Sunday, October 4, 2015

UCHAGUZI WA MWAKA HUU NI WAADILIFU NA WAZALENDO V/S GENGE LA WAHUNI “CARTEL” NA WASAKA MADARAKA KWA MANUFAA BINAFSI


Kwa muda mrefu kikundi cha wahuni kilijaribu na kufanikiwa kupoka madaraka ndani ya Chama cha Mapinduzi. Watu hawa walitaka kujijengea "cartel" ya kuongoza nchi, humo walikuwemo watu kadhaa na hasa wafanyabiashara akiwemo Lowassa na yeye ndiye alikuwa Msanifu wa genge hilo na hasa ili kutimiza ndoto yake ya kuwa Rais hata kwa kuununua Urais wa nchi yetu, alifanya hivyo mwaka 1995 akashindwa maana Mwalimu alikuwepo. Baada ya hapo genge hili lilijiposition kwenye maeneo yote nyeti ya nchi yetu.

Mwaka huu wana CCM tumekataa upumbavu huu wa kudhani Urais na Uongozi unaweza kununuliwa kama nyanya. Tumekataa na tumehakikisha katika ile "CARTEL" au GENGE la WAHUNI hakuna kati yao ambaye anaiona IKULU kwa tiketi ya CCM. Imewauma sana, Huyu bosi ndio kaenda UKAWA na wako waliobaki CCM, tutashughulika nao strategically, lakini kwanza ni lazima tupate Rais Mwadilifu KWANZA ambaye atatusaidia kazi ya Pili ya Kusafisha UFISADI. kazi ya Kwanza imekuwa kuwanyima Dhamana ya Urais kupitia CCM.

Hapa CCM wanapaswa kwakweli kujitoa kimasomaso. GENGE sasa limehamishia mapambano kutoka Kambi ya Upinzani. Utagundua hoja ya UFISADI ilishamiri sana na ndio maana kipindi fulani UKAWA waliunga Mkono kazi yetu ya Katiba ambayo lengo lake lilikuwa kuja kuua CARTEL au GENGE la WAHUNI, leo UKAWA hawana tena uhalali (legitimacy) ya kukemea UFISADI maana UFISADI umetamalaki kati na juu yao.

Hebu tafakari mtu kama ndugu yangu na kaka yangu Saeed Kubenea kwa kazi yooote aliyofanya miaka nenda rudi mpaka akashambuliwa, juzi alijisikiaje pale kawe aliponyooshwa mkono juu na Edward Lowassa? Dhamira yake ilimweleza nini? Na Lowassa hakusita kumpiga kijembe kwamba huyu alikuwa machachari sana kwenye Media sasa apunguze, hivi Kubenea amejiuliza Lowassa alimaanisha apunguze nini na kwa faida ya nani.?

Mimi mpaka TV mbili kubwa zimekataa nisikaribishwe kwenda kwenye vipindi kwa maelekezo ya wamiliki. Je kukataliwa kwangu ni kwa faida ya nani? Mbona kama ni siasa kila siku kwenye TV hizo wadau wa UKAWA wanajimwaga vilivyo, je mimi tatizo langu ni nini? Wengine walifurahia TCRA kutoa tamko la kukataza watu kwenda kwenye vipindi vya moja kwa moja, na wengi walisema mitandaoni wamenikomesha mimi, hivi mimi nikikomeshwa ni kwa faida ya nani?

TCRA walilazimisha kwamba ili uruhusiwe kushiriki kwenye vipindi vya moja kwa moja ni lazima uwe mwakilishi wa vyama vya siasa. Mimi nikasema kwa hakika ningemwambia ndugu Kinana Katibu Mkuu wa CCM angenipa barua ili niendelee kushiriki. Lakini nikasema hivi wanaoruhusiwa kushiriki ni wanasiasa peke yake? Je uchaguzi ni haki uhodhiwe na wanasiasa pekee? Nikaendelea kujiuliza hivi uchaguzi mkuu wanaotakiwa kujadiliana zaidi ni Wananchi wanaochagua ili kutoa dhamana au wale wanaoomba kuchaguliwa ili kupewa dhamana? Nikasema mbona Katiba inasema kuna Uhuru wa kuweka mawazo hadharani je mawazo hayo yako limited wamakati wa uchaguzi?

