mtwara. Kiwanda hiki kimeajiri zaidi ya Watanzania elfu kumi. Serikali pia inapata mapato ya kodi mbalimbali kutoka kwenye kiwanda hicho na kutoka kwa wafanyakazi wa kiwanda hicho. Pia,  Watanzania wengi wameajiriwa na wanauza mazao yao kwa viwanda vya mwekezaji mzawa,  Azam Bakhresa Group of Companies. Dk.Magufuli ameahidi kuwa  moja ya sera zake za kiuchumi ni kuweka mazingira rafiki kwa wawekezaji  wa ndani na nje kuwekeza katika  sekta ya viwanda nchini. Bahati nzuri serikali imeshatenga maeneo maalum ya kiuchumi kule Bagamoyo, Mtwara na Kigoma. Atakachohitaji kufanya Dk.Magufuli ni kuongeza maeneo maalum ya viwanda na kuweka miundombinu muhimu kwa ajili kuleta ufanisi katika shughuli za viwanda katika maeneo hayo. 

Pili, Serikali inaweza kuingia ubia na wawekezaji binafsi kupitia kile kinachojulikana siku hizi kama (Public Private Partnership[PPP]) yaani, ubia kati ya sekta binafsi na sekta ya umma. Kwa taarifa tu viwanda vikubwa katika nchi mbalimbali kama China, Korea, Ujerumani vimeundwa kwa mtindo huo.

Tatu, serikali inaweza ikajenga yenyewe viwanda hasa kwenye maeneo ya kimkakati kwa maslahi ya nchi hasa viwanda vikubwa. Hapa inabidi tuelewe kuwa siyo lazima kuwa na fedha taslimu kama mwandishi alivyoashiria. Kama ilivyo kwa wawekezaji wengine wakubwa, serikali inaweza kukopa mtaji kwa ajili ya kugharamikia uanzishwaji wa viwanda husika. Jambo la msingi ni kufanya upembuzi yakinifu na kuonyesha namna kiwanda kitavyotengeneza faida na kulipa deni. Ukopaji huu ni tofauti na ukopaji ambao tunaufanya kugharamia huduma za jamii badala ya sekta za uzalishaji. Tukiwa na viwanda vinavyofanya kazi kwa faida, Watanzania watapata ajira, tutaondoa utegemezi na kuondoa umaskini. 

Nne, kama alivyobainisha Dk.Magufuli, serikali inaweza ikaanzisha mitaji maalum yaani “venture capital” kwa ajili ya maendeleo ya teknolojia inayohitajika kwa viwanda. Mitaji hii inaweza kupatikana kwa njia mbalimbali kama vile  serikali kukopa, kuingia ubia na wawekezaji, ama kutoka kwenye hazina ya nchi. Mitaji hii kwa kawaida siyo mikubwa lakini ni kichocheo kikubwa katika maendeleo ya teknolojia hasa ya mawasiliano. Ni kwa njia hii ndio viwanda vingi vimechipuka kutoka katika eneo lijulikanalo kama “Silicon Valley” huko Marekani. Hapa ndipo makampuni makubwa ya kiteknolojia kama vile Apple inayozalisha simu za Iphone ilipozaliwa.

Kwa ufupi, hakuna nchi ambayo imeweza kujikomboa katika umaskini na kujiletea maendeleo bila ya kuwa na viwanda. Tanzania haiwezi kukwepa ukweli huo ikiwa inataka kuondokana na mnyororo wa umaskini na matatizo ya kiuchumi yaliyopo.  Tanzania ya viwanda inawezekana tukiweza kuwa na uongozi wenye dira na mikakati dhabiti ya kutufikisha huko.


Na hapa Dk.Magufuli amejipambanua kuwa ana dira na uwezo wa kuleta mapinduzi ya viwanda Tanzania.  

Sunday, October 4, 2015

UCHAGUZI WA MWAKA HUU NI WAADILIFU NA WAZALENDO V/S GENGE LA WAHUNI “CARTEL” NA WASAKA MADARAKA KWA MANUFAA BINAFSI


Kwa muda mrefu kikundi cha wahuni kilijaribu na kufanikiwa kupoka madaraka ndani ya Chama cha Mapinduzi. Watu hawa walitaka kujijengea "cartel" ya kuongoza nchi, humo walikuwemo watu kadhaa na hasa wafanyabiashara akiwemo Lowassa na yeye ndiye alikuwa Msanifu wa genge hilo na hasa ili kutimiza ndoto yake ya kuwa Rais hata kwa kuununua Urais wa nchi yetu, alifanya hivyo mwaka 1995 akashindwa maana Mwalimu alikuwepo. Baada ya hapo genge hili lilijiposition kwenye maeneo yote nyeti ya nchi yetu.

Mwaka huu wana CCM tumekataa upumbavu huu wa kudhani Urais na Uongozi unaweza kununuliwa kama nyanya. Tumekataa na tumehakikisha katika ile "CARTEL" au GENGE la WAHUNI hakuna kati yao ambaye anaiona IKULU kwa tiketi ya CCM. Imewauma sana, Huyu bosi ndio kaenda UKAWA na wako waliobaki CCM, tutashughulika nao strategically, lakini kwanza ni lazima tupate Rais Mwadilifu KWANZA ambaye atatusaidia kazi ya Pili ya Kusafisha UFISADI. kazi ya Kwanza imekuwa kuwanyima Dhamana ya Urais kupitia CCM.

Hapa CCM wanapaswa kwakweli kujitoa kimasomaso. GENGE sasa limehamishia mapambano kutoka Kambi ya Upinzani. Utagundua hoja ya UFISADI ilishamiri sana na ndio maana kipindi fulani UKAWA waliunga Mkono kazi yetu ya Katiba ambayo lengo lake lilikuwa kuja kuua CARTEL au GENGE la WAHUNI, leo UKAWA hawana tena uhalali (legitimacy) ya kukemea UFISADI maana UFISADI umetamalaki kati na juu yao.

Hebu tafakari mtu kama ndugu yangu na kaka yangu Saeed Kubenea kwa kazi yooote aliyofanya miaka nenda rudi mpaka akashambuliwa, juzi alijisikiaje pale kawe aliponyooshwa mkono juu na Edward Lowassa? Dhamira yake ilimweleza nini? Na Lowassa hakusita kumpiga kijembe kwamba huyu alikuwa machachari sana kwenye Media sasa apunguze, hivi Kubenea amejiuliza Lowassa alimaanisha apunguze nini na kwa faida ya nani.?

Mimi mpaka TV mbili kubwa zimekataa nisikaribishwe kwenda kwenye vipindi kwa maelekezo ya wamiliki. Je kukataliwa kwangu ni kwa faida ya nani? Mbona kama ni siasa kila siku kwenye TV hizo wadau wa UKAWA wanajimwaga vilivyo, je mimi tatizo langu ni nini? Wengine walifurahia TCRA kutoa tamko la kukataza watu kwenda kwenye vipindi vya moja kwa moja, na wengi walisema mitandaoni wamenikomesha mimi, hivi mimi nikikomeshwa ni kwa faida ya nani?

TCRA walilazimisha kwamba ili uruhusiwe kushiriki kwenye vipindi vya moja kwa moja ni lazima uwe mwakilishi wa vyama vya siasa. Mimi nikasema kwa hakika ningemwambia ndugu Kinana Katibu Mkuu wa CCM angenipa barua ili niendelee kushiriki. Lakini nikasema hivi wanaoruhusiwa kushiriki ni wanasiasa peke yake? Je uchaguzi ni haki uhodhiwe na wanasiasa pekee? Nikaendelea kujiuliza hivi uchaguzi mkuu wanaotakiwa kujadiliana zaidi ni Wananchi wanaochagua ili kutoa dhamana au wale wanaoomba kuchaguliwa ili kupewa dhamana? Nikasema mbona Katiba inasema kuna Uhuru wa kuweka mawazo hadharani je mawazo hayo yako limited wamakati wa uchaguzi?

Nikafunga safari kwenda TCRA nikawauliza maswali hayo na namshukuru Mungu aliwapa busara kubwa na baadaye walitoa tamko kubatilisha katazo lao la awali. Lakini nikajiuliza zaidi kwanini hata wale wadau wa asasi za kiraia hawakuoneshwa kukasirishwa na kitendo kile cha TCRA? Nikasema hata watu wote wakisimama mimi nitaendelea kudai haki na kweli katika nchi yangu.

