Friday, September 11, 2015

NI SAWA TUNATAKA MABADILIKO: JE NI YA MAGUFULI AU LOWASSA??


Tutafakari kwa Hoja na Sababu

Wagombea Urais wa CCM, Dr. John Magufuli na mwenzake wa CHADEMA Ndg Edward Lowassa wanakubaliana jambo moja kubwa: Haja ya kuwa na mabadiliko katika nchi yetu. Wagombea wote wameahidi kila mmoja kuwa iwapo atashinda ataleta mabadiliko. Tulinganishe sasa na kupima aina ya mabadiliko ambayo yanaweza kutokea iwapo mmojawapo atachaguliwa kuwa Rais wa nchi yetu.

Kulingana na historia ya utendaji wake katika wizara alizokabidhiwa na ahadi anazotoa mgombea wa CCM, Dr. John  Magufuli, chini ya Urais wake inaonekana  utawala wa sheria na nidhamu ya kazi kwa watumishi wa umma itatamalaki.  Magufuli anajulikana zaidi kwa Watanzania kuwa ni mtu anayesimamia sheria hata pale zinapogusa maslahi ya wakubwa zake. Watanzania watakumbuka jinsi Magufuli alivyoweza kurudisha magari yaliyokuwa yameporwa kinyemela  na vigogo wa serikali enzi za utawala wa Benjamin Mkapa.

Kwa upande wa  Ndg. Edward Lowasa, iwapo  atachaguliwa kuwa Rais, kuna uwezekano mkubwa kukawa na utawala unaotegemea hisia za Rais na ‘marafiki’ zake  badala ya utawala wa sheria. Utendaji wake wa nyuma unaonyesha wazi kuwa Lowassa kama kiongozi ni mtu anayeamini matashi yake binafsi bila kuzingatia utawala wa sheria. Watanzania watakumbuka kuwa March 2006, akiwa waziri mkuu, Lowassa alimfukuza kazi mhandisi wa Manispaa ya Temeke bila kumpa nafasi ya kujitetea na tena mbele ya waandishi wa habari na kundi la wananchi waliokuwepo katika tukio la kuporomoka jengo la Chang’ombe Village.  

Hivi karibuni, wakati anazindua kampeni zake, Lowassa alitoa ahadi kuwa ikiwa atashinda atamuchia huru Nguza Viking, maarufu kama Babu Seya aliyefungwa maisha jela kwa kwa kosa la  kubaka na kulawiti watoto katika hukumu iliyotolewa na mahakama ya hakimu mkazi kisutu mwaka 2004. Kesi hiyo ilipelekwa katika mahakama ya rufaa mwaka 2010 na Mahakama ilikubaliana na uamuzi wa mahakama ya chini. Tena, mwaka 2013, jopo la majaji wa mahakama ya rufaa watatu likijumuisha Jaji Nathalia Kimaro, Mbarouk Mbarouk na Salum Msati walifanya mapitio ya mahakama hiyo na kuwaona wafungwa hao kuwa wana hatia.

Ikumbukwe kuwa sheria za Tanzania zinamyima Rais mamlaka ya kusamehe watu waliofungwa kwa makosa ya kubaka na kulawiti. Kwa kutamka kuwa atawachia wazi wafungwa hao,bila ya kusema chochote juu ya wale watoto waliolawitiwa na kubakwa na haja ya kufuata utawala wa sheria nchini ni dhahiri kuwa katika utawala wa  Lowassa utawala wa sheria utawekwa kando na matashi ya watawala ndio yatakuwa yanaongoza nchi. Hili linadhibitishwa na ahadi nyingine  ya  Lowassa  kuwa  akiwa Rais, watuhumiwa wa kesi za ugaidi waliokamatwa huko Zanzibar wataachiwa huru kwa amri ya Rais. Ikumbukwe kuwa kwa sasa dunia iko kwenye vita dhidi ya ugaidi na ugaidi ni hatari kubwa na thahiri kwa maisha ya  wananchi na mali zao.