Nikafunga safari kwenda TCRA nikawauliza maswali hayo na namshukuru Mungu aliwapa busara kubwa na baadaye walitoa tamko kubatilisha katazo lao la awali. Lakini nikajiuliza zaidi kwanini hata wale wadau wa asasi za kiraia hawakuoneshwa kukasirishwa na kitendo kile cha TCRA? Nikasema hata watu wote wakisimama mimi nitaendelea kudai haki na kweli katika nchi yangu.

Leo siwezi kwenda kwenye TV mbili kubwa na wamiliki wameweka msimamo, kwanini? Wale wanaofurahia mimi kukataliwa je wanapata faida gani.? Mbona mimi nikionana na vijana na wadogo zangu ambao wako katika vyama vya upinzani nawapa moyo na kuwaambia watende sawasawa na dhamira zao njema na kwamba walitizame Taifa kwanza? Najiuliza je Tatizo langu ni nini? Au sijitambui? Au niko naïve?

Nitasema kweli Daima na fitina kwangu mwiko na nitatumia elimu yangu kwa manufaa ya Wananchi wa Taifa langu. Kwanini leo baadhi ya watu wamenigeuka, watu ambao walifurahia nilipowaambia pale Ubungo plaza na pale Mlimani city kwamba maslahi binafsi yanahatarisha mustakabali wa Taifa letu. Nilikwenda mbali na kuwataja watu hao na watanzania baadhi na wengi wakanifurahi sana. Mbona leo naendelea kuwasema watu wale wale na baadhi ya watanzania wananiona nimegeuka? Kwanini waliniamini kipindi kile na wakijua mimi ni CCM na nilikuwa nawasema CCM na leo Mimi nikiwa bado CCM nawasema watu ambao wanataka kutununua ili waendeleze GENGE la KIHUNI mbona watu wanaema mimi ni kigeugeu? Naendelea kutafakari.

Siku moja nilikaa na viongozi wawili wa CCM, mmoja akasema nadhani mchakato wa Katiba ni lazima kabla ya kura ya maoni tujenge muafaka na kufanya maridhiano ili kila sauti ya Mtanzania isikilizwe. Kiongozi mwenzake mdogo kidogo kwa cheo akabisha sana na akasema ni lazima twende kwenye kura ya maoni kwasababu tendo la Katiba kwa lilipofika ni kama maji yanayomwaga kutoka katika bilauli kwamba ni lazima yafike chini.

Nikamtazama na kumkazia macho na nikamweleza wacha na mimi nizungumze kama mwana CCM. Nikawaomba niwaeleze historia ndogo ya namna nipo nilipo. Nikasema nianzie kwenye Katiba, nikawaambia unajua mimi nilikuja Tume ya Katiba nikiwa simfahamu mtu yeyote isipokuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano? Nikawaeleza mimi sikumfahamu Mzee Warioba, Jaji Ramadhani, Mzee Butiku, Dkt. Salimu wala Profesa Kabudi na wengineo, sikumfahamu hata mmoja. Nilikuwa namfahamu Rais Kikwete tu. Alipotupa kazi na akatuagiza tuwasikilize watanzania na watakachosema ndicho ambacho tukiandike, tulifanya hivyo kwa unyenyekevu mkubwa kwa watanzania.

Hata pale ambapo Rais alionekana kutoka na msimamo tofauti na wetu nilibaki kuwaambia watanzania kwamba Tanzania njema itajengwa na watanzania wenyewe. Hatukuishia pale tuliokuwa wajumbe wa Tume ya Katiba tulifanya utafiti kwa kuzungumza na wadau mbalimbali, wabunge, viongozi wastaafu, watu mashuhuri ili kuelewa tatizo lilikuwa wapi.