Leo siwezi kwenda kwenye TV mbili kubwa na wamiliki wameweka msimamo, kwanini? Wale wanaofurahia mimi kukataliwa je wanapata faida gani.? Mbona mimi nikionana na vijana na wadogo zangu ambao wako katika vyama vya upinzani nawapa moyo na kuwaambia watende sawasawa na dhamira zao njema na kwamba walitizame Taifa kwanza? Najiuliza je Tatizo langu ni nini? Au sijitambui? Au niko naïve?

Nitasema kweli Daima na fitina kwangu mwiko na nitatumia elimu yangu kwa manufaa ya Wananchi wa Taifa langu. Kwanini leo baadhi ya watu wamenigeuka, watu ambao walifurahia nilipowaambia pale Ubungo plaza na pale Mlimani city kwamba maslahi binafsi yanahatarisha mustakabali wa Taifa letu. Nilikwenda mbali na kuwataja watu hao na watanzania baadhi na wengi wakanifurahi sana. Mbona leo naendelea kuwasema watu wale wale na baadhi ya watanzania wananiona nimegeuka? Kwanini waliniamini kipindi kile na wakijua mimi ni CCM na nilikuwa nawasema CCM na leo Mimi nikiwa bado CCM nawasema watu ambao wanataka kutununua ili waendeleze GENGE la KIHUNI mbona watu wanaema mimi ni kigeugeu? Naendelea kutafakari.

Siku moja nilikaa na viongozi wawili wa CCM, mmoja akasema nadhani mchakato wa Katiba ni lazima kabla ya kura ya maoni tujenge muafaka na kufanya maridhiano ili kila sauti ya Mtanzania isikilizwe. Kiongozi mwenzake mdogo kidogo kwa cheo akabisha sana na akasema ni lazima twende kwenye kura ya maoni kwasababu tendo la Katiba kwa lilipofika ni kama maji yanayomwaga kutoka katika bilauli kwamba ni lazima yafike chini.

Nikamtazama na kumkazia macho na nikamweleza wacha na mimi nizungumze kama mwana CCM. Nikawaomba niwaeleze historia ndogo ya namna nipo nilipo. Nikasema nianzie kwenye Katiba, nikawaambia unajua mimi nilikuja Tume ya Katiba nikiwa simfahamu mtu yeyote isipokuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano? Nikawaeleza mimi sikumfahamu Mzee Warioba, Jaji Ramadhani, Mzee Butiku, Dkt. Salimu wala Profesa Kabudi na wengineo, sikumfahamu hata mmoja. Nilikuwa namfahamu Rais Kikwete tu. Alipotupa kazi na akatuagiza tuwasikilize watanzania na watakachosema ndicho ambacho tukiandike, tulifanya hivyo kwa unyenyekevu mkubwa kwa watanzania.

Hata pale ambapo Rais alionekana kutoka na msimamo tofauti na wetu nilibaki kuwaambia watanzania kwamba Tanzania njema itajengwa na watanzania wenyewe. Hatukuishia pale tuliokuwa wajumbe wa Tume ya Katiba tulifanya utafiti kwa kuzungumza na wadau mbalimbali, wabunge, viongozi wastaafu, watu mashuhuri ili kuelewa tatizo lilikuwa wapi.

Utafiti huu wa chini chini ulinipa fursa ya kuonana na wabunge wengi wa CCM na wa upinzani na wote walikiri kwamba “Bwana Mkubwa amekataa” na tulipozidi kuhoji hoji tulikuja kukutana na wapambe wake kwanza ambao walisema “tatizo lenu mmedhoofisha Urais na kwamba Kikwete anataka kuondoka ameweka masharti na kanuni ngumu za uongozi hilo haliwezekani” wakaendelea kusema “yeye (Kikwete) aende na sisi tubaki na madaraka yale yale au zaidi na tuwe na mamlaka kama aliyonayo sasa katika nchi”.

Wapambe hawa tulizungumza nao kwa maana ya kuwapa elimu ya Rasimu ya Katiba na wakawa wanatuuliza “kwahiyo ninyi (Tume ya Katiba) mnashauri ‘Mkubwa’ achukue Urais wa Tanzania au Urais wa Tanganyika?” Tukasema achukue ya Muungano, wakasema “je itahusisha madini, gesi na ardhi”? Tukasema hapana, wakaendelea kuuliza “je akichukua ya Tanganyika atakuwa na uwezo wa kusafiri nje ya nchi kama Rais Kikwete na kupigiwa mizinga 21”? Tukasema hapana, mmoja wao akasema “anhaaa hapo ndio mnapokosea, sisi tunataka zote za Tanganyika na Muungano ziwe pamoja”, kwa kusema hivyo walikuwa wanamaanisha serikali mbili.

Hatukuchoka tukafanya utaratibu na tukaenda kumuona “Bwana Mkubwa” yaani Edward Lowassa, tulikutania ofisini kwake mikocheni. Ili kuweka uwazi katika mkutano ule tulijumuisha pia wawakilishi watatu wa Asasi za Kiraia na Makamishna Wawili, mimi nikiwa mmojawapo, tulikuwa na kikao ambacho hakikupungua saa mbili.

Ni katika kikao kile nilithibitisha kwamba aliyebuni mkakati wa kuikataa Rasimu ya Warioba kwa CCM alikuwa Edward Lowassa tena akaonesha kufurahishwa na Rais Kikwete kama Mwenyekiti wa Chama kuzomewa na hatimaye Rasimu aliyoipeleka katika Chama kukataliwa. Nilijuliza sana mimi kama Kiongozi kijana, tafsiri yake ni nini? Huyu ni mwana CCM na anafurahia Mwenyekiti wake kudhihakiwa na kutupiwa Rasimu yake katika kikao. Leo najiuliza kama alikuwa na dhamira ya kuikubali rasimu ya Warioba kwanini alikaa kimya wakati Mwenyekiti wake akidhihakiwa?

Nikawaeleza iliyokuwa Tume ya Katiba iliwahi kumwita hata mzee Kingunge aje tujadiliane kuhusu Rasimu ya Warioba na alipokuja aliwatukana wajumbe wa Tume pamoja wageni wengine waalikwa akiwemo Profesa Sherrif kutoka Zanzibar, nilipoona anamwunga mkono Lowassa sasa namwelewa na ndio maana katika mkutano wa Taasisi ya Mwalimu Nyerere nilidiriki kusema Mungu akinipa umri mrefu na kufikia uzee namwomba Mungu nisiwe kama wao.

Nikamwambia yule Kiongozi mdogo, unadhani ni kazi rahisi mimi kama kijana mdogo kusimama kidete kutetea maoni ya Wananchi? Nilijua aliyekuwa na maslahi katika kutupilia maoni ya Wananchi hakuwa Kikwete bali Edward Lowassa ambaye amekuwa akiutafuta Urais wa kifalme. Kuthibitisha hilo nilimtamka kwa jina mara kadhaa Ndugu Edward Lowassa kwamba hafai kuwa Rais wa Tanzania.

Na kwangu mimi nilikuwa najiuliza hata kupitia CCM ambako mimi ni mwanachama, iweje mtu ambaye anakosa kuheshimu watanzania wanapotoa maoni yao ya Katiba akawa ni mtu ambaye atasimama ili wampe dhamana ya kuwa Rais wao. Mimi nilimkataa tangu CCM na nilipoona CCM kama vile wanachelewa, mimi (Polepole), Mzee Butiku na Mzee Warioba tulifanya mdahalo na tukaweka msimamo kama Lowassa atapewa tiketi ya kugombea Urais kupitia CCM basi sisi watatu tusingejitoa bali tungepiga kampeni ya kusema CCM isichaguliwe.