Wagombea wote wameahidi kupambana na ufisadi na rushwa iwapo watachaguliwa kushika nafasi ya Urais. Magufuli ameahidi wazi kuwa ataleta  mabadiliko katika vita dhidi ya rushwa na ufisadi kwa kuanzisha mahakama maalum ya kushughulikia masuala hayo. Kuna uwezekano mkubwa kuwa rushwa itaweza kudhibitiwa katika utawala wake ukizingatia kuwa katika harakati zake zote hakuungwa mkono na genge la mafisadi kama ilivyozoeleka kwa siasa za CCM tangu mwaka 2005 ilipotekwa na genge la wanamtandao.

Hali hii itamfanya aweze kutawala bila kuwa na  deni la kulipa fadhila kwa mtu yeyote. Uzoefu wa siku za karibuni unaonyesha kuwa rushwa na ufisadi mkubwa unasababishwa na kujaza ‘marafiki’ katika nafasi muhimu za maamuzi. Kujaza marafiki hasa waliokufadhili kwenye harakati za uchaguzi kunafanya mifumo ya uwajibkaji katika nchi iwe na ganzi ya kufanya kazi dhidi ya marafiki hao.

Kwa upande wake Lowassa hajaeleza atafanya nini bayana katika kupambana na rushwa zaidi ya kusema atashughulikia rushwa. Kama ambavyo ilibainishwa na waziri mkuu mstaafu na mpambe wa Lowassa katika harakati za Urais, Fredrick Sumaye,  katika viwanja vya jangwani, Lowassa ndiye mwasisi wa ‘mtandao’ uliomwingiza Rais Kikwete madarakani mwaka 2005. Kundi hili lilimjumisha pia Rostam Azizi na Laurence Masha ambao leo hii ndio pia ndio wanaongoza mikakati ya Lowassa. Rushwa katika mikataba ya aina mbalimbali na hata ukwapuaji wa fedha za umma kupitia maskandali mbalimbali kama EPA, Richmond  na Dowans ulifanyika kama njia ya kulipa deni la fadhila wakati wa uchaguzi. Kama tulivyogusia hapo juu, ni vigumu kuchukua hatua dhidi ya marafiki na maswahiba.

Baada ya CCM kujikomboa kutoka katika makucha ya wanamtandao kwa kuwaondoa wagombea wa kundi hili akiwemo Lowassa kwenye kinyang’anyiro cha kugombea Urais kupitia chama hicho, kundi hilo limeweza ‘kuiteka nyara’ CHADEMA na kupitia kwake vyama vikuu vya upinzani kupitia UKAWA. Lowassa amesema waziwazi kuwa fedha anazogawa kwa wananchi mbalimbali zinatokana na ‘marafiki’ zake. Kwa hiyo, kama atachaguliwa, utawala wa Lowassa utaendeleza utawala wa wanamtandao, na watanzania watarajie kushamiri kwa ufisadi nchini kwa sababu tulizoeleza hapo juu.

Watanzania watakumbuka kuwa kile kinachoonekana kuwa ni ushabiki wa kupindukia kwa Lowassa hauna tofauti na ushbiki uliokuwepo mwaka 2005  kwa Kikwete. Hii inatokana na ukweli kuwa kundi linaloratibu na kuongoza kampeni za Lowassa ni lilile lililofanya kazi hiyo mwaka 2005. Tayari, kuna taarifa zinazosema kuwa wanamtandao wameshagawana nafasi muhimu za uongozi na mikataba katika maeneo manono kama bandari, madini na vitalu vya gesi na mafuta iwapo watafanikiwa kuiteka dola kupitia uchaguzi.

Magufuli ameahidi kuwa ataleta mabadiliko katika utendaji wa watumishi wa umma kwa kuweka mifumo imara ya uwajibikaji. Watu walio karibu na Magufuli wanasema kuwa Magufuli ameahidi kuwa akiwa Rais atawekeana mikataba ya utendaji kazi (Perfomance contracts) na mawaziri wake ambapo kila waziri ataingia kama yeye binafsi na akishindwa kufikia malengo atawajibishwa kwa kuondolewa madarakani. Magufuli ameahidi pia kuwa mafisadi watakaotiwa hatiani watafilisiwa mali zao. 

