Saturday, May 23, 2015

TAFAKURI YANGU YA UONGOZI NA MCHAKATO WA NDANI WA CCM KUPATA WAGOMBEA: TUJIREKEBISHE



Mungu ametupa akili, busara na hekima, kisha akatupa ufahamu, fikra na uwezo wa kuunda taasisi ili zitusaidie kuturatibu, kutuwezesha na kutusaidia. Kwa ufahamu aliotupa Mungu, akatuwezesha kuchagua na kuteua kutoka miongoni mwetu watu wa tofauti, watu wasiojipenda wenyewe, watu wenye uwezo mkubwa na maono, watu wapole, wenye uhalali katika jamii wa kuonya na kukemea ili hawa wawe viongozi wetu.

Uongozi ni dhamana, ni jukumu zito, mtu uongozi hupewa na watu, hubarikiwa na hata kulazimishwa, uongozi huwa hautafutwi kwa udi na uvumba. Katika dini zote na jamii za watu katika historia viongozi walitengenezwa, hata wale waliozaliwa katika mnyonyororo wa uongozi iliwapasa kulelewa kiuongozi. Ilimpasa mtu awaye kiongozi, kuhakikisha kwamba anawaleta watu wake pamoja, masikini na matajiri, wakulima na wafanyakazi, wafanyabiashara wadogo na wakubwa.

Kiongozi anapaswa kuwa msingi imara wa umoja wa kitaasisi, jamii na Taifa kwa ujumla. Kiongozi anayeanza na mpasuko na si umoja, kiongozi anayeanza na chuki na si upendo, viongozi wanaoanza na makundi na si taasisi kwanza, tafsiri yake si njema, si afya na ni muendelezo wa nyufa katika taasisi yoyote ile.

Chama cha Mapinduzi (CCM) hivi karibuni kitatoa utaratibu na mchakato wa kumpata mgombea wa Urais kupitia CCM. Tukumbuke tena, CCM ndio chama kilichopo madarakani sasa, hivyo inapaswa kuonesha mfano, CCM inapaswa kuwa kioo, najua CCM imejikwaa wakati mwingine kwa makusudi na wakati mwingine kwa bahati mbaya. Sifa kubwa ya uongozi thabiti ni kuonesha uongozi pale ambapo watu ndani ya taasisi au kwa ujumla Taasisi inapojikwaa. Kuonesha uongozi kunaweza kuwa katika namna nyingi, mojawapo ni kwa hali yoyote kuukumbatia ukweli pasina kuathiri menejimenti ya siasa

Uongozi ni kuonesha kutokuvunjika moyo, kutokukata tamaa, kujikwaa sio kuanguka, na kama CCM imetetereka bado inaweza kuamka tena na kuthibitishia umma wa watanzania kwamba misingi ya kusimamia maadili na miiko ya viongozi bado iko imara kama ilivyo misingi ya CCM ambayo kwayo iliasisiwa.

Labda nitolee mfano wa mambo kadhaa ambayo kwa makusudi baadhi ya wana CCM wamesaidia kuteteresha CCM. Mosi, namna ambayo chama ambacho ndio kimeshika mamlaka ya nchi na serikali kimeshughulikia masuala ya ubadhirifu wa mali ya umma, kumekuwa na tuhuma kadhaa wa kadhaa katika miaka 10 iliyopita. Tumeona uwajibikaji, lakini CCM ingeweza kufanya vizuri zaidi ili kurudisha imani ambayo inaonekana dhahiri kutetereka miongoni mwa wananchi. Uongozi wa CCM unapaswa kuwa mkali zaidi kwa wale wanaokwenda kinyume na misingi ya kuanzishwa kwa CCM. Urafiki ni jambo jema, lakini misingi ya CCM inapaswa kuwa juu ya urafiki wakati wowote.

Wengi wenu, viongozi wa CCM mlikuwepo kipindi cha Mwalimu Nyerere na kwa hakika wengi wenu ni mashahidi wa namna alitenda kama Kiongozi. Hivi kuna kipindi kigumu kama miaka ya 80 mwanzoni? Kipindi kile ambacho ajira rasmi ziliporomoka kwa karibu asilimia 80, matatizo ya njaa na kutetereka kwa uchumi wa nchi. Mwalimu alikuwa mkali kweli kweli, lakini pia alikuwa kama baba, alikuwa msikivu na mpole, kama Kiongozi mkuu ndio mwenye dira, ndiye anayetupa hamasa kupiga makasia katika Bahari iliyochafuka ili tuelekee uelekeo sahihi na salama, ambaye kupitia kwake watu walipaswa kuyaona matumaini, walipaswa kuiona Tanzania njema.

