Sunday, May 10, 2015

TUJIKUMBUSHE HOJA YA SHIRIKISHO LENYE SERIKALI TATU


Kumekuwa na kuchanganya mambo katika majadiliano yetu katika kila kona juu ya suala la shirikisho ambalo limetajwa katika ibara ya kwanza ya Sura ya Kwanza ya Rasimu ya Warioba na suala la muundo wa serikali tatu katika Jamhuri ya Muungano lililomo katika Sura ya Sita ya Rasimu ya Warioba. Imefikia hatua sasa wapo wanaodhani ukizungumzia shirikisho maana yake ni serikali tatu na ukizungumzia serikali mbili umekataa shirikisho. Mtizamo huo sio sahihi kama nitakavyoeleza baadaye.

Pili inaelekea kuwa wapo watu ambao wana mzio (allergy) na neno “Shirikisho” na hivyo kulichukia na kulipa maana hasi ambayo siyo sahihi. Kwa watu hao kwao neno shirikisho wamelipa maana ya kubuni ya kifo cha Muungano. Mtizamo huo  sio sahihi na ni mtizamo potofu kabisa. Hakuna uhusiano wa moja kwa moja wa kufa kwa Miungano duniani na dhana ya shirikisho. Kwani ipo Miungano ya Serikali moja ambayo ilikufa katika kipindi kifupi sana kama ule wa Misri na Syria na ipo Miungano ya shirikisho ambayo inadumu mpaka leo kama vile Ethiopia, Nigeria, Jamhuri ya Shirikisho la Ujerumani, Marekani na India.

Tatu kuna dhana potofu kuwa shirikisho na muungano wa serikali tatu unaopendekezwa katika Rasimu ya Warioba utahamasisha utaifa wa Tanganyika. Dhana hiyo pia ni potofu kwani zipo nchi zenye muungano wa serikali moja kwa sababu ya kulazimisha kufuta utambulisho wa upande mmoja wa Muungano huo leo baada ya zaidi ya miaka hamsini ya Muungano wao upande ule ambao ulizikwa utambulisho wake unadai sasa utaifa wake. Nchi hiyo ni Jamhuri ya Cameroon ambayo ni muungano wa serikali moja  wa iliyokuwa “French Cameroon” na “British Cameroon” zilizoungana mwaka 1961. Hali hiyo imechambuliwa vizuri sana na  Verkijika G. Fanso katika makala yake “Anglophone and Francophone Nationalism in Cameroon” [The Round Table (1991) 350, 281 – 296] na pia katika makala ya Piet Konings na Francis G. Nyamnjoh  “The Anglophone Problem in Cameroon” [The Journal of Modern African Studies, 35, (1997), 207 – 229]

Nilianza kwa kusema kuwa suala la shirikisho na suala serikali tatu hayahusiani ingawa yanaingiliana. Mjadala wa aina ya Muungano wa Tanzania umekuwa na ubishani mkubwa kwa miaka mingi. Je Muungano huu ni serikali moja yaani “Unitary State” au ni wa shirikisho yaani “Federation”?.Wapo wanazuoni maarufu wa sheria hapa Tanzania na wanasiasa wa Chama cha Mapinduzi (CCM) ambao wamechambua Muungano huu wa sasa wa serikali mbili na kuhitimisha kuwa ni wa mfumo wa Shirikisho. Hii ina maana hata sasa tuna shirikisho la serikali mbili. Kwa hali hiyo basi Rasimu ya Warioba ilipendekeza tutoke kwenye shirikisho la serikali mbili la sasa na kwenda katika shirikisho la serikali tatu.

Miongoni wa wanazuoni hao ni Profesa P.B. Srivastava ambaye alifundisha sheria za Katiba (Constitutions and Legal Systems of East Africa) na Sheria za Utawala (Administrative Law) katika Kitivo cha Sheria cha Chuo Kikuu cha Dar es Salaam katika miaka ya 1980 ndiye aliyechambua kwa kina muungano wa Tanzania na kuhitimisha kuwa ni wa aina ya shirikisho katika Mhadhara wake wa Kiprofesa (Professorial Inaugral Lecture) wake alioutoa Machi 1982 iitwayo “The Constitution of the United Republic of Tanzania 1977:Some Salient Features – Some Riddles”.