Nikaendelea kumwambia hili la Katiba Mbaya wake namjua na alijaribu kuhonga watu, ni lazima tujenge muafaka wa kitaifa kwanza. Namshukuru Mungu Kiongozi Yule ni muelewa akasema muafaka ni kitu muhimu, hilo linawezekana na ni kwa maslahi ya watanzania wote sema tu kipindi kile kiligubikwa na ushindani wa kisiasa, ila sasa ni muhimu tukaja pamoja kama Taifa. (Mwisho wa kunukuu kikao change na viongozi wa CCM)

Uhalisia huu ndio umefanya Mzee Joseph Sinde Warioba kupiga kampeni ya Chama cha Mapinduzi. Ila kitu kimoja napenda kuwaeleza kuna maadui ndani ya CCM na nje ya CCM na hasa hasa wale ambao wako chini ya “cartel” au lile GENGE la WAHUNI ambalo linafanya kila jitihada ili Mgombea wa CCM asiye na makundi na asiye na msalie mtume na wezi, wabadhirifu na mafisadi. Maadui hawa wako radhi Mwana Mtandao mwenzao (aliyeondoka CCM na kwenda UKAWA) apewe dhamana ya Urais wa nchi yetu ili waendelee kutunyonya kwa maslahi yao.

Ikumbukwe UKAWA huu sio UKAWA ule ambao mimi na Mzee Butiku na Mzee Warioba tulifanya nao kazi pamoja, si hawa. Hawa UKAWA wa sasa ni watu wenye uchu wa ajabu wa madaraka na kwamba wako tayari kumtumia mtu mwenye nasaba zote na ufisadi ili awafikishe ikulu.

Kama ni masikini na nikaambiwa mwabudu shetani ili niwe tajiri, nitakataa na kutunza utu wangu kama ambavyo Bwana Yesu alikataa kumwabudia shetani kwa sababu hizohizo.

Hivi sielewi hawa wanachama wa Chadema ambao wamekubali kumeza matapishi yao wenyewe, wanapataje amani mioyoni mwao wanapojua mgombea Urais wao ndio Yule mtu waliyesema ni fisadi kwa zaidi ya miaka 8. John Mnyika alisema anao ushahidi wa UFISADI wa Lowassa, Mbowe alisema anashangaa vibaka wanachomwa moto na Lowassa ameachwa anadunda mtaani, Mchungaji Msingwa aliyesema anayemkubali Lowassa akapimwe akili na Godbless Lemay eye amekuwa kimya kidogo ila naye amesema ni halali kumtupia jiwe fisadi lowassa. Hawa leo wanapataje uthubutu wa kusimama katika jukwaa moja na Lowassa na tena wakainuliwa mikono akiwanadi.

Mimi nilijiapiza wale waliokataa maoni ya Wananchi sitaki urafiki nao hata leo, na Lowassa ni mfano mmoja. Na niko tayari kuendelea kuunga mkono mabadiliko chanya yaliyofanywa na Chama cha Mapinduzi (CCM) kwa kuuvunja na kuwanyima Urais kupitia CCM. Hii ndio CCM ya kweli, CCM ya wakulima na wafanyakazi, CCM inayochukia rushwa katika uongozi na sasa tumeanza na Urais na baada ya Urais tutawashukuia wabaya wote waliosalia. CCM ambayo haishurutishwi na matajiri wanaotaka kututengenezea viongozi ikiwemo nafasi ya Urais.


ITAENDELEA

Thursday, October 1, 2015

“HASIRA HASARA”: KUPIGA KURA KWA HASIRA NI UJUHA NA SI HEKIMA, TUPIGE KURA TUKILITIZAMA TAIFA


Utamaduni wa kukosa uhimilivu umetoka wapi?

Bado nimepigwa na butwaa kwa namna ambavyo baadhi ya watanzania wenzangu wanakosa ustahimilivu katika kipindi tunapoelekea uchaguzi mkuu. Nimegundua kwamba unapotoa hoja ambayo wengine hawaiungi mkono basi kumekuwa na ugumu katika kustahimiliana. Nashangazwa zaidi pia pale ambapo hata wale ambao ni wana mageuzi au wafuasi wa vyama vyenye mawazo mbadala, hawa wamekuwa wakali kweli pale mtu anapotoa hoja ambazo hazifanani na mitizamo yao.

Nimeanza kuona dalili ya Taifa kuanza kupoteza utamaduni wa ustahimilivu, utamaduni wa kuheshimiana, utamaduni wa kujadiliana kwa hoja na sababu na utamaduni wa mijadala inayojengwa katika dhana ya nguvu ya hoja na si hoja ya nguvu. Kwa wale ambao ni wafuatiliaji wa mitandao ya kijamii utagundua kwa sasa kuna mgombea ukimjadili ni tatizo, au ukimjadili mmoja bila kumgusa mwingine ni tatizo kubwa.

Jamii yetu imegeuka kuwa kama genge litishalo na kuamulia watu wazungumze nini, kwa nani na wakati gani. Ni katika kipindi hiki na ajabu kabisa baadhi ya wananchi wamekuwa wakilazimisha wananchi wengine na hasa wale wanaopenda kuweka mawazo yao hadharani kwamba ni lazima wawe katikati. Hivi kuwa katikati unapotoa hoja maana yake nini? Mtoa hoja mmoja ambaye pia ni kiongozi wa dini aliwahi kuniasa kuwa ninapojenga hoja niwe katikati au “neutral” na pasina kuainisha nani mbaya na nani mzuri. Nikamwuliza, je katika kazi ya kuhubiri dini, kuna siku amewahi kumtendea haki shetani anapohubiri na kwa maana ya kusema shetani naye ni mzuri kwasababu watu wengi pia wananufaika naye? Au wakati wote yeye huhubiri na kumtukuza Mungu wa Mbinguni pekee kwa yeye ndiye mwema na mtenda mema yote na wema wote huyoka kwako na Shetani au Ibilisi ni mwizi, muuaji na mharibifu na kwake hakuna wema bali ubaya wote.

Je kama mimi ni muumini wa kusimamia kweli na uadilifu, dhambi iko wapi iwapo nitasema katika wagombea Urais mtizamo wangu ni kwamba mgombea fulani kwa vigezo vya kibinadamu yuko vizuri na mgombea fulani kwa vigezo vya kibinadamu namwona sio mwadilifu na ana uchu wa madaraka na anadhani yeye aliandikiwa Urais na Mungu.

Ninaendelea kuuliza hasira iko wapi kama nitatumia uhuru wangu kumjadili mgombea mmoja ambaye kwa ushahidi nafahamu hana sifa ya uadilifu na ananasibishwa na ufisadi kwa zaidi ya miongo miwili?

Labda nieleze kwa sehemu, mimi ni mwana CCM na wakati wa Mchakato wa Katiba nakumbuka watu wote waliotukwamisha na walikuwa katika makundi mawili, kundi la kwanza lilikuwa watu na hasa mtu aliyekuwa hapendi maoni ya wananchi na katika namna yalikuwa yatumike kuandika Katiba Mpya. Mtu huyu anajulikana wazi kwamba alijipambanua kama mgombea pekee na mwenye hatimiliki ya Urais kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM). Mtu huyu mimi na wenzangu tulikuwa na kikao naye cha zaidi ya saa mbili nikimfafanulia Rasimu ya Warioba na faida zake, akakataa katakata. Mtu huyu tuliamua kwenda kumwona baada ya kuambiwa na wapambe wake kwamba Rasimu ya Warioba asingeruhusu ipite na kwamba kaweka mguu chini hivyo labda tukajaribu kumfafanulia, tulifanya hivyo, nilikuwepo na alikataa mbele ya macho yangu na akatupa mapendekezo ambayo ndio hatimaye yalikuwa katika Katiba Inayopendekezwa mwishoni.

Binafsi sikukubaliana naye pale na baada ya pale na nikajiapiza kuendelea kudai maoni ya wananchi nikitumia mbinu zote halali. Itakumbukwa nilipopata mwaliko katika vipindi vya Televisheni nilipata kusema mtu huyu kama “tatizo kubwa la kitaifa” na wenzake wengine hawapaswi kupewa dhamana ya kugombea Urais kupitia CCM. Watu wengi waliniunga mkono wakiwemo wafuasi wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA), nakumbuka mdahalo wa Taasisi ya Mwalimu Nyerere na baada ya kuona kwamba mtu huyu alikuwa kana kwamba anakwenda kufanikiwa kuwahadaa watoa maamuzi wa CCM nikasema pamoja na Mzee Butiku na Mzee Warioba kwamba kama mtu huyu na wenzake watapewa dhamana ya kugombea kupitia CCM basi sisi tusingeondoka CCM ila tungesema CCM isichaguliwe.

