Saturday, May 30, 2015

NIMUONAVYO RAIS WA AWAMU YA TANO: NATEGA KITENDAWILI



Wiki hii joto katika Chama cha Mapinduzi litazidi kuongezeka kadri makada zaidi wanavyopambanua nia zao za kuomba ridhaa ya chama ili washike bendera ya CCM katika Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani ifikapo Oktoba 25 mwaka huu.

Joto hili halitakuwa mahali pamoja, bali kila kona ya Taifa letu, hasa hasa upande wa Tanzania Bara, kule Kaskazini Mashariki, Arusha, Kaskazini kanda ya ziwa, Mwanza, Nyanda za juu kusini, Mbeya na kule kusini mwa Nchi Lindi. Kwa CCM hizi ni ishara njema kwamba kuna watu na kupitia michakato ya kidemokrasia ndani ya chama watu wanajipambanua, lakini chama kisipokuwa makini hii inaweza kuwa dalili isiyokuwa njema, dalili ya mvurugano, dalili ya mpasuko na kugawanyika kwa chama.

Katika Makala hii nataka nieleze kwa sehemu, na kwa mtizamo wangu nimuonavyo Rais wa awamu ya tano ukizingatia nafasi ambayo Marais wa awamu nne zilizotangulia michango yao imekuwa kwa Taifa letu. Ni muhimu kwa wagombea kujitathmini nafasi zao, dhamira zao na mipango yao ili kukidhi mahitaji ya watanzania sasa lakini pia watanzania wanatakiwa pia watambue kila awamu kwa bahati imekuwa na utume wake. Watanzania pia na hasa katika hatua hii wanachama wa CCM wanatakiwa watambue utume unaotakiwa katika awamu ya tano ili waweze kuwapima wagombea kama wana sifa, uwezo, mamlaka, uhalali na dhamira ya kutupatia uongozi wa kutimiza utume wa awamu ya tano.

Ili tuweze kumuona Rais wa awamu ya tano, tuna budi kuelewa utume wa awamu nne zinazotangulia kwa ufupi,-

Awamu ya Kwanza- JK Nyerere

Mwalimu katika nchi yetu ndiye alikuwa na dhamana ya kukata pori na kuianzisha nchi pamoja na sambamba na mashujaa wengine wengi raia wa Taifa letu. Mwalimu alikuwa na kazi ya kwanza kuleta Uhuru wa Tanganyika na baadaye, yeye na Sheikh Abeid Aman Karume kuunganisha Jamhuri ya Tanganyika na Jamhuri ya Watu wa Zanzibar ili kuunda Nchi Mpya Mwaka 1964 ambayo sasa inajulikana kama Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Mwalimu alikuwa na kazi ya kulijenga Taifa awali, kuwaleta watu pamoja, huku akiheshimu makabila ya watu na mtawanyiko wa makabila katika Tanzania mpya lakini akiupinga na kuutokomeza kwa kiasi kikubwa ukabila.

Kisha akawa na kazi ya kuliunganisha Taifa kuwa kitu kimoja, akatusaidia kukuza utanzania na akasimamia lugha ya Kiswahili kama lugha ya Taifa. Akahakikisha kuna amani na Umoja na ili hayo yaendelee akajenga misingi imara na thabiti ya haki na usawa miongoni mwa watu wetu.

Akajua amani na Umoja utakuja kama haki itatendeka, kutakuwepo usawa wa watu na wa kimaeneo hivyo akaanza kwa sehemu kufanya majaribio ya kujenga na kuimarisha uchumi. Akatizama uzalishaji katika ngazi zote, katika ngazi ya Taifa akawezesha dola kushika hatamu katika uchumi kwa maana ya uzalishaji, kutoa huduma na kukusanya kodi. Katika ngazi za msingi akaanzisha vijiji vya ujamaa, watu wafanye kazi kwa pamoja, wazalishe pamoja na wanufaike pamoja na matokeo mazuri ya kufanya kazi kwa mshikamano. Akailinda nchi dhidi ya maadui wa ndani na wa nje. Alitenda kwa sehemu yake mpaka alipomwachia kijiti Mhe. Alhaji Ali Hassan Mwinyi.

Awamu ya Pili- Alhaji Ali Hassan Mwinyi

Mhe. Mwinyi alichukua kijiti wakati nchi ilikuwa bado imara kwa maana ya Umoja, mshikamano, Amani na utulivu, lakini kiuchumi nchi ilikuwa imetetereka sana. Uchumi ulioshikiliwa na dola ulikuwa umelemewa na mahitaji wananchi na utendaji wake haukuwa wenye ufanisi mkubwa. Tulikuwa na udhaifu wa ndani kwa maana ya kutokuwajibika miongoni wa watendaji na Wananchi lakini pia tulikuwa na shinikizo kubwa kutoka nje hasa mataifa makubwa na mashirika ya kimataifa.

Mzee Mwinyi alikuwa na kazi ya kufungua milango ili kila anayeweza kuzalisha basi asaidie kazi ya serikali ya uzalishaji ili chakula na bidhaa ziwafikie watu wa Taifa letu. Kidogo kidogo akaanza kuufanyia marekebisho mfumo wa uchumi wetu kutoka uchumi inaoshikiliwa na dola kwenda kwenye uchumi huria ambao watu na wadau mbalimbali ni washiriki katika kufanya shughuli za uzalishaji na kutoa huduma. Lakini pia akawa mkali kwa wale ambao hawakuwa wawajibikaji, utakumbuka kipindi kile nyimbo maarufu zilikuwa kama vile “usipowajibika ole wako, utakumbwa na fagio la chuma”. Aidha akawapa hamasa Wananchi kwamba kwa hali tuliokuwa nayo kipindi kile ilikuwa budi sote tushikamane, utakumbuka misemo kama “Wananchi sote tujifunge mikanda”.

Ni kipindi hiki Taifa lilianza kuona huduma za kijamii sasa zikianza kutolewa na mashirika yasiyo ya kiserikali, huduma za ughani katika kilimo, mifugo na uzalishaji mdogomdogo. Ni katika kipindi hiki asasi mbalimbali zilianzishwa na kusajiliwa ili ziisaidie serikali katika kujenga Taifa.

Ikawa ni dhahiri kwamba awamu ya pili ilikuwa ya kujenga mfumo mpya wa uchumi kwa Taifa letu na ambao kwa kiasi kikubwa ulikuwa unaendana na mahitaji ya wakati na dunia. Mzee Mwinyi akaweka misingi ya uchumi huria, tuliyumba yumba kidogo lakini ilikuwa mwanzo. Kubwa zaidi Mzee Mwinyi akaimarisha pia misingi ya demokrasia, katika awamu ya pia tukaondoa mfumo wa demokrasia ya chama kimoja na kwenda katika mfumo wa demokrasia ya vyama vingi. Mfumo huu uliongeza uwajibikaji, ushiriki wa mpana wa Wananchi katika uongozi wa nchi na uwazi katika shughuli za serikali.