Miaka minane baadaye, yaani mwaka 1990,  msomi mwingine Profesa Issa Gulamhussein Shivji, ambaye kwa miaka yote kabla ya hapo alikuwa akijihusisha na Sheria za Kazi (Labour Law) alitoa Mhadhara wa Kiprofesa (Professorial Lecture)  wake uitwao “The Legal Foundation  of the Union in Tanzania’s Union and Zanzibar Constitutions” naye alihitimisha kuwa Muungano wa sasa wa Tanzania ni wa mfumo wa shirikisho kama nitavyofafanua baadaye.

Wanasiasa wa CCM ambao walisema kuwa Muungano wa sasa ni shirikisho ni Alhaj Aboud Jumbe Mwinyi aliyekuwa Makamu Mwenyekiti wa CCM, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi. Msimamo huo uliungwa mkono na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika hotuba iliyotolewa na aliyekuwa Waziri Kiongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Brigedia – Jenerali Ramadhan Haji Faki mwaka 1983 alipojibu hoja ya ushauri kuwa Waziri Mkuu wa wakati huo Edward Moringe Sokoine aliposhauri Chama cha Mapinduzi kuwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano ina mamlaka juu ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar. [Zanzibar Government: A Reaction to Prime Minister Ndugu Sokoine’s Advice to the Party to Restructure the Government given to the Party and Government Leaders Tabled by the Chief Minister to the House of Representatives, Zanzibar Printing Press, 1983, p. 5). Msimamo huo pia uliungwa mkono na aliyewahi kuwa Mwanasheria Mkuu wa SMZ, Wolfgang Dourado.

Msimamo huo wa Mzee Jumbe kuwa muundo wa Muungano ni shirikisho ulileta kuchafuka kwa hali ya hewa wakati wa mjadala wa Mabadiliko ya Tano ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano na Mabadiliko ya Katiba ya Zanzibar. Pamoja na Mwasisi wa Muungano na Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere kutofautiana na Mzee Jumbe, kama ilivyoelezwa katika Randama ya Rasimu ya Warioba katika ukurasa wa tatu, nanukuu:

“Kwa mujibu wa kumbukumbu za kikao cha halmashauri ya Taifa ya Chama cha Mapinduzi katika mkutano wa tano ambao ulikuwa maalumu uliofanyika Dodoma Januari 24-30, 1984, Mwalimu Nyerere alitamka kuwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ukiangalia kwa jicho la Zanzibar ni wa Shirikisho lakini ukiangalia kutoka Tanzania Bara ni serikali moja. Mwalimu alikuwa akimjibu Makamu Mwenyekiti wa CCM, Makamu wa Rais na Rais wa Zanzibar Sheikh Aboud Jumbe Mwinyi aliyesema kuwa Muungano wa Tanzania umeunda shirikisho (Federation) na sio serikali moja (Unitary State).

Mfumo wa Shirikisho unaopendekezwa katika Rasimu ya Warioba unaendeleza hadhi ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuwa ni Nchi na ni Dola moja lenye mamlaka kamili yenye serikali tatu, shirikisho hili linatokana na muungano wa hiari wa Tanganyika na Zanzibar ambazo zilikuwa Jamhuri zenye mamlaka kamili kabla ya kuungana tarehe 27 Aprili 1964”

Msimamo huo wa Mwalimu Nyerere kuwa kwa upande wa Zanzibar Jamhuri ya Muungano ya Muungano ina sura ya shirikisho inafanana kwa kiasi fulani na uchambuzi wa mtaalam nguli Mwingereza wa masuala ya katiba Professor S.A. de Smith ambaye katika kitabu chake kiitwacho Constitutional and Administrative Law, 2nd Edition, 1973, p.33 anasema kwamba:

“Tanzania is part federation, since Zanzibar has exclusive fields of competence both in theory and in practice, but for political reasons the term ‘federal’ does not appear in the constitution and in as much as it implies a degree of disunity as well as diversity.”