Na labda niwarudishe nyuma kidogo, kipindi chote cha mchakato wa Katiba sote tulimjua mtu aliyekuwa anatukwamisha, kwa hakika tulimjua kwa jina na sote tuliamini yeye na watu wa aina yake hawapaswi kupewa uongozi ndani au nje ya CCM. UKAWA walijua hili na tulikuwa pamoja. Hata pale tuliposema CCM ikimpa nafasi tungezunguka nchi nzima kusema CCM isichaguliwe, UKAWA walituelewa sana. Ninapata msongo wa mawazo baada ya CCM kusikia kilio cha wananchi, UKAWA na wana CCM wenye mapenzi mema na CCM na hatimaye kumnyima dhamana ya kugombea kupitia CCM na baadaye kwenda UKAWA, iweje tena UKAWA wale wale tulihangaika nao pamoja wageuke kauli na kusema yuleyule ni jemadari? Nashindwa kumuelewa Mhe. Mbatia, huyu namtaja kwa jina ili anisaidie kujua hivi kwa ukigeugeu huu mkubwa, je wanastahili kupewa dhamana na watanzania kama UKAWA?

Leo watu wale wale walioniunga mkono kusema watu wenye nasaba na ufisadi hawapaswi kupewa nafasi za madaraka na hasa nafasi ya madaraka ya Urais wa Jamhuri yetu, ndio hao wananisema kwamba niache kumsema mtu yuleyule ambaye alitusumbua sote, mimi nikiwemo na hata viongozi wa UKAWA zaidi na wanajua tangu alipokuwa CCM.

Watu wengine wataniambia kwamba hiyo ndio siasa, na mimi kwa unyenyekevu mkubwa nasema siamini katika siasa chafu, siasa inayokumbatia wezi, siasa inayopinda ukweli, siasa inayoendeshwa kwa fedha na hata Hayati Mwalimu Nyerere alituasa kwamba ili nchi hii iendelee inahitaji siasa safi na uongozi bora na akatuasa zaidi kwamba Rushwa ni adui wa haki na Utajiri unaotumika kununua watu ili kupata madaraka ni kama na ukoma. Nimekataa kuwa sehemu ya watu hao, ninaendelea na kiapo change kwamba mtu huyu hastahili kupewa dhamana yoyote katika nchi yetu hata kama nitabaki peke yangu ila najua iko siku nikiwa nimetangulia mbele ya haki ukweli utakuja kujulikana na roho yangu itapoa hukohuko mbele ya haki.


Tusisukumwe na Hasira

Mara zote maamuzi wanayofanywa kwa msukumo wa hasira huwa aidha na tija kidogo sana ama huleta hasara kwa watu binafsi na jamii kwa ujumla. Wahenga walikwishasema “Hasira Hasara”. Ni muhimu sana kutafakari busara hizi za wahenga kipindi hiki ambacho Watanzania tunajiandaa kufanya maamuzi ya kikatiba ya kuwachagua viongozi watakaotuongoza kwa kipindi cha miaka mitano ijayo. Huu ni wakati muafaka kwa Watanzania kutafakari ni nani hasa anaefaa kupewa dhamana ya kuiongoza Tanzania kwa manufaa ya Watanzania.

Kwa bahati mbaya sana katika kipindi hiki kueleke Uchanguzi Mkuu wa Oktoba 2015, kumeibuka wimbi la siasa na propaganda zinazopandikiza chuki na kuchochea  hasira miongoni mwa Watanzania. Watu hawa kwa kuelewa vyema athari za chuki na hasira hawapendi kutoa fursa kwa Watanzania kutathimini kwa kina matatizo na mafanikio yetu.

Kutokana uchu wa madaraka na nia ya kutimiza ndoto zao za kushika dola, wanaochochea hasira na chuki, wanaminya nafasi ya wapiga kura kupima uwezo na dhamira ya wagombea katika kutatua matatizo ya kimaendeleo na kuendeleza ama kupanua wigo wa mafanikio na ustawi wa Watanzania. Ni muhimu pia kutambua bayana kuwa katika kinyanga’nyiro cha kutaka kutaka madaraka wanasiasa wengi kama sio wote huweka nguvu nyingi katika ushawishi unaolenga kujenga matumaini kwa wananchi ili mradi tu wapate kura. Ni wajibu wa Watanzania kuhoji na kupima uhalisia wa yale tunayoahidiwa na wagombea kwa kutafakari pasipo chuki wala hasira zinazopandikizwa na wanasiasa.   

Ni vyema tukumbuke kwamba katika hali ya hasira na chuki kuna hatari ya  kutosikiliza na kuhoji kwa makini wagombea wote wa uraisi, ubunge na udiwani ili kupima uwezo, weledi, uadilifu na uzoefu wao katika kutekeleza yale wanayoahidi katika sera  na vyama vyao. Maswali ya kujiuliza ni pamoja na Je kuna tija gani kumchagua mgombea fulani? Je mgombea husika anao uwezo, weledi na uzoefu katika kutekeleza yale anayoahidi? Je mgombea ni mwadilifu na anaweza kudiriki kukemea ufisadi? Je mgombea anaamini katika mfumo wa uzalishaji mali unaotoa fursa sawa kwa watanzania wote? Je mgombea na chama chake wanamipango na nia thabiti ya kuondoa kero mbalimbali za wananchi?

Kwa maslahi mapana ya nchi yetu kamwe tusikubali kutumiwa kukamilisha ndoto za watu wachache. Tuwaulize maswali sahihi ili kama hawana majibu sahihi tuwakatae kwa mujibu wa tathimini yetu juu ya sera na hoja zao. Tunafahamu wazi kuwa wagombea wengi wanaahidi mabadiliko ni jambo jema lakini tuwaulize uhalisia na uhakika wa ahadi zao.

Lakini pia wagombea na vyama vyao watueleze bayana tutanufaikaje na nini athari za muda mfupi na mrefu zinazoambatana na mabadiliko hayo. Mwisho ni vyema tutambue   kuwa hatuwezi kupata viongozi wenye nia thabiti ya kuleta maendeleo kwa kupiga kura za hasira na chuki zinazochochewa na watu wachache wanaotaka kutimiza malengo yao binafsi. Kila tunapowasikiliza wagombea na vyama wakinadi sera zao tuanze sasa kujenga utamaduni wa tuzitafakari na kuzipima hoja zao ili kufanya maamuzi ya busara kupitia sanduku la kura ifikapo tarehe 25 Oktoba 2015.

Friday, September 11, 2015

DR. JOHN POMBE MAGUFULI NA UWEZO WAKE WA KULETA MABADILIKO CHANYA



Tujadiliane kwa HOJA na Sababu

Kuelekea uchaguzi Mkuu 2015  mabadiliko ni miongoni mwa mambo yanayochukua nafasi kubwa katika kampeni na ilani za vyama vya siasa. Hoja nyingi zinatolewa hususani katika dhana ya mabadiliko ya mfumo au kiongozi au yote mawili yaani mfumo na uongozi. Kwa bahati mbaya watanzania hawaelezwi mahusiano kati ya mfumo na viongozi. Mbaya zaidi wengi wetu tumeporwa uwezo wa kutafakari kutokana na kuzamishwa kwenye mahaba kwa wagombea au vyama vya siasa.

Kwa kuwa bado kuna siku zaidi ya arobaini ni vyema tukawatafakari baadhi ya wagombea wa nafasi ya uraisi ambao ndio hasa wanachuana vikali katika kampeni zinazoendelea.  Yapo mambo kadhaa yanayoweza kutuongoza katika kuwapima wagombea na sera zao. Moja, ni kutafakari kama inatosha kuwa mashabiki wa matamko tu yenye kushawishi juu ya kuleta mabadiliko  kama ambavyo baadhi ya wanasiasa wameendelea kuwalaghai wananchi kipindi hiki cha kampeni za uchanguzi mkuu 2015.