Mzee Mwinyi alitenda kwa sehemu yake mpaka Mhe. Benjamin W. Mkapa alipopokea kijiti.

Awamu ya Tatu- Mhe. Benjamin W. Mkapa

Mhe. Mkapa, alikuwa na kazi moja kubwa, kuimarisha hatua zilizopigwa na awamu ya pili hasa katika kuendelea kuupanga na kuuimarisha uchumi wetu katika mfumo mpya tuliouchukua. Serikali ya Awamu ya tatu chini ya uongozi wa Mzee Mkapa ilijikita katika kuhakikisha kuna “transition” nzuri kutoka uchumi uloshikwa na dola awali kwenda uchumi huria ambao umeshikwa na watu katika sekta binafsi. Kipindi chake kilikuwa na kazi kubwa ya marekebisho ya kimfumo na kitaasisi, wengi wenu mtakumbuka Tume maarufu ya “Parastatal Sector Reform Commission (PSRC)” ambayo ilianzishwa kwa sheria ya Mashirika ya Umma ya mwaka 1992 na kazi kubwa ilikuwa kufanya ubinafsishwaji wa mashirika ya umma.

Mzee Mkapa katika ujenzi wa uchumi huria imara alisimamia uwazi na ukweli hasa kipindi chake cha kwanza, alipiga vita na alichukizwa na rushwa. Hata katika kampeni zake za Urais alitoa ahadi ya kupambana na rushwa, baada ya ushindi mwaka 1996 aliunda Tume ya Kupambana na Rushwa iliyojulikana kama “Tume ya Warioba”. Kwa hakika kulikuwa na matatizo ya hapa na pale tena mengi tu, lakini sote tunakubaliana kwamba Mzee Mkapa alituimarishia uchumi wetu katika mfumo wa soko huria. Uchumi Mkubwa ulikuwa unakuwa mpaka anaondoka kwa asilimia karibu saba. Kazi aliyokuwa ameiacha haijatimia ilikuwa ni kuutafsiri ukuaji wa uchumi mkubwa ambao ulionesha mafanikio makubwa katika maisha ya watu wa Kawaida. Kazi hiyo ilikuwa sasa ni ya Mhe. Dkt. Jakaya Kikwete Rais wa Awamu ya Nne ambaye alipokea kijiti.

Awamu ya Nne- Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete

Awamu ya nne kama ambavyo ilivyojinasib wakati wa kampeni zake wakati wa uchaguzi mkuu wa mwaka 2005 kwamba “Maisha bora kwa kila Mtanzania”. Ukiitafsiri kauli mbiu hii utakubaliana nami, uongozi wa awamu ya nne ulikuwa na kazi ya kutafsiri uchumi Mkubwa (Macro) kutokana na tija itokanayo na viwanda na uwekezaji mkubwa kwenda uchumi wa kati (Meso) katika jamii zetu na kisekta kama vile kilimo (Kilimo Kwanza), elimu (shule za Kata) na hata tushuke kiuchumi hadi ngazi ya mtu wa kawaida (micro) hapa ndio tungeona uhalisia wa maisha bora, watu wenye nyumba nzuri, ajira zenye staha, kipato chenye kukidhi mahitaji na watu wanaokopesheka.

Awamu ya nne imekuwa na jukumu la kuendelea kujitahidi kugawa keki ya Taifa katika mazingira na uhalisia tofauti tofauti, kama vile ujenzi zaidi wa barabara, uwekezaji zaidi katika elimu na kilimo. Nchi inapofika katika kiwango cha kuanza kugawa keki ya Taifa huwa inafanya hivyo baada ya kunufaika na ukuaji mkubwa wa kiuchumi na huwa ni wajibu wa serikali kuhakikisha kwamba ugawaji wa keki unaenda sambamba na jitihada za kuendelea kukuza na kuuimarisha uchumi mkubwa.

Awamu ya nne imeendelea pia kushughulikia pia ujenzi wa demokrasia na kuimarisha mifumo ya udhibiti na kuweka ukomo wa matumizi ya madaraka kwa watumishi na viongozi wa umma, hili mpaka sasa halijakamilika. Mifano ni maboresho mbalimbali ya kitaasisi katika serikali, kuanzishwa kwa mchakato wa Katiba Mpya ambayo ungehakikisha ugawanaji wa keki unawanufaisha wengi na sio makundi ya wajanja wachache, hili halijakamilika.

Utagundua pia katika awamu zote nne, kimsingi tuna kila kitu ambacho kama nchi inahitaji ili kupiga hatua. Kwa mtizamo wangu kilichobaki ni kufanya sasa marekebisho ya mifumo na taasisi na fikra za watu (Wananchi, watumishi na viongozi wetu) na kuhakikisha wote waliopewa dhamana wanatenda hivyo kwa uadilifu na wakijua wakipotoka watawajibishwa kwa mujibu wa sheria na kamwe hawatakaa juu ya sheria.

Awamu ya Tano- Nimuonavyo Rais huyu (…)

Namuona Rais wa awamu ya akisheheni haiba ya uadilifu, mtu asiyejikweza, mwenye kukubalika na watu, mwenye “moral authority” yaani mtu mwenye uwezo na mamlaka ya kukemea wezi, watu wasio na uadilifu. Mtu ambaye anatambua kwamba mafanikio yote tuliyoyapata katika awamu zote nne hayawezi kutimia pasina kuwa na mifumo ya udhibiti “systems and controls” inayofanya kazi katika taasisi zetu kutoka ngazi ya kitaifa mpaka mtu mmoja mmoja.

Kuna kipindi katika historia za dini kuna kitu kiliitwa “reformation” au matengenezo, tumefika pahala ambapo tunahitaji Kiongozi ambaye atakuja kufanya matengenezo, marekebisho na maboresho kuanzia ikulu hadi katika jamii zetu. Baada ya kipindi cha reformation kupita sasa nitawaona wajenzi wa barabara, wajenzi wa shule, waboresha kilimo na huduma za afya. Kwa sasa tunataka mtu wa kuja kutunyooshea njia, kuturudishia maadili ya Taifa, Maadili ya utumishi na Uongozi wa Umma, kutujengea mifumo na taasisi imara na madhubuti ambazo zitahakikisha kuna uadilifu na uwajibikaji katika sekta ya umma na sekta binafsi.

Rais ajaye nimuonavyo ni yule ambaye anajua watanzania wameshaibiwa sana, vijana wanasema tumeshapigwa sana. Kilimo hakikui kwasababu kuna watu wananufaika na kuagiza mchele kutoka nje. Kilimo cha sukari hakikui kwasababu kuna watu wana mirija ya chuma katika kuagiza sukari kutoka nje. Reli ya Kati inadororora kila siku kwasababu watu wana maslahi na biashara ya maroli. Tunataka Rais ajaye aje na aanzie hapo kutuwekea mifumo ya kudhibiti matumizi mabaya ya madaraka.

