Saturday, May 16, 2015

SERIKALI IKISEMA “NDIYO” UJUE KUNA SABABU YA KUSEMA HAPANA


Pale tunapokuwa na maswali mengi zaidi kuliko majibu na hekaya za mbio za sakafuni

Ni dhahiri sasa kwamba serikali imejipambanua moja kwa moja kwamba inaunga mkono Katiba Inayopendekezwa. Serikali imekwenda mbali zaidi na kutoa maelekezo kwa wananchi kwamba wakati ukifika waipigie kura ya “Ndiyo” Katiba Inayopendekezwa. Huenda mnashtuka, ndiyo, kwani hamkufuatilia Sherehe za Miaka 51 ya Muungano wetu mwezi uliopita. Shamra shamra na jumbe za maadhimisho zilijinasibu na hamasa ya kuipigia kura ya ndiyo Katiba Inayopendekezwa. Ilikuwa bayana kwamba haikuwa bahati mbaya, maadhimisho ya Muungano ni sherehe za kitaifa na zinaandaliwa, kuratibiwa na kuendeshwa na serikali, kwa mwenzangu na mimi ujumbe ulifika bayana kabisa.
Labda nirejee msingi wa utawala wa nchi yetu Tanzania, Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 1977 Toleo la 2005 na ndio Katiba inayotumika sasa inasema katika Ibara yake ya 8 inasema “Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni Nchi inayofuata misingi ya demokrasia na haki ya kijamii, na kwa hiyo - (a) wananchi ndio msingi wa mamlaka yote, na Serikali itapata madaraka na mamlaka yake yote kutoka kwa wananchi kwa mujibu wa Katiba hii; (b) lengo kuu la serikali litakuwa ni ustawi wa wananchi; (c) Serikali itawajibika kwa wananchi; (d) wananchi watashiriki katika shughuli za Serikali yao kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii”.
Wananchi ndio msingi wa mamlaka yote, maneno haya ni maneno mazito kabisa, na kwa lugha nyingine, cheo kikubwa kabisa cha msingi katika Taifa letu ni raia (citizen), huyu ndio mwananchi mtanzania. Imesemwa pia, kwamba “Serikali ni watu” na kwa hakika watu wenyewe ndio kwa ujumla wao huitwa raia wa Jamhuri ya Muungano, na wananchi wa Taifa letu.
Serikali hupaswa kutenda sawasawa na matakwa ya watu yanayozingatia maslahi mapana ya Taifa letu. Sifa kubwa ya serikali bora tangu kuasisiwa kwa Taifa letu imekuwa ni ile ambayo ni sikivu kwa wananchi. Usikivu huu wa serikali sio ni matokeo ya utashi pekee, la hasha, bali ni msingi ambao sisi kama Taifa tumekubaliana kuujenga na kuuweka katika Katiba kwamba “Serikali itapata madaraka na mamlaka yake yote kutoka kwa wananchi kwa mujibu wa Katiba hii pamoja na Serikali itawajibika kwa wananchi”
Unapoanza kuona serikali inatenda lwake, mbali na wananchi wanataka nini, tunapaswa kujihoji tunakotoka, tuliko na tunakokwenda kwa maana ya namna tunaishi na kusimamia misingi muhimu ya Taifa letu.
Sisi kama Taifa tumekubaliana kwa pamoja kwamba tutaandika Katiba Mpya na ili kuhitimisha mchakato wa huu, sisi raia tutaamua kama ipite ama isipite kwa kuifanyia uamuzi wa Kura ya Ndio au Hapana. Kifungu cha 35 cha sheria ya Kura ya Maoni kimeliweka sharti hili bayana kabisa. Kila raia ana haki ya kuamua ama apige kura ya NDIO au kura ya HAPANA, sisi raia na taasisi zetu za kiraia vikiwemo na vyama vya siasa na taasisi za kidini tunashiriki kujadiliana kwa hoja na sababu. Kuna maeneo tunakubaliana na kuna maeneo tunahitaji mjadala zaidi, na tunaendelea kufanya hivyo.