Muhimu sana ni  kupima nia na zaidi sana uwezo wa  kiongozi husika kutafsiri madhui ya ahadi zake katika vitendo.  Hasa kwa kuzingatia ukweli kwamba  wameibuka wanasiasa wanaotoa matumaini hewa kwa wananchi kwa kusema tu yale ambayo wananchi wangependa kusikia. Ni jambo jema kuwajengea wananchi matumaini lakini ni hatari pia kuwalaghai wananchi kwa mambo ambayo kiongozi husika sio tu yeye mwenyewe hayaamini au hana uwezo wala dhamira ya dhati kutimiza. Maswali mawili ni muhimu kuulizwa katika hili, moja ni mfumo gani unaolengwa kubadilishwa ili kuleta mabadiliko ya kweli kwa watanzania? Je viongozi husika wanavyo vigezo, uwezo  na uzoefu katika kujenga mifumo endelevu?

Edward Lowasa na dhana ya mabadiliko ndani ya UKAWA

Tukianza  na kambi  ya UKAWA inayowakilishwa na Edward Lowasa, tukivipima vyama vya siasa vinavyounda UKAWA kwa mifano na kutafuta vielelezo vya kimfumo inaonekana  dhahiri kuwa  aidha hakuna kabisa mifumo bali haiba (personalities)  au kuna baadhi ya viashiria vya kuwepo kwa mfumo lakini kutoka na kujengwa kwenye misingi dhaifu mifumo hii imekuwa sio endelevu. Pengine kwa kutambua udhaifu huu UKAWA imefungua milango kupokea baadhi ya  wanasiasa ambao wamewahi kuongoza nchi yetu katika nafasi kubwa za uongozi kama ile ya Waziri Mkuu. Hawa ni pamoja na Edward Lowasa ambae ndio mgombe uraisi na Fredrick Sumaye .

Hata hivyo  ukiwauliza au hata ukijaribu kutafuta na kupima jambo gani la kimfumo waliwezakulifanya katika nafasi zao?  Kinachojitokeza ni aidha viongozi hawa hawakuwa na uelewa sahihi wa masuala ya kimfumo hivyo kushindwa kufanya uchambuzi sahihi wa matatizo ya kimfumo na kuyapatia majawabu ya kiutendaji. Mara nyingine  walidandia miradi ya maendeleo na kuisukuma kwa mabavu bila kuweka misingi ya kimkakati ikiwa ni pamoja na kujenga  taasisi imara  kutekeleza na kusimamia sekta husika mambo hayo licha ya kuwa mazuri yaligeuka kusongwa na changamoto nyingi.

Mbaya zaidi viongozi hawa na wengine wanaofanana nao walitumia nafasi zao kujinufaisha wenyewe ikiwa ni pamoja na kujenga mitandao ya kukwapua fedha za umma kwa maslahi yao binafsi na washirika wao. Kinachopaswa kuogopwa sana na Watanzania ni ile hulka ya viongozi hawa kutaka kujilimbikizia mali kwa namna yeyote ile. Hawa ni miongoni mwa viongozi  ambao wamediliki hata kusema kuwa wakichaguliwa kuongoza nchi hii watatengeneza kundi la aina  fulani ya matajiri ambao wataendesha uchumi wa taifa letu.

Swali la kujiuliza ni kama huu ni mkakati wa kimfumo na je haya ndio mabadiliko ambayo Watanzania watarajie? Hii ni dhana hatari inayolenga kuchochea kuongezeka kwa tabaka la maskini na matajiri. Ni muhimu kutambua kuwa matajiri kazi yao kubwa ni kutengeneza faida kutokana na mitaji yao. Haishangazi kuona kuwa matajiri hawa wanaotajwa na mmoja wa wagombea wa uraisi kuwa ni “marafiki” zake wamekuwa wakifadhili harakati za mgombea huyo kuingia madarakani kwa zaidi ya miaka kumi iliyopita. Jambo jingine la kujiuliza ni Je kwa uwekezaji huu matajiri hawa wanatarajia kuvuna nini? Wasiwasi wangu ni kwamba chondechode mgombea huyu asijekuwa ameweka rehani rasilimali za nchi hii na ikiwa ni pamoja na maisha ya watanzania ili tu atimize ndoto yake ya kuwa raisi wa inchi.

Rai yangu ni kwamba Watanzania tufungue fahamu zetu kipindi hiki cha kampeni na kupima wagombea na hoja  zao pasipo ushabiki na ushawishi mwepesi. Naelewa vyema haja ya kufanya mabadiliko lakini tujiulize ni mabadiliko ya aina gani tunahitaji. Haifai kabisa kumkubali mgombea hana kabisa vigezo vya kuleta mabadiliko eti tu kwa sababu tunataka mabadiliko. Mgombea ambae hana uwezo wala uthubutu wa kukemea ufisadi  hatufai kabisa hasa kwa kuzingatia hulka za kifisadi ambazo zimeshamiri katika jamii yetu sio tu kwenye sekta ya umma bali hata sekta binafsi. Ni nani asiefahamu kuwa ufisadi uwe mkubwa au mdogo ni kikwazo kikubwa katika maendeleo na ustawi ya nchi yetu.

Je ni mara ngapi tumesikia mgombea uraisi kupitia CHADEMA na UKAWA akiweka bayana  mkakati wa kupambana na ufisadi? Ni nani asietambua kuwa ajenda ya mapambano dhidi ya ufisadi ndio iliyowafanya wananchi wengi kuvutiwa na sera za CHADEMA hususani chini ya Uongozi wa Katibu Mkuu wa zamani wa chama hicho Dr. Wilbroad Slaa?  Tujiulize kwanini vita  dhidi ya ufisadi sio tena hoja kubwa kwa CHADEMA na UKAWA mara tu baada ya kumpitisha Edward Lowasa kupeperusha bendera ya chama hich na umoja huo katika nafasi ya urais kwenye uchanguzi Mkuu.

Zaidi sana tujiulize ni kwa nini Edward Lowasa anapata kigugumizi kukemea ufisadi? Tumhoji atawezaje kutekeleza ahadi zake lukuki za mabadiliko bila kuwa na haki na uthubutu wa kukemea ufisadi? Atahakikishaje huduma za jamii zinapatika kwa wananchi wote, elimu burekwa wote mpaka chuo kikuu, na kuongeza tija kwenye sekta mbalimbali za uzalishaji bila kudhibiti mianya ya ufisadi? Au anaikwepa vita dhidi ya ufisadi kwa sababu anajua ni kupitia ufisadi pekee hasa kwa njia ya manunuzi na mikataba feki ndio anaweza kulipa hisani kwa marafiki zake wanaoendelea kufadhiri mradi wake wa kuingia Ikulu. Nachelea kusema kuwa kwa Edward Lowasa uraisi ni mradi wakunenepesha mitaji ya matajiri wanaojiita marafiki zake ambao sasa wamekaa mkao wa kula. Sioni dalili za mabadiliko chanya yanayowezakutokana na kiongozi wa aina hii kwenye nchi yetu kwa kuzingatia muktaza tulionao kijamii, Kisiasa na kiuchumi.

Wapo wanaosema eti kwa sababu ajenda ya ufisadi ipo ndani ya Ilani ya CHADEMA ambayo pia inanadiwa na UKAWA, hivyo ikitokea Edward Lowasa akashinda atalazimishwa na ilani hiyo kukemea ufisadi. Wachambuzi hawa wanawezakuwa sahihi endapo wafanya tathmini ya taswira ya uraisi anaoutamani Edward Lowasa na ukweli kwamba ataapishwa kama Edward Lowasa.  Hasa kwa kuzingatia Katiba ya sasa ni dhahiri kwamba atakapoingia tu madarakani sioni kama CHADEMA watakuwa tena na nguvu ya kumdhibiti.

Tusisahau pia kuwa ni CHADEMA na UKAWA ndio walimbembeleza Edward Lowassa kujiunga nao na ni dhahiri kwamba sharti ambalo aliwapatia ni kumpitisha yeye kugombea uraisi. Kana kwamba haitoshi kampeni za mgombea uraisi kupitia CHADEMA na UKAWA zinafadhiliwa kwa asilimia kubwa na Edward Lowassa na Marafiki zake. Maana yake ni kwamba watakapoanza kutaka kudhibiti utekelezaji wa mradi wake wa kunenepesha mitaji ya mafisadi waliofadhili safari yake kuingia Ikulu atawauliza swali dogo tu mnategemea nitalipaje madeni ya kampeni za uchaguzi? Kwa kuufahamu ukweli wa mkataba kati ya viongozi wa CHADEMA/UKAWA na Edward Lowasa lakini pia kwa madaraka makubwa atakayokuwanayo kama raisi wakati huo hawataweza kumdhibiti. 