Tunataka Rais ajaye Kiongozi akila rushwa hatasubiri akemewe atajiondoa mwenyewe haraka. Tunataka baba, Kiongozi, mtu ambaye tukimtizama tutakuwa na amani na maisha yetu, tunamtaka mtu ambaye sasa anaonesha kupenda heshima ya Wananchi. Tunamtaka mtu ambaye atarudisha heshima ya cheo cha msingi ambacho ni “Raia”. Tunamtaka mtu asiyejipeleka kwa “wazi” au kwa “kificho”, kwa “kelele” au “kimya kimya”.

Mwisho tunamtaka na nimwonavyo Rais wa Awamu ya Tano, ni mtu mwenye uhalali, mtu anayekubalika katika pande zote za Muungano kwa maana ya Tanzania Bara na Zanzibar. Mtu ambaye kwasasa Wananchi wanajinasibisha naye, kwasababu anawajua, na wanajua anajua mahitaji yao. Mtu ambaye amesimama nao bega kwa bega na ambaye hajaona aibu kusimamia maslahi yao wakati wowote.

Naomba mnitegulie kitendawili.


Saturday, May 23, 2015

TAFAKURI YANGU YA UONGOZI NA MCHAKATO WA NDANI WA CCM KUPATA WAGOMBEA: TUJIREKEBISHE



Mungu ametupa akili, busara na hekima, kisha akatupa ufahamu, fikra na uwezo wa kuunda taasisi ili zitusaidie kuturatibu, kutuwezesha na kutusaidia. Kwa ufahamu aliotupa Mungu, akatuwezesha kuchagua na kuteua kutoka miongoni mwetu watu wa tofauti, watu wasiojipenda wenyewe, watu wenye uwezo mkubwa na maono, watu wapole, wenye uhalali katika jamii wa kuonya na kukemea ili hawa wawe viongozi wetu.

Uongozi ni dhamana, ni jukumu zito, mtu uongozi hupewa na watu, hubarikiwa na hata kulazimishwa, uongozi huwa hautafutwi kwa udi na uvumba. Katika dini zote na jamii za watu katika historia viongozi walitengenezwa, hata wale waliozaliwa katika mnyonyororo wa uongozi iliwapasa kulelewa kiuongozi. Ilimpasa mtu awaye kiongozi, kuhakikisha kwamba anawaleta watu wake pamoja, masikini na matajiri, wakulima na wafanyakazi, wafanyabiashara wadogo na wakubwa.

Kiongozi anapaswa kuwa msingi imara wa umoja wa kitaasisi, jamii na Taifa kwa ujumla. Kiongozi anayeanza na mpasuko na si umoja, kiongozi anayeanza na chuki na si upendo, viongozi wanaoanza na makundi na si taasisi kwanza, tafsiri yake si njema, si afya na ni muendelezo wa nyufa katika taasisi yoyote ile.

Chama cha Mapinduzi (CCM) hivi karibuni kitatoa utaratibu na mchakato wa kumpata mgombea wa Urais kupitia CCM. Tukumbuke tena, CCM ndio chama kilichopo madarakani sasa, hivyo inapaswa kuonesha mfano, CCM inapaswa kuwa kioo, najua CCM imejikwaa wakati mwingine kwa makusudi na wakati mwingine kwa bahati mbaya. Sifa kubwa ya uongozi thabiti ni kuonesha uongozi pale ambapo watu ndani ya taasisi au kwa ujumla Taasisi inapojikwaa. Kuonesha uongozi kunaweza kuwa katika namna nyingi, mojawapo ni kwa hali yoyote kuukumbatia ukweli pasina kuathiri menejimenti ya siasa

Uongozi ni kuonesha kutokuvunjika moyo, kutokukata tamaa, kujikwaa sio kuanguka, na kama CCM imetetereka bado inaweza kuamka tena na kuthibitishia umma wa watanzania kwamba misingi ya kusimamia maadili na miiko ya viongozi bado iko imara kama ilivyo misingi ya CCM ambayo kwayo iliasisiwa.

Labda nitolee mfano wa mambo kadhaa ambayo kwa makusudi baadhi ya wana CCM wamesaidia kuteteresha CCM. Mosi, namna ambayo chama ambacho ndio kimeshika mamlaka ya nchi na serikali kimeshughulikia masuala ya ubadhirifu wa mali ya umma, kumekuwa na tuhuma kadhaa wa kadhaa katika miaka 10 iliyopita. Tumeona uwajibikaji, lakini CCM ingeweza kufanya vizuri zaidi ili kurudisha imani ambayo inaonekana dhahiri kutetereka miongoni mwa wananchi. Uongozi wa CCM unapaswa kuwa mkali zaidi kwa wale wanaokwenda kinyume na misingi ya kuanzishwa kwa CCM. Urafiki ni jambo jema, lakini misingi ya CCM inapaswa kuwa juu ya urafiki wakati wowote.

Wengi wenu, viongozi wa CCM mlikuwepo kipindi cha Mwalimu Nyerere na kwa hakika wengi wenu ni mashahidi wa namna alitenda kama Kiongozi. Hivi kuna kipindi kigumu kama miaka ya 80 mwanzoni? Kipindi kile ambacho ajira rasmi ziliporomoka kwa karibu asilimia 80, matatizo ya njaa na kutetereka kwa uchumi wa nchi. Mwalimu alikuwa mkali kweli kweli, lakini pia alikuwa kama baba, alikuwa msikivu na mpole, kama Kiongozi mkuu ndio mwenye dira, ndiye anayetupa hamasa kupiga makasia katika Bahari iliyochafuka ili tuelekee uelekeo sahihi na salama, ambaye kupitia kwake watu walipaswa kuyaona matumaini, walipaswa kuiona Tanzania njema.

Mnakumbuka vikao vya Karimjee vya kuokoa uchumi wa Taifa letu miaka ya 80 katikati, nafasi ya Mzee Kawawa ya menejimenti ya siasa au “political management” katika vikao pale hali ilipochafuka. Hali ilipokuwa tete, na hasira ziko juu, Mzee Kawawa kwa busara na hekima zake alijua namna ya kutukwamua na hali ikapoa, kisha Mwalimu akaahirisha kikao mpaka siku inayofuata, hiyo ndio ilikuwa CCM.

Leo hii nidhamu ya baadhi ya wana CCM na viongozi imeshuka, nasikia hata kuzomeana kumo katika vikao. Kuheshimia miongoni mwa viongozi ndio msingi mkubwa wa kujengeana imani na kuaminiana. Viongozi wasioaminiana, hawaheshimiani, viongozi wasioheshimiana hawapendani, na viongozi wasiopendana hawazungumzi kwa uwazi na ukweli. Tunapofika hapo, taasisi ya chama iko mashakani, uongozi wa nchi kutoka katika chama unawekwa rehani.

