Saturday, August 29, 2015

CCM, UKAWA NA KUNG’OA MFUMO WA KIFISADI NCHINI



Wananchi wengi tunakubalina kuwa adui mkubwa wa Tanzania kwa sasa ni  ufisadi ambao ndio umekuwa chanzo kikubwa cha utajirisho wa  watu wachache  na huku ukistawisha umaskini kwa wananchi walio wengi. Baadhi ya wananchi wamekuwa na mawazo kuwa hatuwezi kupambana na ufisadi bila ya kwanza kuiondoa CCM madarakani kwani kwa maoni yao CCM ndio mfumo wenyewe wa kifisadi.  Lengo langu leo ni kutaka tutafakari usahihi wa dhana hii katika uhalisia wake ili itusaidie kuchukua hatua sahihi katika kuung’oa mfumo wa kifisadi nchini.

Kwanza, kuna haja ya kutambua ukweli kuwa rushwa na ufisadi ndiyo adui mkubwa wa maendeleo ya kweli ya nchi yetu. Ukweli huu uligundulika mapema kabisa  baada ya nchi yetu kupata uhuru pale ambapo sehemu ya tabaka la watu walioshika nafasi za uongozi baada ya uhuru kutaka kutumia nafasi zao kwa ajili ya kujitajirisha wao binafsi kwa gharama ya wananchi wenzao. Tabaka hili lililokuwa linajulikana enzi hizo kama wabenzi, ikimaanisha wamiliki wa magari ya Mercedez Benz ambayo ndio ilikuwa alama ya kuwa tajiri, liliona kuwa kushika nafasi ya uongozi katika dola ni kupata fursa ya kijitajirisha. 

Hali  hiyo ingeruhusiwa kuendelea ingewakatisha tamaa wananchi na kujenga ufa baina yao na uongozi wa nchi. Pia hali hiyo ilionekana kusaliti matumaini ya wananchi katika kupigania na kupata uhuru. Hakika hali hiyo ingeruhusiwa kuendelea  ingefanya uhuru usiwe na maana kwa wananchi. Kwa bahati nzuri uongozi wa TANU chini ya Baba wa Taifa uliligundua tatizo hilo na kuchukua hatua za kukabiliana nazo.

Ili kupambana na ufisadi uliokuwa umeanza kujengeka, mwaka 1966 , Mwalimu Nyerere baada ya kupokea changamoto kutoka kwa wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar Es Salaam waliokuwa wanaandamana, wakilalamika pamoja na mambo mengine kuwa viongozi walikuwa wanatumia nafasi zao kujinufaisha alipunguza mishahara ya  viongozi kwa kuanzia na kupunguza mshahara wake kwa asilimia ishirini. Mwaka 1967, TANU ilitangaza sera ya Ujamaa na Kujitengemea iliyokuwa inalengo la kujenga jamii yenye usawa na haki na kukomesha unyonyaji na ukupe kati ya mtu na mtu.

Miiko ya uongozi iliwekwa  ili kuhakikisha kuwa viongozi wanatumia madaraka yao kulingana na dhamana waliyokabidhiwa na si kwa faida  zao binafsi. Miiko hiyo ilidumu mpaka mwaka 1992 tulipoingia kwenye mfumo wa vyama vingi.  Baadhi ya Miiko hii bado ni sehemu ya katiba ya CCM. Ibara ya 18 ya Katiba ya CCM inazuia  kiongozi:- “(1) Kutumia madaraka aliyopewa ama kwa ajili ya manufaa yake binafsi au kwa upendeleo, au kwa namna yoyote ambayo ni kinyume cha lengo lililokusudiwa madaraka hayo. (2) Kupokea mapato ya kificho, kutoa au kupokea rushwa, kushiriki katika mambo yoyote ya magendo au mambo mengine yaliyo kinyume cha lengo lililokusudiwa madaraka hayo.” 