Utafiti huu wa chini chini ulinipa fursa ya kuonana na wabunge wengi wa CCM na wa upinzani na wote walikiri kwamba “Bwana Mkubwa amekataa” na tulipozidi kuhoji hoji tulikuja kukutana na wapambe wake kwanza ambao walisema “tatizo lenu mmedhoofisha Urais na kwamba Kikwete anataka kuondoka ameweka masharti na kanuni ngumu za uongozi hilo haliwezekani” wakaendelea kusema “yeye (Kikwete) aende na sisi tubaki na madaraka yale yale au zaidi na tuwe na mamlaka kama aliyonayo sasa katika nchi”.

Wapambe hawa tulizungumza nao kwa maana ya kuwapa elimu ya Rasimu ya Katiba na wakawa wanatuuliza “kwahiyo ninyi (Tume ya Katiba) mnashauri ‘Mkubwa’ achukue Urais wa Tanzania au Urais wa Tanganyika?” Tukasema achukue ya Muungano, wakasema “je itahusisha madini, gesi na ardhi”? Tukasema hapana, wakaendelea kuuliza “je akichukua ya Tanganyika atakuwa na uwezo wa kusafiri nje ya nchi kama Rais Kikwete na kupigiwa mizinga 21”? Tukasema hapana, mmoja wao akasema “anhaaa hapo ndio mnapokosea, sisi tunataka zote za Tanganyika na Muungano ziwe pamoja”, kwa kusema hivyo walikuwa wanamaanisha serikali mbili.

Hatukuchoka tukafanya utaratibu na tukaenda kumuona “Bwana Mkubwa” yaani Edward Lowassa, tulikutania ofisini kwake mikocheni. Ili kuweka uwazi katika mkutano ule tulijumuisha pia wawakilishi watatu wa Asasi za Kiraia na Makamishna Wawili, mimi nikiwa mmojawapo, tulikuwa na kikao ambacho hakikupungua saa mbili.

Ni katika kikao kile nilithibitisha kwamba aliyebuni mkakati wa kuikataa Rasimu ya Warioba kwa CCM alikuwa Edward Lowassa tena akaonesha kufurahishwa na Rais Kikwete kama Mwenyekiti wa Chama kuzomewa na hatimaye Rasimu aliyoipeleka katika Chama kukataliwa. Nilijuliza sana mimi kama Kiongozi kijana, tafsiri yake ni nini? Huyu ni mwana CCM na anafurahia Mwenyekiti wake kudhihakiwa na kutupiwa Rasimu yake katika kikao. Leo najiuliza kama alikuwa na dhamira ya kuikubali rasimu ya Warioba kwanini alikaa kimya wakati Mwenyekiti wake akidhihakiwa?

Nikawaeleza iliyokuwa Tume ya Katiba iliwahi kumwita hata mzee Kingunge aje tujadiliane kuhusu Rasimu ya Warioba na alipokuja aliwatukana wajumbe wa Tume pamoja wageni wengine waalikwa akiwemo Profesa Sherrif kutoka Zanzibar, nilipoona anamwunga mkono Lowassa sasa namwelewa na ndio maana katika mkutano wa Taasisi ya Mwalimu Nyerere nilidiriki kusema Mungu akinipa umri mrefu na kufikia uzee namwomba Mungu nisiwe kama wao.

Nikamwambia yule Kiongozi mdogo, unadhani ni kazi rahisi mimi kama kijana mdogo kusimama kidete kutetea maoni ya Wananchi? Nilijua aliyekuwa na maslahi katika kutupilia maoni ya Wananchi hakuwa Kikwete bali Edward Lowassa ambaye amekuwa akiutafuta Urais wa kifalme. Kuthibitisha hilo nilimtamka kwa jina mara kadhaa Ndugu Edward Lowassa kwamba hafai kuwa Rais wa Tanzania.

Na kwangu mimi nilikuwa najiuliza hata kupitia CCM ambako mimi ni mwanachama, iweje mtu ambaye anakosa kuheshimu watanzania wanapotoa maoni yao ya Katiba akawa ni mtu ambaye atasimama ili wampe dhamana ya kuwa Rais wao. Mimi nilimkataa tangu CCM na nilipoona CCM kama vile wanachelewa, mimi (Polepole), Mzee Butiku na Mzee Warioba tulifanya mdahalo na tukaweka msimamo kama Lowassa atapewa tiketi ya kugombea Urais kupitia CCM basi sisi watatu tusingejitoa bali tungepiga kampeni ya kusema CCM isichaguliwe.