Zamani ilikuwa tunasema zidumu fikra za Mwenyekiti, usemi huu haukuwa wa bahati mbaya, ni kwamba Kiongozi alilitizama Taifa na akatuhamasisha kupiga juhudi kuelekea kule wananchi wetu wanapaswa kuwa, nikizungumza kwa nahau, kule kwenye nchi ya maziwa na asali. Leo hii fikra za Mwenyekiti si jambo tena, inaweza isiwe kama kipindi kile cha zamani, lakini sidhani kama Mwenyekiti anapewa heshima yake kama Kiongozi. Kuhusu ubadhirifu wa mali za umma, akaja na falsafa ya “kujivua gamba”, hii imeshindwa kabisa na kubaki kuwa mzaha, wana CCM hawakusimama bega kwa bega na Mwenyekiti wao. Kushindwa kwa falsafa hii kukapelekea pia kushindwa kutoa msukumo uliostahili wa kushughulikia ubadhirifu katika serikali na vyombo vyake.

Pili, ni Mchakato wa Katiba, huu umekuwa ni dhihaka kwa watanzania. Mwenyekiti wa CCM ambaye pia ndiye Mkuu wa Nchi alianzisha mchakato wa kuandikwa Katiba mpya kwa maslahi ya Taifa la Tanzania na Wananchi wake. Nini kilitokea katika kusimamia fikra yake hii adhimu na adimu kwa Taifa letu? Mzaha kabisa. Wako waliomhoji, ninaposema kumhoji simaanishi katika namna ya heshima ya kutaka taarifa au maelezo kutoka kwa Kiongozi wako, bali katika namna ya kiburi, dharau na ujuvi usio na tija kwa CCM na kwa Taifa.

Kilichotokea ni Mwenyekiti kukosa kuungwa mkono katika CCM katika jambo ambalo lililokuwa na maslahi kwa Taifa. Naikumbuka dhamira yake, nayakumbuka maono yake, nayasoma maandiko yake, nasikiliza hotuba zake, kwa hakika kilichokuja kuwa Katiba Inayopendekezwa hakiakisi dhamira ile ya awali. Hapa CCM lazima mjirekebishe, na iwe sasa na si baadaye, na mfanye upesi maana mkichelewa chelewa mtakuta mtoto si wenu. Ile tabia ya ninyi kulalama kila kona ya nchi huku mkiwasema watendaji wa serikali muiache, ninyi hampaswi kulalama, mnapowalaumu kwanini hili na lile halijatokea na wao wanawashangaa ninyi ambao mko wengi bungeni na mmeshika madaraka ya serikali, mnapaswa kutoa uongozi.

Kitu kibaya kabisa ni pale ambapo Kituo cha Demokrasia (TCD) kilipopiga hatua ya kuwa na “Makubaliano na Rais” juu ya kuokoa mchakato wa Katiba na kutoka na mapendekezo ya kutuvusha katika Uchaguzi Mkuu wa 2015 na CCM ikapuuza juhudi hii kubwa. Ninyi mnajua CCM iliwakilishwa na Kiongozi wa juu kabisa, Makamu wa Mwenyekiti, Mhe. Phillip Mangula, na yeye hajawahi kukana kuwa sehemu ya mchakato wa TCD, haipendezi pale ambapo Makamu wa Mwenyekiti hajakana matokeo halafu Katibu wa Itikadi na Uenezi aje aseme chama hakiko huko. Vitendo kama hivi Wananchi na wanachama wanavitizama kwa ukaribu sana, vitendo vinavunja mioyo ya Wananchi na wanachama.

Leo ni tarehe 24 Mei, kama CCM haitachukua uamuzi wa haraka kutoa uongozi katika Mchakato wa Katiba na Uchaguzi Mkuu, hii haitakuwa ishara nzuri ya chama kuimarika na kukua kiuongozi. Hebu tufuatilia kalenda hii, Tume ya Uchaguzi imesema itamaliza kuandikisha wapiga kura Julai 16, kisha litafuata zoezi ya uhakiki wa orodha kwa mkoa wa Dar es Salaam na mikoa mingine itakuwa imemaliza au inamalizia zoezi la uhakiki. Ikumbukwe pia kwa desturi Bunge huvunjwa mwezi wa Julai, na imekuwa desturi kwamba kampeni za uchaguzi mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani huanza kwenye tarehe 20 Agosti mpaka siku ya uchaguzi ambayo huwa wiki ya mwisho ya mwezi Oktoba.

Mpaka leo, hakuna mswada wowote wa kurekebisha Katiba ya Mwaka 1977 ambao kuna fununu au ambao imejulikana kwamba utapelekwa Bungeni ili kutekeleza “Makubaliano ya Rais na TCD”. Sitaki kusema kwamba tunakwenda kwenye uchaguzi mkuu bila marekebisho ya Katiba ya Mwaka 1977 kwa maana hata si kila dalili ya mawingu huleta mvua.

Iko bayana kwamba hatuwezi kufanya kura ya maoni mwaka huu, kwa kalenda niliyoieleza hapo juu, Kura ya Maoni inataka siku 30 za kampeni, kati ya leo na Oktoba hakuna siku 30 za bure ambazo hazitaingilia ratiba ya uchaguzi mkuu. Katika hili lazima CCM ioneshe uongozi, mkishindwa katika hili, mimi nitaendelea kupenda misingi ya kuanzishwa CCM ila heshima ya viongozi wetu katika chama na chama kama taasisi itakuwa inakaribia ukingoni. Tusifike huko.

Viongozi wetu, wenye dhamana katika CCM nawaombea mkaongozwe na hekima ya kiMungu. Mkawatazame viongozi wenye nia ya kushika hatamu ya Taifa letu kwa macho ya kiMungu na si vinginevyo.

Mkifanya maamuzi mabaya, mtaivuruga CCM, wanachama na watanzania watahuzunika sana, mtatuachia matatizo, leo hii sura ya CCM haijatukuka katika kiwango chake, watu wetu wana maswali zaidi kuliko majibu.

Nihitimishe kwa kusemea siasa za makundi CCM, wala tusijaribu kujitoa ufahamu, Makundi yalitetemesha CCM Mwaka 1995 bahati nzuri alikuwepo Mwalimu Nyerere akasaidia. Makundi yalitikisa chama mwaka 2005 na bahati mbaya athari zake ziko hata leo. CCM haiwezi kumudu mwendelezo wa siasa za makundi zisizo na tija, uzoefu unaonesha CCM inadhoofika kutokana na makundi haya.

Wana CCM wanapaswa kuchagua hivi leo kwamba watakitazama chama na kukiimarisha ama sivyo wana CCM waamue kufuata uelekeo wa siasa za mihemko ya makundi na wale wote watumiao mbinu mbaya za makundi ambayo mwishowe yatakivuruga Chama cha Mapinduzi.

