Monday, April 13, 2015

TCD MSIPOLISEMEA HILI LA MAREKEBISHO YA KATIBA YA 1977, MTAPOTEZA HESHIMA YENU

Hatuwezi kwenda kwenye uchaguzi mkuu hivi hivi

Kuahirishwa kwa Kura ya Maoni

Wiki iliyopita nilieleza furaha yangu baada ya serikali kupitia Tume ya Taifa ya Uchaguzi kuahirisha Kura ya Maoni iliyokuwa ifanyike tarehe 30 Aprili, kitendo cha serikali ni cha kiungwana licha ya kwamba kimekuja kwa kuchelewa sana. Serikali kwa ukubwa wake na taasisi zake lukuki ambazo nyingine zimepewa hata dhamana ya kutumia intelijensia kuyaelewa mambo na kutoa ushauri stahiki kwa viongozi wetu, hatukutarajia tupige kelele kwa miezi mitano kusema Kura ya Maoni haiwezekani mwaka 2015, na hasahasa mwezi wane. Sote tulijua bado hatukuwa na vifaa (BVR) vya kuwaandikisha watu, sote tulijua tunatumia mfumo mpya kuwaandikisha watu na hivyo kutarajia sintofahamu kadhaa wa kadhaa, sote tulijua sheria ya Kura ya Maoni ilikuwa imeweka utaratibu na masharti ya kuzingatiwa kabla ya kwenda kwenye zoezi la Kura ya Maoni, na sote tunajua masharti hayo na utaratibu kwa kiasi kikubwa haukuwahi kufuatwa.

Zaidi ya yote, kila mtu anajua kwamba mpaka mwezi wa pili kwenda wa tatu na hata leo bado tunaendelea kugawa Katiba Inayopendekezwa kwa umma wa watanzania. Na sote tunafahamu kwa serikali yetu imechapa nakala milioni mbili za Katiba Inayopendekezwa ambayo ni wastani wa Katiba Inayopendekezwa moja inapaswa kusomwa na watu kati ya 12 hadi 13. Katiba Inayopendekezwa moja kusomwa na watu 12 au 13, tafsiri yake ni kwamba, wewe ambaye hujapata kuiona Katiba Inayopendekezwa kuna wenzake 11 au 12 ambao wakimaliza kusoma ndipo na wewe itafika zamu yako, kuwa mvumilivu maana sasa una muda wa kutosha.

Ilikuwa bayana pia kwamba tusingeweza kwenda kwenye Kura ya Maoni tukiwa tumegawika kabisa, kisiasa na kiimani. Kura ya Maoni ingeendeleza mpasuko ambayo kuuziba ingetugharimu zaidi kama Taifa. Na kama ambavyo utakuwa umefuatilia, dini zote mbili zina madai na kwa msingi huo, zote hazijaridhika na zote zilishajipanga kupiga kura ya Hapana. Kwa maneno mengine tarehe 30 Aprili angekuwa ni mtu basi angeshakuwa mhanga wa mpasuko wa kijamii na kwa maana hiyo tokeo lolote la Aprili 30 lingekuwa limepasua Taifa kuliko kutujenga.

Nyote mmeshuhudia kwamba kuelekea Kura ya Maoni Aprili 30 ambayo sasa imeahirishwa tulikuwa tayari na mpasuko mkubwa wa kisiasa, vyama vikubwa vilikuwa vimesusia kushiriki katika zoezi la Kura ya Maoni. Kuna baadhi ya watu walichukulia mzaha kwamba hata wakisusia kama vyama itakuwa kazi bure iwapo watu watajitokeza na kushiriki katika Kura ya Maoni. Baadhi ya watu hawa walienda mbali zaidi na kuhamasisha kwamba watu wapuuze msimamo wa vyama kususia na badala yake wakashiriki Kura ya Maoni. Mimi kwa mfano chama changu hakikususia, na nilikuwa nimejiandaa kwenda kupiga kura ya Hapana na vivyo hivyo nikajaribu kulisemea hili kwamba kuna tofauti kubwa kati ya msimamo wa chama kama taasisi na haki ya mwananchi kushiriki katika shughuli za umma ikiwemo kupiga kura ya maoni.

Watu huenda kupiga kura kama raia wa Tanzania, na hushiriki zoezi la kupiga kura kama haki yao ya kimsingi na haijalishi watu hawa ni wanachama wa chama cha siasa au la. Chama cha Siasa kama taasisi inayotambuliwa kisheria (rejea Sheria ya Vyama vya Siasa Sura ya 258), kina uongozi, kina utaratibu wa kufanya uamuzi kupitia vikao na kadharika,chama kinaweza kutoa msimamo, kufanya uamuzi na uamuzi huo usiingiliwe na uhuru wa raia mmoja mmoja kutumia haki zake katika Jamhuri yetu. Kwahiyo vyama vikisema tunasusia Kura ya Maoni hilo ni tatizo na wa kulitatua sio wananchi bali ni vyama kukaa na kutatua matatizo yaliyopo miongoni mwao.