Nikaendelea kumwambia hili la Katiba Mbaya wake namjua na alijaribu kuhonga watu, ni lazima tujenge muafaka wa kitaifa kwanza. Namshukuru Mungu Kiongozi Yule ni muelewa akasema muafaka ni kitu muhimu, hilo linawezekana na ni kwa maslahi ya watanzania wote sema tu kipindi kile kiligubikwa na ushindani wa kisiasa, ila sasa ni muhimu tukaja pamoja kama Taifa. (Mwisho wa kunukuu kikao change na viongozi wa CCM)

Uhalisia huu ndio umefanya Mzee Joseph Sinde Warioba kupiga kampeni ya Chama cha Mapinduzi. Ila kitu kimoja napenda kuwaeleza kuna maadui ndani ya CCM na nje ya CCM na hasa hasa wale ambao wako chini ya “cartel” au lile GENGE la WAHUNI ambalo linafanya kila jitihada ili Mgombea wa CCM asiye na makundi na asiye na msalie mtume na wezi, wabadhirifu na mafisadi. Maadui hawa wako radhi Mwana Mtandao mwenzao (aliyeondoka CCM na kwenda UKAWA) apewe dhamana ya Urais wa nchi yetu ili waendelee kutunyonya kwa maslahi yao.

Ikumbukwe UKAWA huu sio UKAWA ule ambao mimi na Mzee Butiku na Mzee Warioba tulifanya nao kazi pamoja, si hawa. Hawa UKAWA wa sasa ni watu wenye uchu wa ajabu wa madaraka na kwamba wako tayari kumtumia mtu mwenye nasaba zote na ufisadi ili awafikishe ikulu.

Kama ni masikini na nikaambiwa mwabudu shetani ili niwe tajiri, nitakataa na kutunza utu wangu kama ambavyo Bwana Yesu alikataa kumwabudia shetani kwa sababu hizohizo.

Hivi sielewi hawa wanachama wa Chadema ambao wamekubali kumeza matapishi yao wenyewe, wanapataje amani mioyoni mwao wanapojua mgombea Urais wao ndio Yule mtu waliyesema ni fisadi kwa zaidi ya miaka 8. John Mnyika alisema anao ushahidi wa UFISADI wa Lowassa, Mbowe alisema anashangaa vibaka wanachomwa moto na Lowassa ameachwa anadunda mtaani, Mchungaji Msingwa aliyesema anayemkubali Lowassa akapimwe akili na Godbless Lemay eye amekuwa kimya kidogo ila naye amesema ni halali kumtupia jiwe fisadi lowassa. Hawa leo wanapataje uthubutu wa kusimama katika jukwaa moja na Lowassa na tena wakainuliwa mikono akiwanadi.

Mimi nilijiapiza wale waliokataa maoni ya Wananchi sitaki urafiki nao hata leo, na Lowassa ni mfano mmoja. Na niko tayari kuendelea kuunga mkono mabadiliko chanya yaliyofanywa na Chama cha Mapinduzi (CCM) kwa kuuvunja na kuwanyima Urais kupitia CCM. Hii ndio CCM ya kweli, CCM ya wakulima na wafanyakazi, CCM inayochukia rushwa katika uongozi na sasa tumeanza na Urais na baada ya Urais tutawashukuia wabaya wote waliosalia. CCM ambayo haishurutishwi na matajiri wanaotaka kututengenezea viongozi ikiwemo nafasi ya Urais.


ITAENDELEA

3 comments:

  1. Endelea tu kuongea kadri utakavyo lakini baada ya Octoba 25 tutataka uendelee kuongea kama hivi hivi.

    ReplyDelete
  2. Thanks polepole, ni kero sana kushabikia uraghai, cdm niwaraghai

    ReplyDelete