Saturday, May 16, 2015

SERIKALI IKISEMA “NDIYO” UJUE KUNA SABABU YA KUSEMA HAPANA


Pale tunapokuwa na maswali mengi zaidi kuliko majibu na hekaya za mbio za sakafuni

Ni dhahiri sasa kwamba serikali imejipambanua moja kwa moja kwamba inaunga mkono Katiba Inayopendekezwa. Serikali imekwenda mbali zaidi na kutoa maelekezo kwa wananchi kwamba wakati ukifika waipigie kura ya “Ndiyo” Katiba Inayopendekezwa. Huenda mnashtuka, ndiyo, kwani hamkufuatilia Sherehe za Miaka 51 ya Muungano wetu mwezi uliopita. Shamra shamra na jumbe za maadhimisho zilijinasibu na hamasa ya kuipigia kura ya ndiyo Katiba Inayopendekezwa. Ilikuwa bayana kwamba haikuwa bahati mbaya, maadhimisho ya Muungano ni sherehe za kitaifa na zinaandaliwa, kuratibiwa na kuendeshwa na serikali, kwa mwenzangu na mimi ujumbe ulifika bayana kabisa.
Labda nirejee msingi wa utawala wa nchi yetu Tanzania, Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 1977 Toleo la 2005 na ndio Katiba inayotumika sasa inasema katika Ibara yake ya 8 inasema “Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni Nchi inayofuata misingi ya demokrasia na haki ya kijamii, na kwa hiyo - (a) wananchi ndio msingi wa mamlaka yote, na Serikali itapata madaraka na mamlaka yake yote kutoka kwa wananchi kwa mujibu wa Katiba hii; (b) lengo kuu la serikali litakuwa ni ustawi wa wananchi; (c) Serikali itawajibika kwa wananchi; (d) wananchi watashiriki katika shughuli za Serikali yao kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii”.
Wananchi ndio msingi wa mamlaka yote, maneno haya ni maneno mazito kabisa, na kwa lugha nyingine, cheo kikubwa kabisa cha msingi katika Taifa letu ni raia (citizen), huyu ndio mwananchi mtanzania. Imesemwa pia, kwamba “Serikali ni watu” na kwa hakika watu wenyewe ndio kwa ujumla wao huitwa raia wa Jamhuri ya Muungano, na wananchi wa Taifa letu.
Serikali hupaswa kutenda sawasawa na matakwa ya watu yanayozingatia maslahi mapana ya Taifa letu. Sifa kubwa ya serikali bora tangu kuasisiwa kwa Taifa letu imekuwa ni ile ambayo ni sikivu kwa wananchi. Usikivu huu wa serikali sio ni matokeo ya utashi pekee, la hasha, bali ni msingi ambao sisi kama Taifa tumekubaliana kuujenga na kuuweka katika Katiba kwamba “Serikali itapata madaraka na mamlaka yake yote kutoka kwa wananchi kwa mujibu wa Katiba hii pamoja na Serikali itawajibika kwa wananchi”
Unapoanza kuona serikali inatenda lwake, mbali na wananchi wanataka nini, tunapaswa kujihoji tunakotoka, tuliko na tunakokwenda kwa maana ya namna tunaishi na kusimamia misingi muhimu ya Taifa letu.
Sisi kama Taifa tumekubaliana kwa pamoja kwamba tutaandika Katiba Mpya na ili kuhitimisha mchakato wa huu, sisi raia tutaamua kama ipite ama isipite kwa kuifanyia uamuzi wa Kura ya Ndio au Hapana. Kifungu cha 35 cha sheria ya Kura ya Maoni kimeliweka sharti hili bayana kabisa. Kila raia ana haki ya kuamua ama apige kura ya NDIO au kura ya HAPANA, sisi raia na taasisi zetu za kiraia vikiwemo na vyama vya siasa na taasisi za kidini tunashiriki kujadiliana kwa hoja na sababu. Kuna maeneo tunakubaliana na kuna maeneo tunahitaji mjadala zaidi, na tunaendelea kufanya hivyo.
Wajibu wa serikali katika mchakato huu ni uwezeshwaji, uraghibishi au “facilitation”, na ndio maana kwa mujibu wa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba na Sheria ya Kura ya Maoni serikali kwanza ilituundia Tume ya Katiba, kisha serikali ikatuundia Bunge Maalum na hatimaye serikali kupitia Tume ya Taifa ya Uchaguzi itatuendeshea kura ya maoni. Hakuna wajibu mwingine kisheria ambao serikali imepewa juu ya mchakato huu isipokuwa kuuwezesha kifedha, kwa kutoa rasilimali watu na vitendea kazi kila inapobidi.
Wakati wa Bunge Maalum, kidogo serikali ilijisahau, ikajikuta inapanga na kupangua hoja na kidogo kidogo tukaanza kuona kumbe viongozi wetu katika serikali wana msimamo katika mchakato huu. Mimi sina tatizo la kimsingi kama viongozi wetu wa kuchaguliwa wakiwa na msimamo na hii ni kuanzia kwa Mhe. Rais, Mawaziri, Wabunge, Madiwani na wenyeviti wa serikali za mitaa na vitongoji. Hawa najua tunaweza kuhojiana nao kwa hoja, sababu na ushahidi na nina uhakika inapokuja kwenye suala la maoni ya Katiba Mpya, wananchi nao wanajua walisema nini, kwahiyo sina shaka.
Tatizo langu ni kuingiza Serikali jumla jumla, hilo ni kosa, ni kosa kubwa sana, na ndio maana nahoji, Kama serikali ikisema NDIO nani wa kupinga? Ninapata moyo mkuu wakati huu kwasababu najua viongozi wetu wa kisiasa wengi wao wana lao jambo na wanatumia kila mbinu kupitisha masuala ambayo yatalinda maslahi yao. Mbinu hizi wanazotumia viongozi wetu wa kisiasa zinajumuisha kuitumia “machinery” au taasisi ya serikali kwenye kupenyeza ushawishi wao wa kutafuta kura za NDIO, hilo ni kosa.
Mimi kama raia, nasema HAPANA kwa tabia hii isiyofaa, serikali inapaswa kutokuwa na upande au “neutral” na nitoe rai kwa wanasiasa kuacha kutumia “machinery” ya serikali kwa manufaa binafsi, ni makosa makubwa. Na kama tabia hii itaendelea mimi, hata kama nitabaki peke yangu, nitaendelea kuikemea kuwa ni mbaya na isiyofaa na nitaongeza jitihada za kuwaeleza watanzania kwamba Katiba Inayopendekezwa imelinda viongozi na imepora haki za wananchi.
Leo niendelee na uthibitisho wa namna ambavyo Katiba Inayopendekezwa inawalinda viongozi na ndio maana wanaipigia chapuo. Usikubali ee mwananchi, Katiba Mpya Bora itatusaidia kudhibiti matumizi mabaya ya baadhi ya viongozi wetu.
Utolewa, usimamizi, uhifadhi na udumishwaji wa haki za binadamu ni jukumu la serikali pamoja na umma wa watanzania. Haki za binadamu zikichezewa, watu wetu wataendelea kunyanyaswa pasina heshima ya utu wao, kuwa mafukara katika nchi yao wenyewe yenye utajiri wa kila namna. Ili kuhahakisha haki za binadamu zinatunzwa, zinatolewa, zinahifadhiwa, zinalindwa na kuheshimiwa na watu na kwa watu wote, Rasimu ya Katiba Mpya Toleo la Pili ijulikanayo kama Rasimu ya Warioba iliweka masharti yafuatayo;-
Ibara ya 210(1) inahusu Kazi na Majukumu ya Tume ya Haki za Binadamu, “(i) kutembelea magereza, vituo vya polisi au mahali penginepopote ambapo mtu au watu wanazuiliwa kwa madhumuniya kutathmini na kukagua hali za watu anaozuiliwa katikasehemu hizo na kutoa mapendekezo yatakayowezeshakurekebisha kasoro zilizopo;
(j) kutoamapendekezoyanayohusiananasheriailiyokwi shatungwa au inayokusudiwa kutungwa, kanuni, aumambo ya kiutawala ili kuhakikisha zinakidhi
viwango vyakimataifa na kikanda vya haki za binadamu;
(k) kuwasilisha taarifa na maoni huru kwenye vyombo na taasisiza kimataifa na za kikanda kuhusu hali ya haki za binadamunchini pale inapobidi;
(l) kuihamasisha Serikali kutia saini na kuridhia mikataba aumakubaliano ya kimataifa yanayohusu haki za binadamu,kufuatilia na kutathmini utekelezaji wa haki za binadamu zilizomo kwa mujibu wa Katiba hii, Katiba za NchiWashirika, sheria za nchi na mikataba au makubaliano yakimataifa ambayo Jamhuri ya Muungano inawajibika nayo; na
(m) kwa kupitia Serikalini, kushirikiana na wawakilishi waUmoja wa Mataifa, Mashirika ya Umoja wa Mataifa, Umojawa Nchi za Afrika, Jumuiya ya Madola na taasisi nyinginezenye mahusiano baina yao, miongoni mwao au ya kikanda na taasisi za nchi nyingine katika maeneo ya hifadhi naukuzaji wa haki za binadamu”.
Ibara ya 210(2) ikaweka Masharti yafuatayo;- “Tume ya Haki za Binadamu itakuwa na mamlaka maalum kama ifuatavyo: (a) kumuita mtu yeyote mbele ya Tume na kumtaka awasilishembele yake nyaraka zozote, kumbukumbu au kitu chochotekilicho katika mamlaka yake kinachohusiana na jambolinalochunguzwa na Tume; (b) kumtaka mtu yeyote kutoa taarifa anayoifahamu kwa Tumejuu ya jambo linalochunguzwa na Tume; (c) kusababisha mtu yeyote anayekiuka maagizo au taratibu zaTume kufunguliwa mashtaka ya jinai mahakamani”.
Masharti haya yote yaliyokuwamo kwenye Rasimu ya Warioba yamefutwa na hayamo katika Katiba Inayopendekezwa. Najiuliza dhamira ya waandishi wa Katiba Inayopendekezwa ilikuwa ni ipi? Na Najiuliza dhamira ya Serikali kutulazimisha kupigia Kura ya NDIO kwa Katiba Inayopendekezwa ilhali ikijua kuna mapungufu yote hayo ni ipi.
Mwisho kabisa nitoe RAI kwa Tume ya Uchaguzi, kwamba tarehe ya Kura ya Maoni ni jambo linalopaswa kuwa bayana, tusigeuze tarehe ya Kura ya Maoni kama siku ya kurudi Masiha, kwa maana haijulikani siku wala saa. Sifa moja kubwa ya utawala bora na wenye ufanisi ni “predictability” hali ya kuwa bayana na mambo ya baadaye.
Leo ni tarehe 17 Mei 2015, bado tunaandikisha wapiga kura mpaka mwezi wa saba. Bunge huenda litavunjwa mwezi wa saba na baraza la wawakilishi mwezi wa nane. Kampeni za Uchaguzi Mkuu ni zaidi ya siku 60, kwa maana kwamba kampeni zitaanza mwishoni mwa mwezi wa Agosti na kumalizika wiki ya mwisho ya Mwezi Oktoba. Sasa kweli kabla ya Uchaguzi Mkuu unaona hapo Kura ya Maoni ikifanyika? Haiwezekani! Haya tuangalie marekebisho ya Katiba ya Mwaka 1977 ili tuvuke Uchaguzi Mkuu bila tashwishwi, mpaka leo hakuna mswada wa sheria wa marekebisho ya Katiba na Bunge la bajeti litaendelea hadi karibu na mwisho wa mwezi wa Juni.
Je ukitizama unaona nini mbele? Ninaona muda hautoshi, ninaona busara inahitajika zaidi hasa kuhusu Kura ya Maoni na Uchaguzi Mkuu ni lazima. Tafakari na tujadiliane.
WASAMBAZIE NA WENGINE na USISAHAU ku-LIKE Humphrey Polepole