Wapo wanaoweka imani kwenye uwezekano wa kubadilisha katiba ili pamoja na mambo mengine kupunguza madaraka ya raisi. Ufahamu wangu juu ya uwezo wa watu binafsi kufanya mabadiliko na kiwango   cha mabadiliko huchangiwa sana na historia ya muhusika na kundi/kizazi/tabaka anakotoka. Kwa mfano mara nyingi wazee ni hawapendi madiliko hasa yale yanayokinzana na matakwa yao. Simuoni mzee Edward Lowasa katika umri wake eti anatakakuleta mabadiliko ya kasi hasa ukizingatia yeye ukiacha majanga ya kisiasa aliyokutana nayo yupo katika tabaka la matajiri.

Dkt. John Pombe Magufuli na Mabadiliko ndani ya CCM

Watanzania wengi bila kujali itikadi na nafasi zao wamewahi ama  kusikia, kukiri, au kuthibitisha kwa vitendo kuwa  Dkt. Magufuli ni kiongozi shupavu, mwenye dira na uwezo wa kubadili mifumo  na utendaji  katika sekta mbalimbali. Hii inathibitika wazi pale watu wanapoamua kufanya tathmini sahihi ya utumishi wa kiongozi huyu kwa kuangalia  utendaji wake na mafanikio yaliyofikiwa na sekta au taasisi ambazo Dkt Magufuli amewahi kuzisimamia.  Hapa ni vigumu kupinga ukweli kwamba Dkt magufuli ndiye aliyeleta mabadiliko na maboresho katika sekta ya Ujenzi hususani wa miundo mbinu ya barabara.

Maeneo mengine ambayo Dkt Magufuli ameacha  mbegu ya maboresho ni  katika sekta ya ardhi pamoja na ile ya mifugo na uvuvi  licha ya kuzitumikia sekta hizi kwa muda mfupi kabla ya kurejea tena kwenye sekta ya Ujenzi. Taswira ya sasa ya sekta ya ujenzi ambayo sio tu kwamba ina mifumo bayana na thabiti licha ya changamoto kadhaa, sekta hii inasimamiwa na taasisi madhubuti ambazo zinalenga kutafsiri dira na mikakati ya sekta katika uhalisia na vitendo.

Akiwa Naibu wa waziri wa ujenzi katika serikali ya awamu ya tatu, ni Dkt. Magufuli ndie alibadilisha mfumo wa kutegemea wahisani kwa asilimia miamoja katika sekta ya ujenzi wa barabara.Mfumo huu umefanikiwa kwa kiwango kikubwa. Kwa mujibu wa takwimu za wizara ya Ujenzi, takribani asilimia sabini (70%) ya miradi yote ya ujenzi wa barabara inchini inajengwa kwa kutumia fedha za serikali. Ni asilimia thelasini pekee ya miradi yote ya ujenzi inafaddiliwa na wahisani. Swali la kujiuliza ni je nini kimefanikisha utelekezaji wa mfumo huu? Hapa ndipo unawezakuona uwezo na uzoefu wa kiongozi katika kubadili mfumo kwa kujenga taasisi zinazotakiwa ili kusimamia na kuendeleze mfumo.  Ni Dkt. John Pombe Magufuli ndie alieanzisha harakati za maboresho katika usimamizi, utekelezaji na uendelezaji wa sekta ya ujenzi nchini.

Kiongozi huyu amesimamia kuanzishwa kwa taasisi kadhaa muhimu katika sekta ya ujenzi ambazo ni pamoja na Mfuko wa barabara (Road Funds) ambao mapato yake yameongezeka kutoka shilingi bilioni 73.08 mwaka 2005/2006 hadi shilingi bilioni 751.7 mwaka 2014/15. Taasisi nyingine ni pamoja na Wakalawa barabara (TANROADS) inayosimamia ujenzi, ukarabati na matengenezo ya barabara na madaraja. Pia zipo taasisi kama Wakala wa Majengo Tanzania (TBA); Board ya Usajili wa Wahandisi (ERB); Bodi ya Usajili wa Makandarasi (CRD na Bodi ya Usajili wa Wabunifu wa Majengo na Wakadiriaji Majenzi (AQRB). Taasisi zote hizi zinalenga kutelekeza majukumu tofauti lakini yanayotegemeana katika ustawi wa sekta ya ujenzi. Hapa unaweza kuona mantiki ya ujenzi wa mfumo sio hisia wala propaganda.

Mifano hii michache ni kielelezo cha uzoefu, dhamira na upeo, na umakini wa kiongozi katika  kuchambua, kuamua na kusimamia mambo miradi ya maendeleo. Ni mgombea Dkt. John Pombe Magufuli ndie ambae amembanua wazi dhamira na mikakati yake kuhusu vita dhidi ya ufisadi. Huyu sio tu kwamba anasema dhahiri kwamba  atafungua mahakama maalumu ya kushughulikia kesi za ufisadi lakini pia uzoefu katika wizara alozitumikia una akisi dhamira hii.


Ni vigumu kupinga ukweli kwamba hatua ambayo nchi yetu imefika inahitaji kiongozi ambae sio tu anapenda kusema kile ambacho watanzania wanapenda kusikia bali kile watanzania wanachohitaji yaani Kiongozi mwenye uwezo wa kurejesha uadilifu, uaminifu na uchapa kazi katika sekta zote.

NI SAWA TUNATAKA MABADILIKO: JE NI YA MAGUFULI AU LOWASSA??


Tutafakari kwa Hoja na Sababu

Wagombea Urais wa CCM, Dr. John Magufuli na mwenzake wa CHADEMA Ndg Edward Lowassa wanakubaliana jambo moja kubwa: Haja ya kuwa na mabadiliko katika nchi yetu. Wagombea wote wameahidi kila mmoja kuwa iwapo atashinda ataleta mabadiliko. Tulinganishe sasa na kupima aina ya mabadiliko ambayo yanaweza kutokea iwapo mmojawapo atachaguliwa kuwa Rais wa nchi yetu.

Kulingana na historia ya utendaji wake katika wizara alizokabidhiwa na ahadi anazotoa mgombea wa CCM, Dr. John  Magufuli, chini ya Urais wake inaonekana  utawala wa sheria na nidhamu ya kazi kwa watumishi wa umma itatamalaki.  Magufuli anajulikana zaidi kwa Watanzania kuwa ni mtu anayesimamia sheria hata pale zinapogusa maslahi ya wakubwa zake. Watanzania watakumbuka jinsi Magufuli alivyoweza kurudisha magari yaliyokuwa yameporwa kinyemela  na vigogo wa serikali enzi za utawala wa Benjamin Mkapa.

Kwa upande wa  Ndg. Edward Lowasa, iwapo  atachaguliwa kuwa Rais, kuna uwezekano mkubwa kukawa na utawala unaotegemea hisia za Rais na ‘marafiki’ zake  badala ya utawala wa sheria. Utendaji wake wa nyuma unaonyesha wazi kuwa Lowassa kama kiongozi ni mtu anayeamini matashi yake binafsi bila kuzingatia utawala wa sheria. Watanzania watakumbuka kuwa March 2006, akiwa waziri mkuu, Lowassa alimfukuza kazi mhandisi wa Manispaa ya Temeke bila kumpa nafasi ya kujitetea na tena mbele ya waandishi wa habari na kundi la wananchi waliokuwepo katika tukio la kuporomoka jengo la Chang’ombe Village.  