Kwa kiswahili akimaanisha “Tanzania kwa sehemu ni shirikisho kwa sababu Zanzibar ina mamlaka yake kamili ya ndani kinadharia na kivitendo lakini kwa sababu za kisiasa neno shirikisho halionekani katika Katiba huku hali hii ikionesha kiwango cha utengano pamoja na utofauti” (Tafsiri ni yangu).

Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere katika kitabu chake cha “Uongozi wetu na Hatima ya Tanzania” katika ukurasa wa 15, alipata kusema “Nchi mbili zinapoungana na kuwa Nchi Moja mifumo ya kawaida mifumo ya miundo ya Katiba ni miwili: Kwa mfumo wa kwanza kila nchi itafuta serikali yake, na Nchi mpya inayozaliwa itakuwa ni nchi moja yenye serikali moja.

Katika mfumo wa pili kila nchi itajivua madaraka fulani ambayo yatashikwa na serikali ya shirikisho, na itakuwa na serikali ambayo itakuwa na mamlaka juu ya mambo yaliobaki. Mambo yatakayoshikwa na serikali ya shirikisho ni yale ambayo yakibaki katika mamlaka ya nchi zilizoungana basi nchi hizo huwa huru. Shirikisho halisi la nchi mbili litakuwa ni nchi moja yenye serikali tatu, Serikali ya shirikisho na serikali mbili za zile nchi mbili za awali zilizoungana kuzaa nchi mpya moja.”

Muundo wa Shirikisho, ambao ni tofauti na muundo wa serikali moja. Katika muundo huu, nchi zinapoungana kunakuwa na ngazi mbili za serikali, yaani serikali ya muungano au shirikisho na serikali za washirika. Serikali ya Muungano inakuwa na mamlaka kwa masuala yote yaliyokubaliwa kuwa ya muungano, wakati serikali za washirika zinakuwa na mamlaka ya kikatiba kushughulikia mambo yote yasiyo ya muungano.

Sababu nyingine ya kuendelea kupendekeza muundo wa shirikisho lenye serikali tatu ni uhalisia kwamba Muundo wa Shirikisho utaendelea kuhifadhi asili, taswira na hadhi ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika jumuiya ya kimataifa kwa mujibu wa Kifungu cha 2 cha Mkataba wa Montevideo wa mwaka 1933 unaohusu Haki na Majukumu ya Nchi (the Montevideo Convention on Rights and Duties of States) unaosema na ninanukuu “the federal state shall constitute a sole person in the eyes of international law” inayomaanisha nchi yenye muundo wa shirikisho katika sheria za kimataifa ni nchi na dola moja.

Katika mfumo huu, kwa kawaida mamlaka ya mwisho au mamlaka kamili (sovereignty) yanabaki katika serikali ya shirikisho. Kama nilivyosema, utambulisho wa nchi katika mahusiano ya kimataifa na vyombo vya ulinzi na usalama hubaki katika serikali ya shirikisho. Sifa nyingine ya shirikisho ni kuwa mwananchi anatawaliwa na serikali mbili ilihali katika muundo wa muungano wa serikali moja mwananchi anatawaliwa na serikali moja pekee. Muungano wa Tangannyika na Zanzibar siku zote umekuwa na sura mbili. Kwa wananchi wa Zanzibar wamekuwa katika shirikisho tangu mwaka 1964 kwa sababu wanatawaliwa na serikali mbili (serikali ya muungano na serikali ya Zanzibar). Kwa upande wa Tanzania Bara kuna sura ya muungano zaidi kwa sababu kuna serikali moja kwa maana serikali ya Tanzania Bara au Tanganyika haipo.