Sunday, May 10, 2015

TUJIKUMBUSHE HOJA YA SHIRIKISHO LENYE SERIKALI TATU


Kumekuwa na kuchanganya mambo katika majadiliano yetu katika kila kona juu ya suala la shirikisho ambalo limetajwa katika ibara ya kwanza ya Sura ya Kwanza ya Rasimu ya Warioba na suala la muundo wa serikali tatu katika Jamhuri ya Muungano lililomo katika Sura ya Sita ya Rasimu ya Warioba. Imefikia hatua sasa wapo wanaodhani ukizungumzia shirikisho maana yake ni serikali tatu na ukizungumzia serikali mbili umekataa shirikisho. Mtizamo huo sio sahihi kama nitakavyoeleza baadaye.

Pili inaelekea kuwa wapo watu ambao wana mzio (allergy) na neno “Shirikisho” na hivyo kulichukia na kulipa maana hasi ambayo siyo sahihi. Kwa watu hao kwao neno shirikisho wamelipa maana ya kubuni ya kifo cha Muungano. Mtizamo huo  sio sahihi na ni mtizamo potofu kabisa. Hakuna uhusiano wa moja kwa moja wa kufa kwa Miungano duniani na dhana ya shirikisho. Kwani ipo Miungano ya Serikali moja ambayo ilikufa katika kipindi kifupi sana kama ule wa Misri na Syria na ipo Miungano ya shirikisho ambayo inadumu mpaka leo kama vile Ethiopia, Nigeria, Jamhuri ya Shirikisho la Ujerumani, Marekani na India.