Hivi karibuni, wakati anazindua kampeni zake, Lowassa alitoa ahadi kuwa ikiwa atashinda atamuchia huru Nguza Viking, maarufu kama Babu Seya aliyefungwa maisha jela kwa kwa kosa la  kubaka na kulawiti watoto katika hukumu iliyotolewa na mahakama ya hakimu mkazi kisutu mwaka 2004. Kesi hiyo ilipelekwa katika mahakama ya rufaa mwaka 2010 na Mahakama ilikubaliana na uamuzi wa mahakama ya chini. Tena, mwaka 2013, jopo la majaji wa mahakama ya rufaa watatu likijumuisha Jaji Nathalia Kimaro, Mbarouk Mbarouk na Salum Msati walifanya mapitio ya mahakama hiyo na kuwaona wafungwa hao kuwa wana hatia.

Ikumbukwe kuwa sheria za Tanzania zinamyima Rais mamlaka ya kusamehe watu waliofungwa kwa makosa ya kubaka na kulawiti. Kwa kutamka kuwa atawachia wazi wafungwa hao,bila ya kusema chochote juu ya wale watoto waliolawitiwa na kubakwa na haja ya kufuata utawala wa sheria nchini ni dhahiri kuwa katika utawala wa  Lowassa utawala wa sheria utawekwa kando na matashi ya watawala ndio yatakuwa yanaongoza nchi. Hili linadhibitishwa na ahadi nyingine  ya  Lowassa  kuwa  akiwa Rais, watuhumiwa wa kesi za ugaidi waliokamatwa huko Zanzibar wataachiwa huru kwa amri ya Rais. Ikumbukwe kuwa kwa sasa dunia iko kwenye vita dhidi ya ugaidi na ugaidi ni hatari kubwa na thahiri kwa maisha ya  wananchi na mali zao.

Wagombea wote wameahidi kupambana na ufisadi na rushwa iwapo watachaguliwa kushika nafasi ya Urais. Magufuli ameahidi wazi kuwa ataleta  mabadiliko katika vita dhidi ya rushwa na ufisadi kwa kuanzisha mahakama maalum ya kushughulikia masuala hayo. Kuna uwezekano mkubwa kuwa rushwa itaweza kudhibitiwa katika utawala wake ukizingatia kuwa katika harakati zake zote hakuungwa mkono na genge la mafisadi kama ilivyozoeleka kwa siasa za CCM tangu mwaka 2005 ilipotekwa na genge la wanamtandao.

Hali hii itamfanya aweze kutawala bila kuwa na  deni la kulipa fadhila kwa mtu yeyote. Uzoefu wa siku za karibuni unaonyesha kuwa rushwa na ufisadi mkubwa unasababishwa na kujaza ‘marafiki’ katika nafasi muhimu za maamuzi. Kujaza marafiki hasa waliokufadhili kwenye harakati za uchaguzi kunafanya mifumo ya uwajibkaji katika nchi iwe na ganzi ya kufanya kazi dhidi ya marafiki hao.

Kwa upande wake Lowassa hajaeleza atafanya nini bayana katika kupambana na rushwa zaidi ya kusema atashughulikia rushwa. Kama ambavyo ilibainishwa na waziri mkuu mstaafu na mpambe wa Lowassa katika harakati za Urais, Fredrick Sumaye,  katika viwanja vya jangwani, Lowassa ndiye mwasisi wa ‘mtandao’ uliomwingiza Rais Kikwete madarakani mwaka 2005. Kundi hili lilimjumisha pia Rostam Azizi na Laurence Masha ambao leo hii ndio pia ndio wanaongoza mikakati ya Lowassa. Rushwa katika mikataba ya aina mbalimbali na hata ukwapuaji wa fedha za umma kupitia maskandali mbalimbali kama EPA, Richmond  na Dowans ulifanyika kama njia ya kulipa deni la fadhila wakati wa uchaguzi. Kama tulivyogusia hapo juu, ni vigumu kuchukua hatua dhidi ya marafiki na maswahiba.

Baada ya CCM kujikomboa kutoka katika makucha ya wanamtandao kwa kuwaondoa wagombea wa kundi hili akiwemo Lowassa kwenye kinyang’anyiro cha kugombea Urais kupitia chama hicho, kundi hilo limeweza ‘kuiteka nyara’ CHADEMA na kupitia kwake vyama vikuu vya upinzani kupitia UKAWA. Lowassa amesema waziwazi kuwa fedha anazogawa kwa wananchi mbalimbali zinatokana na ‘marafiki’ zake. Kwa hiyo, kama atachaguliwa, utawala wa Lowassa utaendeleza utawala wa wanamtandao, na watanzania watarajie kushamiri kwa ufisadi nchini kwa sababu tulizoeleza hapo juu.

Watanzania watakumbuka kuwa kile kinachoonekana kuwa ni ushabiki wa kupindukia kwa Lowassa hauna tofauti na ushbiki uliokuwepo mwaka 2005  kwa Kikwete. Hii inatokana na ukweli kuwa kundi linaloratibu na kuongoza kampeni za Lowassa ni lilile lililofanya kazi hiyo mwaka 2005. Tayari, kuna taarifa zinazosema kuwa wanamtandao wameshagawana nafasi muhimu za uongozi na mikataba katika maeneo manono kama bandari, madini na vitalu vya gesi na mafuta iwapo watafanikiwa kuiteka dola kupitia uchaguzi.

Magufuli ameahidi kuwa ataleta mabadiliko katika utendaji wa watumishi wa umma kwa kuweka mifumo imara ya uwajibikaji. Watu walio karibu na Magufuli wanasema kuwa Magufuli ameahidi kuwa akiwa Rais atawekeana mikataba ya utendaji kazi (Perfomance contracts) na mawaziri wake ambapo kila waziri ataingia kama yeye binafsi na akishindwa kufikia malengo atawajibishwa kwa kuondolewa madarakani. Magufuli ameahidi pia kuwa mafisadi watakaotiwa hatiani watafilisiwa mali zao. 

Kwa upande wake Lowassa amesema kuwa akiingia madarakani atabadilisha mfumo wote wa nchi. Hii ina maana kuwa Lowassa akiwa Rais, taasisi za utawala kama vile Polisi, Jeshi, Utumishi wa Umma na vyombo vingine vitafumuliwa na kuundwa upya na kuwekwa watu wapya. Muhimu hapa ni kukubaliana  kuwa siyo rahisi kwa jambo hilo kufanyika kwa kuwa kama ilivyo duniani kote yeyote atakaye shinda atalazimika kufanya kazi na vyombo hivyo. Mabadiliko yeyote ya utendaji wa vyombo hivyo vitategemea na hulka, tabia na haiba ya Rais. Hakika duniani kote mabadiliko katika nchi huletwa kwa vyombo hivyo kufanya kazi zao ipasavyo kutokana na uongozi na usimamizi dhabiti wa mkuu wa nchi.

Hitimisho


 Haya ni baadhi ya mabadiliko yanaweza kutokea iwapo mmoja wa wagombea wetu watachaguliwa katika nafasi ya Urais. Mabadiliko haya yanaonyesha wazi kuwa uchaguzi ni muhimu sana kwa mustakabali wetu kama mtu mmoja mmoja na kama Taifa. Kwa sababu hiyo, ushabiki na uungwaji mkono wa wagombea lazima uzingatie faida na hasara zake kwa nchi na kwetu binafsi. Ni wakati wa kuwahoji na kuwatathimini wagombea wetu ili siku ya upigaji kura tisije tukafanya kosa litakalotuathiri sisi na vizazi vyetu.  Tathmini hiyo ni muhimu kwa kujua kuwa utendaji kazi wa Rais huakisi na kuathiri utendaji kazi wa serikali na taasisi zote zilizo chini yake. Yaani Rais akiwa fisadi serikali na vyombo vyote chini yake vitakuwa vya kifisadi. La, Rais akiwa mwadilifu na mchapakazi na serikali yake itakuwa vivyo hivyo. 

Saturday, August 29, 2015

CCM, UKAWA NA KUNG’OA MFUMO WA KIFISADI NCHINI



Wananchi wengi tunakubalina kuwa adui mkubwa wa Tanzania kwa sasa ni  ufisadi ambao ndio umekuwa chanzo kikubwa cha utajirisho wa  watu wachache  na huku ukistawisha umaskini kwa wananchi walio wengi. Baadhi ya wananchi wamekuwa na mawazo kuwa hatuwezi kupambana na ufisadi bila ya kwanza kuiondoa CCM madarakani kwani kwa maoni yao CCM ndio mfumo wenyewe wa kifisadi.  Lengo langu leo ni kutaka tutafakari usahihi wa dhana hii katika uhalisia wake ili itusaidie kuchukua hatua sahihi katika kuung’oa mfumo wa kifisadi nchini.