Kwa upande wake Lowassa amesema kuwa akiingia madarakani atabadilisha mfumo wote wa nchi. Hii ina maana kuwa Lowassa akiwa Rais, taasisi za utawala kama vile Polisi, Jeshi, Utumishi wa Umma na vyombo vingine vitafumuliwa na kuundwa upya na kuwekwa watu wapya. Muhimu hapa ni kukubaliana  kuwa siyo rahisi kwa jambo hilo kufanyika kwa kuwa kama ilivyo duniani kote yeyote atakaye shinda atalazimika kufanya kazi na vyombo hivyo. Mabadiliko yeyote ya utendaji wa vyombo hivyo vitategemea na hulka, tabia na haiba ya Rais. Hakika duniani kote mabadiliko katika nchi huletwa kwa vyombo hivyo kufanya kazi zao ipasavyo kutokana na uongozi na usimamizi dhabiti wa mkuu wa nchi.

Hitimisho


 Haya ni baadhi ya mabadiliko yanaweza kutokea iwapo mmoja wa wagombea wetu watachaguliwa katika nafasi ya Urais. Mabadiliko haya yanaonyesha wazi kuwa uchaguzi ni muhimu sana kwa mustakabali wetu kama mtu mmoja mmoja na kama Taifa. Kwa sababu hiyo, ushabiki na uungwaji mkono wa wagombea lazima uzingatie faida na hasara zake kwa nchi na kwetu binafsi. Ni wakati wa kuwahoji na kuwatathimini wagombea wetu ili siku ya upigaji kura tisije tukafanya kosa litakalotuathiri sisi na vizazi vyetu.  Tathmini hiyo ni muhimu kwa kujua kuwa utendaji kazi wa Rais huakisi na kuathiri utendaji kazi wa serikali na taasisi zote zilizo chini yake. Yaani Rais akiwa fisadi serikali na vyombo vyote chini yake vitakuwa vya kifisadi. La, Rais akiwa mwadilifu na mchapakazi na serikali yake itakuwa vivyo hivyo. 

1 comment:

  1. asante kwa uchambuzi mzuri japo umesahau kuelezea uuzwaji wa wa nyumba za selekali ambapo magufuli anahusishwa. Binafsi nakubaliana na wote wanaotaka mabadiliko lakini pia sikubaliani na njia wanayotaka kuitumia. Mimi nimekuwa mpinzani wa Lowasa tangu alipokuwa anatafuta kuteuliwa na Chama chake CCM kwasabu naamini kama angeteuliwa na mwisho angekuwa raisi nchi ingeendelea kuendeshwa kwa kulipana fadhila kama ilivyokuwa enzi za JK. Wanamtandao walimwingiza Ikulu, baada ya hapo likaundwa baraza la mawaziri la watu 60, Lowasa akawa waziri mkuu na baada ya muda mfupi wakatuletea Richmond. Ilikuwa ni kulipana fadhila tu. Nashukuru mwaka huu Mwenyekiti wa CCM amehakikisha mtandao ulomwingiza yy mwenyewe madarakani hauendelei kuitesa nchi. Bila shaka Lowasa akiwa raisi ufisadi utashika hatamu. Nafikiria alitumia pesa kiasi gani kuhakikisha wale wajumbe waloimba wana imani na LOwasa pale NEC Dodoma. mipesa alokuwa anamwaga kwenye HARAMBEE ambayo alikuwa anadai anapata toka kwa marafiki zake. Mwisho wa siku akiingia madarakani hao marafiki zake watakuwa hawalipi kodi wala hawaguswi na yeyote. Na nadhani mbaka sasa hakuna tajiri aliyezoea ujanja ujanja anayependa Magufuli aingie ikulu. mana itakuwa shida kwake.

    Mwisho sina uhakika kama magufuli ataweza kupambana na watu wa rushwa kubwa kama alivoahidi mana mfumo wa mahakama zetu tunaujua. majaji wapo mifukoni mwa matajiri...na p[ia wanaweza waka M'SOKOINE

    Kingine Mgufuli amesahau kabisa kuongelea vita ya madawa ya kulevya.cjui anaogopa????

    0685818951

    ReplyDelete