Tatu kuna dhana potofu kuwa shirikisho na muungano wa serikali tatu unaopendekezwa katika Rasimu ya Warioba utahamasisha utaifa wa Tanganyika. Dhana hiyo pia ni potofu kwani zipo nchi zenye muungano wa serikali moja kwa sababu ya kulazimisha kufuta utambulisho wa upande mmoja wa Muungano huo leo baada ya zaidi ya miaka hamsini ya Muungano wao upande ule ambao ulizikwa utambulisho wake unadai sasa utaifa wake. Nchi hiyo ni Jamhuri ya Cameroon ambayo ni muungano wa serikali moja  wa iliyokuwa “French Cameroon” na “British Cameroon” zilizoungana mwaka 1961. Hali hiyo imechambuliwa vizuri sana na  Verkijika G. Fanso katika makala yake “Anglophone and Francophone Nationalism in Cameroon” [The Round Table (1991) 350, 281 – 296] na pia katika makala ya Piet Konings na Francis G. Nyamnjoh  “The Anglophone Problem in Cameroon” [The Journal of Modern African Studies, 35, (1997), 207 – 229]

Nilianza kwa kusema kuwa suala la shirikisho na suala serikali tatu hayahusiani ingawa yanaingiliana. Mjadala wa aina ya Muungano wa Tanzania umekuwa na ubishani mkubwa kwa miaka mingi. Je Muungano huu ni serikali moja yaani “Unitary State” au ni wa shirikisho yaani “Federation”?.Wapo wanazuoni maarufu wa sheria hapa Tanzania na wanasiasa wa Chama cha Mapinduzi (CCM) ambao wamechambua Muungano huu wa sasa wa serikali mbili na kuhitimisha kuwa ni wa mfumo wa Shirikisho. Hii ina maana hata sasa tuna shirikisho la serikali mbili. Kwa hali hiyo basi Rasimu ya Warioba ilipendekeza tutoke kwenye shirikisho la serikali mbili la sasa na kwenda katika shirikisho la serikali tatu.

Miongoni wa wanazuoni hao ni Profesa P.B. Srivastava ambaye alifundisha sheria za Katiba (Constitutions and Legal Systems of East Africa) na Sheria za Utawala (Administrative Law) katika Kitivo cha Sheria cha Chuo Kikuu cha Dar es Salaam katika miaka ya 1980 ndiye aliyechambua kwa kina muungano wa Tanzania na kuhitimisha kuwa ni wa aina ya shirikisho katika Mhadhara wake wa Kiprofesa (Professorial Inaugral Lecture) wake alioutoa Machi 1982 iitwayo “The Constitution of the United Republic of Tanzania 1977:Some Salient Features – Some Riddles”.

Miaka minane baadaye, yaani mwaka 1990,  msomi mwingine Profesa Issa Gulamhussein Shivji, ambaye kwa miaka yote kabla ya hapo alikuwa akijihusisha na Sheria za Kazi (Labour Law) alitoa Mhadhara wa Kiprofesa (Professorial Lecture)  wake uitwao “The Legal Foundation  of the Union in Tanzania’s Union and Zanzibar Constitutions” naye alihitimisha kuwa Muungano wa sasa wa Tanzania ni wa mfumo wa shirikisho kama nitavyofafanua baadaye.

Wanasiasa wa CCM ambao walisema kuwa Muungano wa sasa ni shirikisho ni Alhaj Aboud Jumbe Mwinyi aliyekuwa Makamu Mwenyekiti wa CCM, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi. Msimamo huo uliungwa mkono na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika hotuba iliyotolewa na aliyekuwa Waziri Kiongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Brigedia – Jenerali Ramadhan Haji Faki mwaka 1983 alipojibu hoja ya ushauri kuwa Waziri Mkuu wa wakati huo Edward Moringe Sokoine aliposhauri Chama cha Mapinduzi kuwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano ina mamlaka juu ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar. [Zanzibar Government: A Reaction to Prime Minister Ndugu Sokoine’s Advice to the Party to Restructure the Government given to the Party and Government Leaders Tabled by the Chief Minister to the House of Representatives, Zanzibar Printing Press, 1983, p. 5). Msimamo huo pia uliungwa mkono na aliyewahi kuwa Mwanasheria Mkuu wa SMZ, Wolfgang Dourado.

Msimamo huo wa Mzee Jumbe kuwa muundo wa Muungano ni shirikisho ulileta kuchafuka kwa hali ya hewa wakati wa mjadala wa Mabadiliko ya Tano ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano na Mabadiliko ya Katiba ya Zanzibar. Pamoja na Mwasisi wa Muungano na Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere kutofautiana na Mzee Jumbe, kama ilivyoelezwa katika Randama ya Rasimu ya Warioba katika ukurasa wa tatu, nanukuu:

“Kwa mujibu wa kumbukumbu za kikao cha halmashauri ya Taifa ya Chama cha Mapinduzi katika mkutano wa tano ambao ulikuwa maalumu uliofanyika Dodoma Januari 24-30, 1984, Mwalimu Nyerere alitamka kuwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ukiangalia kwa jicho la Zanzibar ni wa Shirikisho lakini ukiangalia kutoka Tanzania Bara ni serikali moja. Mwalimu alikuwa akimjibu Makamu Mwenyekiti wa CCM, Makamu wa Rais na Rais wa Zanzibar Sheikh Aboud Jumbe Mwinyi aliyesema kuwa Muungano wa Tanzania umeunda shirikisho (Federation) na sio serikali moja (Unitary State).

Mfumo wa Shirikisho unaopendekezwa katika Rasimu ya Warioba unaendeleza hadhi ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuwa ni Nchi na ni Dola moja lenye mamlaka kamili yenye serikali tatu, shirikisho hili linatokana na muungano wa hiari wa Tanganyika na Zanzibar ambazo zilikuwa Jamhuri zenye mamlaka kamili kabla ya kuungana tarehe 27 Aprili 1964”

Msimamo huo wa Mwalimu Nyerere kuwa kwa upande wa Zanzibar Jamhuri ya Muungano ya Muungano ina sura ya shirikisho inafanana kwa kiasi fulani na uchambuzi wa mtaalam nguli Mwingereza wa masuala ya katiba Professor S.A. de Smith ambaye katika kitabu chake kiitwacho Constitutional and Administrative Law, 2nd Edition, 1973, p.33 anasema kwamba:

“Tanzania is part federation, since Zanzibar has exclusive fields of competence both in theory and in practice, but for political reasons the term ‘federal’ does not appear in the constitution and in as much as it implies a degree of disunity as well as diversity.”

Kwa kiswahili akimaanisha “Tanzania kwa sehemu ni shirikisho kwa sababu Zanzibar ina mamlaka yake kamili ya ndani kinadharia na kivitendo lakini kwa sababu za kisiasa neno shirikisho halionekani katika Katiba huku hali hii ikionesha kiwango cha utengano pamoja na utofauti” (Tafsiri ni yangu).

Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere katika kitabu chake cha “Uongozi wetu na Hatima ya Tanzania” katika ukurasa wa 15, alipata kusema “Nchi mbili zinapoungana na kuwa Nchi Moja mifumo ya kawaida mifumo ya miundo ya Katiba ni miwili: Kwa mfumo wa kwanza kila nchi itafuta serikali yake, na Nchi mpya inayozaliwa itakuwa ni nchi moja yenye serikali moja.