KUTEKWA CCM NA UFISADI

Kwa hiyo, CCM kwa asili yake na mfumo wake imeundwa kupambana na ufisadi na si kukumbatia ufisadi, hata hivyo tunajua kuwa  kwa miaka ya karibuni ufisadi umemea na kukuwa kwa kiwango kikubwa nchini. Hali hii imesababishwa kwa kiwango kikubwa na kufanikiwa kwa kundi la watu wachache lakini lenye ukwasi mkubwa lijulikanalo kama ‘mtandao’  kufanikiwa ‘kuiteka nyara’ CCM kwa kufadhili wagombea kwenye nafasi za ubunge na Uraisi.  Walioshika madaraka katika nyadhifa za uongozi walitumia nafasi hizo kulipa fadhila kwa wafadhili wao kwa njia ya mikataba minono lakini yenye athari kubwa kwa maisha ya wananchi. Ni katika kipindi hichi ndio tumeshuhudia maskandali  ya kifisadi kama vile mkataba wa Richmond, Meremeta, ukwapuaji wa fedha za EPA, n.k. Hali hii ilitokea ili ngenge la mtandao liweze kufidia gharama walizotumia kufadhili kampeni za mawakala wao kuingia madarakani. Hali hii iliimarika zaidi baada ya  uchaguzi wa 2005.

Katika uchaguzi wa mwaka huu na kama ilivyokuwa katika chaguzi za kuanzia mwaka 1995, ili kuendelea kunufaika na rasilimali za nchi kundi la mtandao, limejizatiti kwa kutumia nguvu ya hela kuingiza mawakala wao katika nafasi ya Urais. 

Hata hivyo, mara hii CCM ilifanikiwa kuzishinda  jitihada za kundi hili ‘kuiteka’na kuhakikisha kuwa mgombea wa kundi hili  katika nafasi ya Urais hateuliwi kugombea Urais kupitia chama hicho.  Jitihada hizo ndio zilisababisha mgombea wa sasa wa Urais wa Tanzania kupitia CCM, Dr. John Magufuli kuteuliwa. Sifa kubwa iliyombeba Magufuli ni kutokuwa ngenge la watu wenye fedha wanaomfadhili.  Kwa uteuzi wa Magufuli, CCM inaonyesha kuwa imejizatiti kurudi kwenye asili yake ya chama kinacho simamia maadili na miiko ya viongozi.

KUTEKWA NYARA KWA UKAWA

Baada ya kundi la mtandao kung’olewa CCM na ili liendelee kunyonya  na kufisadi rasilimali za nchi,  lilifanya jitihada kubwa kwa kutumia nguvu ya pesa kuviteka vyama vya upinzani vyenye nguvu nchini kupitia umoja wao wa UKAWA. Kwa kuelewa kuwa kundi hili linataka madaraka si kwa sababu nyingine ila kuendelea ‘kuifaidi’ Tanzania lakini kwa gharama  ya maisha ya Mtanzania wa leo na vizazi vijavyo, waasisi wa UKAWA ambao walitoa maisha yao  kuunda na kuujenga UKAWA  kama njia ya kuimarisha upinzani nchini, Dr Wilbroad Slaa na Prof. Haruna Lipumba wameamua kukaa pembeni ili kuepuka kushiriki kuingiza madarakani mfumo wa kifisadi ambao walitumia muda na maisha yao kupambana nao.

Hakika historia itawakumbuka viongozi hawa  kwa misimamo yao imara ya kupinga mfumo wa  ufisadi kokote hata kama wanufaika wa mfumo  huo watakuwa wao. Maana nafasi zao ziliwahakikishia kufaidi matunda ya mfumo huo kwa sasa na ikitokea kundi hilo likashinda uchaguzi.

KUNG’OA MFUMO WA KIFISADI

Tumeona kuwa chanzo kikubwa cha kuvurugika kwa mfumo wa maadili nchini ni ngenge la mtandao ambalo kwa kutumia nguvu ya pesa limeweza kuingiza mawakala wao kwenye nafasi za uongozi kupitia CCM. Bahati nzuri CCM wameweza kupambana na kundi hilo kwa kuzuia jitihada zake za kuendelea kuiteka nyara. Tumeona kuwa, baada ya kushindwa kundi hilo sasa limeuteka upinzani nchini kupitia UKAWA kwa kutumia nguvu ya fedha. Wananchi wameshuhudia kundi hili likigawa hela kwa makundi mbalimbali ya wananchi katika kujihakikishia wanapata uungwaji mkono ili  mgombea wao aweze kushinda Urais.


Kundi hili haliamini katika sera au itikadi yeyote ndio maana liliposhindwa CCM limehamia UKAWA  ambapo kila chama kina ilani,sera na itikadi tofauti. Hali haliwasumbui kwa maana shida yao kama wanavyosema wenyewe siyo sera bali kushika madaraka ili waendelee kuifisadi nchi.  Kwa kuhitimisha kama tunataka kung’oa ufisadi nchini, inabidi tuhakikishe kuwa kundi hili la haliingii tena kushika madaraka ya nchi.