Wajibu wa serikali katika mchakato huu ni uwezeshwaji, uraghibishi au “facilitation”, na ndio maana kwa mujibu wa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba na Sheria ya Kura ya Maoni serikali kwanza ilituundia Tume ya Katiba, kisha serikali ikatuundia Bunge Maalum na hatimaye serikali kupitia Tume ya Taifa ya Uchaguzi itatuendeshea kura ya maoni. Hakuna wajibu mwingine kisheria ambao serikali imepewa juu ya mchakato huu isipokuwa kuuwezesha kifedha, kwa kutoa rasilimali watu na vitendea kazi kila inapobidi.
Wakati wa Bunge Maalum, kidogo serikali ilijisahau, ikajikuta inapanga na kupangua hoja na kidogo kidogo tukaanza kuona kumbe viongozi wetu katika serikali wana msimamo katika mchakato huu. Mimi sina tatizo la kimsingi kama viongozi wetu wa kuchaguliwa wakiwa na msimamo na hii ni kuanzia kwa Mhe. Rais, Mawaziri, Wabunge, Madiwani na wenyeviti wa serikali za mitaa na vitongoji. Hawa najua tunaweza kuhojiana nao kwa hoja, sababu na ushahidi na nina uhakika inapokuja kwenye suala la maoni ya Katiba Mpya, wananchi nao wanajua walisema nini, kwahiyo sina shaka.
Tatizo langu ni kuingiza Serikali jumla jumla, hilo ni kosa, ni kosa kubwa sana, na ndio maana nahoji, Kama serikali ikisema NDIO nani wa kupinga? Ninapata moyo mkuu wakati huu kwasababu najua viongozi wetu wa kisiasa wengi wao wana lao jambo na wanatumia kila mbinu kupitisha masuala ambayo yatalinda maslahi yao. Mbinu hizi wanazotumia viongozi wetu wa kisiasa zinajumuisha kuitumia “machinery” au taasisi ya serikali kwenye kupenyeza ushawishi wao wa kutafuta kura za NDIO, hilo ni kosa.
Mimi kama raia, nasema HAPANA kwa tabia hii isiyofaa, serikali inapaswa kutokuwa na upande au “neutral” na nitoe rai kwa wanasiasa kuacha kutumia “machinery” ya serikali kwa manufaa binafsi, ni makosa makubwa. Na kama tabia hii itaendelea mimi, hata kama nitabaki peke yangu, nitaendelea kuikemea kuwa ni mbaya na isiyofaa na nitaongeza jitihada za kuwaeleza watanzania kwamba Katiba Inayopendekezwa imelinda viongozi na imepora haki za wananchi.
Leo niendelee na uthibitisho wa namna ambavyo Katiba Inayopendekezwa inawalinda viongozi na ndio maana wanaipigia chapuo. Usikubali ee mwananchi, Katiba Mpya Bora itatusaidia kudhibiti matumizi mabaya ya baadhi ya viongozi wetu.
Utolewa, usimamizi, uhifadhi na udumishwaji wa haki za binadamu ni jukumu la serikali pamoja na umma wa watanzania. Haki za binadamu zikichezewa, watu wetu wataendelea kunyanyaswa pasina heshima ya utu wao, kuwa mafukara katika nchi yao wenyewe yenye utajiri wa kila namna. Ili kuhahakisha haki za binadamu zinatunzwa, zinatolewa, zinahifadhiwa, zinalindwa na kuheshimiwa na watu na kwa watu wote, Rasimu ya Katiba Mpya Toleo la Pili ijulikanayo kama Rasimu ya Warioba iliweka masharti yafuatayo;-
Ibara ya 210(1) inahusu Kazi na Majukumu ya Tume ya Haki za Binadamu, “(i) kutembelea magereza, vituo vya polisi au mahali penginepopote ambapo mtu au watu wanazuiliwa kwa madhumuniya kutathmini na kukagua hali za watu anaozuiliwa katikasehemu hizo na kutoa mapendekezo yatakayowezeshakurekebisha kasoro zilizopo;