Katika mfumo wa pili kila nchi itajivua madaraka fulani ambayo yatashikwa na serikali ya shirikisho, na itakuwa na serikali ambayo itakuwa na mamlaka juu ya mambo yaliobaki. Mambo yatakayoshikwa na serikali ya shirikisho ni yale ambayo yakibaki katika mamlaka ya nchi zilizoungana basi nchi hizo huwa huru. Shirikisho halisi la nchi mbili litakuwa ni nchi moja yenye serikali tatu, Serikali ya shirikisho na serikali mbili za zile nchi mbili za awali zilizoungana kuzaa nchi mpya moja.”

Muundo wa Shirikisho, ambao ni tofauti na muundo wa serikali moja. Katika muundo huu, nchi zinapoungana kunakuwa na ngazi mbili za serikali, yaani serikali ya muungano au shirikisho na serikali za washirika. Serikali ya Muungano inakuwa na mamlaka kwa masuala yote yaliyokubaliwa kuwa ya muungano, wakati serikali za washirika zinakuwa na mamlaka ya kikatiba kushughulikia mambo yote yasiyo ya muungano.

Sababu nyingine ya kuendelea kupendekeza muundo wa shirikisho lenye serikali tatu ni uhalisia kwamba Muundo wa Shirikisho utaendelea kuhifadhi asili, taswira na hadhi ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika jumuiya ya kimataifa kwa mujibu wa Kifungu cha 2 cha Mkataba wa Montevideo wa mwaka 1933 unaohusu Haki na Majukumu ya Nchi (the Montevideo Convention on Rights and Duties of States) unaosema na ninanukuu “the federal state shall constitute a sole person in the eyes of international law” inayomaanisha nchi yenye muundo wa shirikisho katika sheria za kimataifa ni nchi na dola moja.

Katika mfumo huu, kwa kawaida mamlaka ya mwisho au mamlaka kamili (sovereignty) yanabaki katika serikali ya shirikisho. Kama nilivyosema, utambulisho wa nchi katika mahusiano ya kimataifa na vyombo vya ulinzi na usalama hubaki katika serikali ya shirikisho. Sifa nyingine ya shirikisho ni kuwa mwananchi anatawaliwa na serikali mbili ilihali katika muundo wa muungano wa serikali moja mwananchi anatawaliwa na serikali moja pekee. Muungano wa Tangannyika na Zanzibar siku zote umekuwa na sura mbili. Kwa wananchi wa Zanzibar wamekuwa katika shirikisho tangu mwaka 1964 kwa sababu wanatawaliwa na serikali mbili (serikali ya muungano na serikali ya Zanzibar). Kwa upande wa Tanzania Bara kuna sura ya muungano zaidi kwa sababu kuna serikali moja kwa maana serikali ya Tanzania Bara au Tanganyika haipo.

Sababu nyingine ya kupendekeza muundo wa shirikisho ni kukuza demokrasia kwa maana ya kutoa mamlaka zaidi kwa nchi washirika kujiamulia mambo yao wenyewe. Hii inatekeleza madai ya miaka mingi ya Zanzibar kuwa na Shirikisho la Serikali Tatu tangu wakati wa Mzee Aboud Jumbe Mwinyi na baada ya hapo ambalo liliungwa mkono na watu wengi akiwemo Profesa Issa Gulamhussein Shivji. Hoja hiyo ya Prof. Issa Shivji kuunga mkono madai ya Zanzibar ya kuanzishwa kwa mfumo wa shirikisho lenye serikali tatu limo katika kitabu chake kiitwacho “Pan-Africanism or Pragmatism?: Lessons of the Tanganyika – Zanzibar Union (2008 ukurasa 250 anaposisitiza kuwa;

“A demand for a three government federation, greater autonomy for Zanzibar, reduction in union matters, from Zanzibar was a demand for the right to self-determination, a democratic demand” [ yaani, madai ya shirkisho la serikali tatu na kupunguzwa kwa mambo ya muungano yanayotolewa na Zanzibar ni madai ya haki ya kujiamulia mambo yao na ni haki ya kidemokrasia Uk. I.G. Shivji, Pan Africanism or Pragmatism? Lessons of Tanganyika- Zanzibar Union,2008, P. 250]
 
Pia, Chini ya mfumo wa Muungano wa Shirikisho, ugawaji wa madaraka huwekwa kwenye Katiba kiasi kwamba katika hali ya kawaida serikali ya muungano haiwezi kuingilia na kunyang’anya madaraka ya serikali za washirika bila ya kufuata utaratibu uliyowekwa kwenye Katiba. Nchi ambazo zimeimarika katika mfumo huo ni pamoja na Marekani, Kanada, India, Brazil, Ujerumani, Uswisi, Australia, Nigeria na Ethiopia. Mfumo wa Shirikisho unawezesha nchi washiriki kuwa na nguvu kubwa ya kushughulikia maslahi ya pamoja huku kila moja ikiwa na mamlaka ya kushughulika masuala yasiyo ya pamoja. Mfumo huu unawapa washirika wa Muungano fursa ya kuhifadhi utambulisho wao wa kihistoria.

Sababu nyingine muhimu ya kupendekeza muungano wa shirikisho la serikali tatu ni kuweka bayana mamlaka tatu ndani ya Jamhuri ya Muungano zilizobainishwa na Katiba ya sasa ya Jamhuri ya Muungano  ya Mwaka 1977 katika Ibara ya 4, 34, 64 na 102. Mamlaka hizo ni Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Serikali ya Zanzibar na Serikali ya Tanzania Bara.  Hoja hii inatiliwa nguvu na Msomi Maarufu wa Masuala ya Katiba Professor Srivastava, kwamba:

 “The United Republic envisages a triangular system with Tanzania Mainland and Zanzibar forming two corners of the base and the United Republic constituting the vortex. Accordingly, there are three jurisdictional areas territory-wise and subject-wise for the operation of governmental powers, both legislative and executive, which necessitate existence of three governments, namely, Government of United Republic, Government of Tanzania Mainland and Government of Zanzibar corresponding to three jurisdictions.


[Tafsiri yangu: Jamhuri ya Muungano ni mfumo wa serikali tatu, Tanzania Bara na Zanzibar zikiwa ni nguzo za pembeni na Jamhuri ya Muungano ikiwa ni kilele chake: Hivyo, kuna mamlaka tatu kieneo na kimatumizi ya madaraka ya kiserikali, kibunge ambayo yanalazimu kuwe na serikali tatu: yaani serikali ya Jamhuri ya Muungano, Serikali ya Tanzania Bara na Serikali ya Zanzibar] { B. P. Srivastava, 'The Constitution of the United Republic of Tanzania 1977 - Some Salient Features, Some Riddles' Eastern Africa Law Review 11-14 (1978-81}, 73-127, at pp.79-80.}