Mnakumbuka vikao vya Karimjee vya kuokoa uchumi wa Taifa letu miaka ya 80 katikati, nafasi ya Mzee Kawawa ya menejimenti ya siasa au “political management” katika vikao pale hali ilipochafuka. Hali ilipokuwa tete, na hasira ziko juu, Mzee Kawawa kwa busara na hekima zake alijua namna ya kutukwamua na hali ikapoa, kisha Mwalimu akaahirisha kikao mpaka siku inayofuata, hiyo ndio ilikuwa CCM.

Leo hii nidhamu ya baadhi ya wana CCM na viongozi imeshuka, nasikia hata kuzomeana kumo katika vikao. Kuheshimia miongoni mwa viongozi ndio msingi mkubwa wa kujengeana imani na kuaminiana. Viongozi wasioaminiana, hawaheshimiani, viongozi wasioheshimiana hawapendani, na viongozi wasiopendana hawazungumzi kwa uwazi na ukweli. Tunapofika hapo, taasisi ya chama iko mashakani, uongozi wa nchi kutoka katika chama unawekwa rehani.

Zamani ilikuwa tunasema zidumu fikra za Mwenyekiti, usemi huu haukuwa wa bahati mbaya, ni kwamba Kiongozi alilitizama Taifa na akatuhamasisha kupiga juhudi kuelekea kule wananchi wetu wanapaswa kuwa, nikizungumza kwa nahau, kule kwenye nchi ya maziwa na asali. Leo hii fikra za Mwenyekiti si jambo tena, inaweza isiwe kama kipindi kile cha zamani, lakini sidhani kama Mwenyekiti anapewa heshima yake kama Kiongozi. Kuhusu ubadhirifu wa mali za umma, akaja na falsafa ya “kujivua gamba”, hii imeshindwa kabisa na kubaki kuwa mzaha, wana CCM hawakusimama bega kwa bega na Mwenyekiti wao. Kushindwa kwa falsafa hii kukapelekea pia kushindwa kutoa msukumo uliostahili wa kushughulikia ubadhirifu katika serikali na vyombo vyake.

Pili, ni Mchakato wa Katiba, huu umekuwa ni dhihaka kwa watanzania. Mwenyekiti wa CCM ambaye pia ndiye Mkuu wa Nchi alianzisha mchakato wa kuandikwa Katiba mpya kwa maslahi ya Taifa la Tanzania na Wananchi wake. Nini kilitokea katika kusimamia fikra yake hii adhimu na adimu kwa Taifa letu? Mzaha kabisa. Wako waliomhoji, ninaposema kumhoji simaanishi katika namna ya heshima ya kutaka taarifa au maelezo kutoka kwa Kiongozi wako, bali katika namna ya kiburi, dharau na ujuvi usio na tija kwa CCM na kwa Taifa.

Kilichotokea ni Mwenyekiti kukosa kuungwa mkono katika CCM katika jambo ambalo lililokuwa na maslahi kwa Taifa. Naikumbuka dhamira yake, nayakumbuka maono yake, nayasoma maandiko yake, nasikiliza hotuba zake, kwa hakika kilichokuja kuwa Katiba Inayopendekezwa hakiakisi dhamira ile ya awali. Hapa CCM lazima mjirekebishe, na iwe sasa na si baadaye, na mfanye upesi maana mkichelewa chelewa mtakuta mtoto si wenu. Ile tabia ya ninyi kulalama kila kona ya nchi huku mkiwasema watendaji wa serikali muiache, ninyi hampaswi kulalama, mnapowalaumu kwanini hili na lile halijatokea na wao wanawashangaa ninyi ambao mko wengi bungeni na mmeshika madaraka ya serikali, mnapaswa kutoa uongozi.