(j) kutoamapendekezoyanayohusiananasheriailiyokwi shatungwa au inayokusudiwa kutungwa, kanuni, aumambo ya kiutawala ili kuhakikisha zinakidhi
viwango vyakimataifa na kikanda vya haki za binadamu;
(k) kuwasilisha taarifa na maoni huru kwenye vyombo na taasisiza kimataifa na za kikanda kuhusu hali ya haki za binadamunchini pale inapobidi;
(l) kuihamasisha Serikali kutia saini na kuridhia mikataba aumakubaliano ya kimataifa yanayohusu haki za binadamu,kufuatilia na kutathmini utekelezaji wa haki za binadamu zilizomo kwa mujibu wa Katiba hii, Katiba za NchiWashirika, sheria za nchi na mikataba au makubaliano yakimataifa ambayo Jamhuri ya Muungano inawajibika nayo; na
(m) kwa kupitia Serikalini, kushirikiana na wawakilishi waUmoja wa Mataifa, Mashirika ya Umoja wa Mataifa, Umojawa Nchi za Afrika, Jumuiya ya Madola na taasisi nyinginezenye mahusiano baina yao, miongoni mwao au ya kikanda na taasisi za nchi nyingine katika maeneo ya hifadhi naukuzaji wa haki za binadamu”.
Ibara ya 210(2) ikaweka Masharti yafuatayo;- “Tume ya Haki za Binadamu itakuwa na mamlaka maalum kama ifuatavyo: (a) kumuita mtu yeyote mbele ya Tume na kumtaka awasilishembele yake nyaraka zozote, kumbukumbu au kitu chochotekilicho katika mamlaka yake kinachohusiana na jambolinalochunguzwa na Tume; (b) kumtaka mtu yeyote kutoa taarifa anayoifahamu kwa Tumejuu ya jambo linalochunguzwa na Tume; (c) kusababisha mtu yeyote anayekiuka maagizo au taratibu zaTume kufunguliwa mashtaka ya jinai mahakamani”.
Masharti haya yote yaliyokuwamo kwenye Rasimu ya Warioba yamefutwa na hayamo katika Katiba Inayopendekezwa. Najiuliza dhamira ya waandishi wa Katiba Inayopendekezwa ilikuwa ni ipi? Na Najiuliza dhamira ya Serikali kutulazimisha kupigia Kura ya NDIO kwa Katiba Inayopendekezwa ilhali ikijua kuna mapungufu yote hayo ni ipi.
Mwisho kabisa nitoe RAI kwa Tume ya Uchaguzi, kwamba tarehe ya Kura ya Maoni ni jambo linalopaswa kuwa bayana, tusigeuze tarehe ya Kura ya Maoni kama siku ya kurudi Masiha, kwa maana haijulikani siku wala saa. Sifa moja kubwa ya utawala bora na wenye ufanisi ni “predictability” hali ya kuwa bayana na mambo ya baadaye.
Leo ni tarehe 17 Mei 2015, bado tunaandikisha wapiga kura mpaka mwezi wa saba. Bunge huenda litavunjwa mwezi wa saba na baraza la wawakilishi mwezi wa nane. Kampeni za Uchaguzi Mkuu ni zaidi ya siku 60, kwa maana kwamba kampeni zitaanza mwishoni mwa mwezi wa Agosti na kumalizika wiki ya mwisho ya Mwezi Oktoba. Sasa kweli kabla ya Uchaguzi Mkuu unaona hapo Kura ya Maoni ikifanyika? Haiwezekani! Haya tuangalie marekebisho ya Katiba ya Mwaka 1977 ili tuvuke Uchaguzi Mkuu bila tashwishwi, mpaka leo hakuna mswada wa sheria wa marekebisho ya Katiba na Bunge la bajeti litaendelea hadi karibu na mwisho wa mwezi wa Juni.
Je ukitizama unaona nini mbele? Ninaona muda hautoshi, ninaona busara inahitajika zaidi hasa kuhusu Kura ya Maoni na Uchaguzi Mkuu ni lazima. Tafakari na tujadiliane.
WASAMBAZIE NA WENGINE na USISAHAU ku-LIKE Humphrey Polepole

No comments:

Post a Comment