Sababu nyingine ya kupendekeza muundo wa shirikisho ni kukuza demokrasia kwa maana ya kutoa mamlaka zaidi kwa nchi washirika kujiamulia mambo yao wenyewe. Hii inatekeleza madai ya miaka mingi ya Zanzibar kuwa na Shirikisho la Serikali Tatu tangu wakati wa Mzee Aboud Jumbe Mwinyi na baada ya hapo ambalo liliungwa mkono na watu wengi akiwemo Profesa Issa Gulamhussein Shivji. Hoja hiyo ya Prof. Issa Shivji kuunga mkono madai ya Zanzibar ya kuanzishwa kwa mfumo wa shirikisho lenye serikali tatu limo katika kitabu chake kiitwacho “Pan-Africanism or Pragmatism?: Lessons of the Tanganyika – Zanzibar Union (2008 ukurasa 250 anaposisitiza kuwa;

“A demand for a three government federation, greater autonomy for Zanzibar, reduction in union matters, from Zanzibar was a demand for the right to self-determination, a democratic demand” [ yaani, madai ya shirkisho la serikali tatu na kupunguzwa kwa mambo ya muungano yanayotolewa na Zanzibar ni madai ya haki ya kujiamulia mambo yao na ni haki ya kidemokrasia Uk. I.G. Shivji, Pan Africanism or Pragmatism? Lessons of Tanganyika- Zanzibar Union,2008, P. 250]
 
Pia, Chini ya mfumo wa Muungano wa Shirikisho, ugawaji wa madaraka huwekwa kwenye Katiba kiasi kwamba katika hali ya kawaida serikali ya muungano haiwezi kuingilia na kunyang’anya madaraka ya serikali za washirika bila ya kufuata utaratibu uliyowekwa kwenye Katiba. Nchi ambazo zimeimarika katika mfumo huo ni pamoja na Marekani, Kanada, India, Brazil, Ujerumani, Uswisi, Australia, Nigeria na Ethiopia. Mfumo wa Shirikisho unawezesha nchi washiriki kuwa na nguvu kubwa ya kushughulikia maslahi ya pamoja huku kila moja ikiwa na mamlaka ya kushughulika masuala yasiyo ya pamoja. Mfumo huu unawapa washirika wa Muungano fursa ya kuhifadhi utambulisho wao wa kihistoria.

Sababu nyingine muhimu ya kupendekeza muungano wa shirikisho la serikali tatu ni kuweka bayana mamlaka tatu ndani ya Jamhuri ya Muungano zilizobainishwa na Katiba ya sasa ya Jamhuri ya Muungano  ya Mwaka 1977 katika Ibara ya 4, 34, 64 na 102. Mamlaka hizo ni Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Serikali ya Zanzibar na Serikali ya Tanzania Bara.  Hoja hii inatiliwa nguvu na Msomi Maarufu wa Masuala ya Katiba Professor Srivastava, kwamba:

 “The United Republic envisages a triangular system with Tanzania Mainland and Zanzibar forming two corners of the base and the United Republic constituting the vortex. Accordingly, there are three jurisdictional areas territory-wise and subject-wise for the operation of governmental powers, both legislative and executive, which necessitate existence of three governments, namely, Government of United Republic, Government of Tanzania Mainland and Government of Zanzibar corresponding to three jurisdictions.


[Tafsiri yangu: Jamhuri ya Muungano ni mfumo wa serikali tatu, Tanzania Bara na Zanzibar zikiwa ni nguzo za pembeni na Jamhuri ya Muungano ikiwa ni kilele chake: Hivyo, kuna mamlaka tatu kieneo na kimatumizi ya madaraka ya kiserikali, kibunge ambayo yanalazimu kuwe na serikali tatu: yaani serikali ya Jamhuri ya Muungano, Serikali ya Tanzania Bara na Serikali ya Zanzibar] { B. P. Srivastava, 'The Constitution of the United Republic of Tanzania 1977 - Some Salient Features, Some Riddles' Eastern Africa Law Review 11-14 (1978-81}, 73-127, at pp.79-80.}

No comments:

Post a Comment