Kwanza, kuna haja ya kutambua ukweli kuwa rushwa na ufisadi ndiyo adui mkubwa wa maendeleo ya kweli ya nchi yetu. Ukweli huu uligundulika mapema kabisa  baada ya nchi yetu kupata uhuru pale ambapo sehemu ya tabaka la watu walioshika nafasi za uongozi baada ya uhuru kutaka kutumia nafasi zao kwa ajili ya kujitajirisha wao binafsi kwa gharama ya wananchi wenzao. Tabaka hili lililokuwa linajulikana enzi hizo kama wabenzi, ikimaanisha wamiliki wa magari ya Mercedez Benz ambayo ndio ilikuwa alama ya kuwa tajiri, liliona kuwa kushika nafasi ya uongozi katika dola ni kupata fursa ya kijitajirisha. 

Hali  hiyo ingeruhusiwa kuendelea ingewakatisha tamaa wananchi na kujenga ufa baina yao na uongozi wa nchi. Pia hali hiyo ilionekana kusaliti matumaini ya wananchi katika kupigania na kupata uhuru. Hakika hali hiyo ingeruhusiwa kuendelea  ingefanya uhuru usiwe na maana kwa wananchi. Kwa bahati nzuri uongozi wa TANU chini ya Baba wa Taifa uliligundua tatizo hilo na kuchukua hatua za kukabiliana nazo.

Ili kupambana na ufisadi uliokuwa umeanza kujengeka, mwaka 1966 , Mwalimu Nyerere baada ya kupokea changamoto kutoka kwa wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar Es Salaam waliokuwa wanaandamana, wakilalamika pamoja na mambo mengine kuwa viongozi walikuwa wanatumia nafasi zao kujinufaisha alipunguza mishahara ya  viongozi kwa kuanzia na kupunguza mshahara wake kwa asilimia ishirini. Mwaka 1967, TANU ilitangaza sera ya Ujamaa na Kujitengemea iliyokuwa inalengo la kujenga jamii yenye usawa na haki na kukomesha unyonyaji na ukupe kati ya mtu na mtu.

Miiko ya uongozi iliwekwa  ili kuhakikisha kuwa viongozi wanatumia madaraka yao kulingana na dhamana waliyokabidhiwa na si kwa faida  zao binafsi. Miiko hiyo ilidumu mpaka mwaka 1992 tulipoingia kwenye mfumo wa vyama vingi.  Baadhi ya Miiko hii bado ni sehemu ya katiba ya CCM. Ibara ya 18 ya Katiba ya CCM inazuia  kiongozi:- “(1) Kutumia madaraka aliyopewa ama kwa ajili ya manufaa yake binafsi au kwa upendeleo, au kwa namna yoyote ambayo ni kinyume cha lengo lililokusudiwa madaraka hayo. (2) Kupokea mapato ya kificho, kutoa au kupokea rushwa, kushiriki katika mambo yoyote ya magendo au mambo mengine yaliyo kinyume cha lengo lililokusudiwa madaraka hayo.” 

KUTEKWA CCM NA UFISADI

Kwa hiyo, CCM kwa asili yake na mfumo wake imeundwa kupambana na ufisadi na si kukumbatia ufisadi, hata hivyo tunajua kuwa  kwa miaka ya karibuni ufisadi umemea na kukuwa kwa kiwango kikubwa nchini. Hali hii imesababishwa kwa kiwango kikubwa na kufanikiwa kwa kundi la watu wachache lakini lenye ukwasi mkubwa lijulikanalo kama ‘mtandao’  kufanikiwa ‘kuiteka nyara’ CCM kwa kufadhili wagombea kwenye nafasi za ubunge na Uraisi.  Walioshika madaraka katika nyadhifa za uongozi walitumia nafasi hizo kulipa fadhila kwa wafadhili wao kwa njia ya mikataba minono lakini yenye athari kubwa kwa maisha ya wananchi. Ni katika kipindi hichi ndio tumeshuhudia maskandali  ya kifisadi kama vile mkataba wa Richmond, Meremeta, ukwapuaji wa fedha za EPA, n.k. Hali hii ilitokea ili ngenge la mtandao liweze kufidia gharama walizotumia kufadhili kampeni za mawakala wao kuingia madarakani. Hali hii iliimarika zaidi baada ya  uchaguzi wa 2005.

Katika uchaguzi wa mwaka huu na kama ilivyokuwa katika chaguzi za kuanzia mwaka 1995, ili kuendelea kunufaika na rasilimali za nchi kundi la mtandao, limejizatiti kwa kutumia nguvu ya hela kuingiza mawakala wao katika nafasi ya Urais. 

Hata hivyo, mara hii CCM ilifanikiwa kuzishinda  jitihada za kundi hili ‘kuiteka’na kuhakikisha kuwa mgombea wa kundi hili  katika nafasi ya Urais hateuliwi kugombea Urais kupitia chama hicho.  Jitihada hizo ndio zilisababisha mgombea wa sasa wa Urais wa Tanzania kupitia CCM, Dr. John Magufuli kuteuliwa. Sifa kubwa iliyombeba Magufuli ni kutokuwa ngenge la watu wenye fedha wanaomfadhili.  Kwa uteuzi wa Magufuli, CCM inaonyesha kuwa imejizatiti kurudi kwenye asili yake ya chama kinacho simamia maadili na miiko ya viongozi.

KUTEKWA NYARA KWA UKAWA

Baada ya kundi la mtandao kung’olewa CCM na ili liendelee kunyonya  na kufisadi rasilimali za nchi,  lilifanya jitihada kubwa kwa kutumia nguvu ya pesa kuviteka vyama vya upinzani vyenye nguvu nchini kupitia umoja wao wa UKAWA. Kwa kuelewa kuwa kundi hili linataka madaraka si kwa sababu nyingine ila kuendelea ‘kuifaidi’ Tanzania lakini kwa gharama  ya maisha ya Mtanzania wa leo na vizazi vijavyo, waasisi wa UKAWA ambao walitoa maisha yao  kuunda na kuujenga UKAWA  kama njia ya kuimarisha upinzani nchini, Dr Wilbroad Slaa na Prof. Haruna Lipumba wameamua kukaa pembeni ili kuepuka kushiriki kuingiza madarakani mfumo wa kifisadi ambao walitumia muda na maisha yao kupambana nao.

Hakika historia itawakumbuka viongozi hawa  kwa misimamo yao imara ya kupinga mfumo wa  ufisadi kokote hata kama wanufaika wa mfumo  huo watakuwa wao. Maana nafasi zao ziliwahakikishia kufaidi matunda ya mfumo huo kwa sasa na ikitokea kundi hilo likashinda uchaguzi.

KUNG’OA MFUMO WA KIFISADI

Tumeona kuwa chanzo kikubwa cha kuvurugika kwa mfumo wa maadili nchini ni ngenge la mtandao ambalo kwa kutumia nguvu ya pesa limeweza kuingiza mawakala wao kwenye nafasi za uongozi kupitia CCM. Bahati nzuri CCM wameweza kupambana na kundi hilo kwa kuzuia jitihada zake za kuendelea kuiteka nyara. Tumeona kuwa, baada ya kushindwa kundi hilo sasa limeuteka upinzani nchini kupitia UKAWA kwa kutumia nguvu ya fedha. Wananchi wameshuhudia kundi hili likigawa hela kwa makundi mbalimbali ya wananchi katika kujihakikishia wanapata uungwaji mkono ili  mgombea wao aweze kushinda Urais.


Kundi hili haliamini katika sera au itikadi yeyote ndio maana liliposhindwa CCM limehamia UKAWA  ambapo kila chama kina ilani,sera na itikadi tofauti. Hali haliwasumbui kwa maana shida yao kama wanavyosema wenyewe siyo sera bali kushika madaraka ili waendelee kuifisadi nchi.  Kwa kuhitimisha kama tunataka kung’oa ufisadi nchini, inabidi tuhakikishe kuwa kundi hili la haliingii tena kushika madaraka ya nchi.