Kitu kibaya kabisa ni pale ambapo Kituo cha Demokrasia (TCD) kilipopiga hatua ya kuwa na “Makubaliano na Rais” juu ya kuokoa mchakato wa Katiba na kutoka na mapendekezo ya kutuvusha katika Uchaguzi Mkuu wa 2015 na CCM ikapuuza juhudi hii kubwa. Ninyi mnajua CCM iliwakilishwa na Kiongozi wa juu kabisa, Makamu wa Mwenyekiti, Mhe. Phillip Mangula, na yeye hajawahi kukana kuwa sehemu ya mchakato wa TCD, haipendezi pale ambapo Makamu wa Mwenyekiti hajakana matokeo halafu Katibu wa Itikadi na Uenezi aje aseme chama hakiko huko. Vitendo kama hivi Wananchi na wanachama wanavitizama kwa ukaribu sana, vitendo vinavunja mioyo ya Wananchi na wanachama.

Leo ni tarehe 24 Mei, kama CCM haitachukua uamuzi wa haraka kutoa uongozi katika Mchakato wa Katiba na Uchaguzi Mkuu, hii haitakuwa ishara nzuri ya chama kuimarika na kukua kiuongozi. Hebu tufuatilia kalenda hii, Tume ya Uchaguzi imesema itamaliza kuandikisha wapiga kura Julai 16, kisha litafuata zoezi ya uhakiki wa orodha kwa mkoa wa Dar es Salaam na mikoa mingine itakuwa imemaliza au inamalizia zoezi la uhakiki. Ikumbukwe pia kwa desturi Bunge huvunjwa mwezi wa Julai, na imekuwa desturi kwamba kampeni za uchaguzi mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani huanza kwenye tarehe 20 Agosti mpaka siku ya uchaguzi ambayo huwa wiki ya mwisho ya mwezi Oktoba.

Mpaka leo, hakuna mswada wowote wa kurekebisha Katiba ya Mwaka 1977 ambao kuna fununu au ambao imejulikana kwamba utapelekwa Bungeni ili kutekeleza “Makubaliano ya Rais na TCD”. Sitaki kusema kwamba tunakwenda kwenye uchaguzi mkuu bila marekebisho ya Katiba ya Mwaka 1977 kwa maana hata si kila dalili ya mawingu huleta mvua.

Iko bayana kwamba hatuwezi kufanya kura ya maoni mwaka huu, kwa kalenda niliyoieleza hapo juu, Kura ya Maoni inataka siku 30 za kampeni, kati ya leo na Oktoba hakuna siku 30 za bure ambazo hazitaingilia ratiba ya uchaguzi mkuu. Katika hili lazima CCM ioneshe uongozi, mkishindwa katika hili, mimi nitaendelea kupenda misingi ya kuanzishwa CCM ila heshima ya viongozi wetu katika chama na chama kama taasisi itakuwa inakaribia ukingoni. Tusifike huko.

Viongozi wetu, wenye dhamana katika CCM nawaombea mkaongozwe na hekima ya kiMungu. Mkawatazame viongozi wenye nia ya kushika hatamu ya Taifa letu kwa macho ya kiMungu na si vinginevyo.

Mkifanya maamuzi mabaya, mtaivuruga CCM, wanachama na watanzania watahuzunika sana, mtatuachia matatizo, leo hii sura ya CCM haijatukuka katika kiwango chake, watu wetu wana maswali zaidi kuliko majibu.

Nihitimishe kwa kusemea siasa za makundi CCM, wala tusijaribu kujitoa ufahamu, Makundi yalitetemesha CCM Mwaka 1995 bahati nzuri alikuwepo Mwalimu Nyerere akasaidia. Makundi yalitikisa chama mwaka 2005 na bahati mbaya athari zake ziko hata leo. CCM haiwezi kumudu mwendelezo wa siasa za makundi zisizo na tija, uzoefu unaonesha CCM inadhoofika kutokana na makundi haya.

Wana CCM wanapaswa kuchagua hivi leo kwamba watakitazama chama na kukiimarisha ama sivyo wana CCM waamue kufuata uelekeo wa siasa za mihemko ya makundi na wale wote watumiao mbinu mbaya za makundi ambayo mwishowe yatakivuruga Chama cha Mapinduzi.

No comments:

Post a Comment