Makubaliano ya Rais na TCD

Juzi juzi hapa nikapata kusikia jamaa yangu mmoja ambaye alisemalo mara nyingi huwa ama huwa lina wakilisha msimamo, huyu jamaa ni kama mpishi, mpishi akikwambia leo hakuna nyama ni maharagwe usimbishie maana yeye anakaa jikoni kila wakati, anajua. Katika mazungumzo anaonesha kana kwamba hakuna kitu kama Makubaliano ya Rais na Kituo cha Demokrasia Tanzania (TCD). Watu kama hawa huwa sio wa kupuuzwa hata kidogo, lakini kubwa ni kwamba yeye namshukulia kama mwakilisha fikra, na mimi nawaeleza ninyi wanachama wa TCD. Napenda kuwaeleza kwamba Tanzania na watanzania waliona mwanga kupitia ninyi, waliwaamini na kuwaheshimu, nawasihi enendeni kwa moyo huyo.

Naomba niwakumbushe, siku Mhe. Cheyo anasoma Makubaliano ya Rais na TCD, kushoto kwake aliketi Mhe. Dovutwa na kushoto kwa Mhe. Dovutwa aliketi Mhe. Philip Mangula. Kwa ishara hii ya umoja na mshikamano wa TCD, tusaidie watanzania kuvuka kipindi hiki chenye changamoto nyingi. Ninyi (viongozi na wanachama wa TCD) mnajua fika, na ninajua mnajua na mko katika nafasi ya kujua ukweli wa mambo kwamba hatuwezi tena kuwa na Kura ya Maoni mwaka huu. Kinyume na fikra hiyo ni kujaribu kulazimisha mambo halafu mwishowe tuharibu kila kitu, na ninauhakika miongoni mwenu kuna wazee wenye hekima na wenye hofu ya Mungu, mnajua fika kwa joto la kisiasa lilipo sasa hivi kuelekea uchaguzi mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani, kimsingi haiwezekani tena kuchomeka Katiba Inayopendekezwa ili ipigiwe Kura ya Maoni.

Juzi waziri mmoja wa zamani akaandika katika mitandao ya kijamii, kulikoni katika chama cha Mapinduzi, mbona kimya mpaka sasa kuhusu kinyang’anyiro cha watangaza nia ya Urais kupitia CCM ilhali kila kitu kinapaswa kuwa kimekamilika ifikapo mwezi Mei. Swali la makusudi kutoka kwa mwanasiasa huyu maarufu, ni ishara inayotuonesha uzito wa hali ilivyo kisiasa nchini, huku kwenye CCM peke yake kuna hali ngumu, kuna joto mithiri ya tanuruni, bado kwenye vyama vinavyoboresha mawazo (wengine wanaita vyama vya upinzani) vinyang’anyiro bado. Katika ngazi za ubunge, wabunge wa sasa pamoja na watangaza nia za ubunge wote akili zinawapaa kujaribu kuwapa maneno matamu matamu ya lala salama au maneno matamu ya kufunga uchumba kwa miaka mingine mitano au mwanzo mpya wa miaka mitano.

Kama kwenye Urais na Ubunge watu hawalali mpaka kieleweke, kwenye udiwani, vikumbo ni zaidi katika ngazi ya kata. Sasa nikuulize unadhani Taifa liko katika akili iliyotulia ya kuipigia Kura ya Maoni Katiba Inayopendekezwa kwa maana viongozi wetu waongoza kampeni ambao wengi ni wanataka kuendelea kushikilia majimbo au wametingwa na kutangaza nia pamoja na wananchi raia mmoja mmoja ambao saizi tunatathmini nani abaki na nani asirudi na kwanini abaki na kwanini asirudi. Hivi kweli ukituongezea na Katiba Inayopendekezwa si utatuvuruga?

Kibaya zaidi, kitendo chochote cha kuchanganya Kura ya Maoni na Uchaguzi Mkuu itakuwa ni dhambi kubwa kuliko, tutageuza Mchakato wa Katiba na Katiba Inayopendekezwa kuwa ajenda ya uchaguzi, hilo litavuruga maana ya Katiba isiyopasualiwa kisiasa katika ya ndio na hapana zinazohamasishwa kwa minajiri ya siasa zetu ambazo mara nyingi huwa hazina maslahi ya umma mpana wa watanzania.

TCD, nawasihi tena, kutaneni na jadilini, huyu Rais wetu ni muungwana na msikivu, mkimweleza kwa hoja hizi na zenu nzuri zaidi atawaelewa na twaweza kuona Bunge lijalo tukijadili marekebisho ya Katiba ya Mwaka 1977 ili tuvuke salama katika Uchaguzi Mkuu. Msipofanya hivyo, viongozi wangu wa CCM, CHADEMA, NCCR-MAGEUZI, TLP na UDP kama sehemu ya TCD, mtapoteza imani yenu mbele ya umma wa watanzania. Nawasihi fanyeni hili kwa maslahi ya Taifa na zaidi tumsaidie Mhe. Rais amalize na Uchaguzi kwa mara ya kwanza usio na tashwishwi wala waa na huo utakuwa sehemu ya utumishi wake uliotukuka kwetu na sisi kwa hakika tutamkumbuka ikiwemo pamoja na mchakato wa Katiba ambao tutaendelea nao mwakani. Na wala msihofu, tukifanya marekebisho, lazima tutatunga na masharti yatokanayo na masharti ya mpito na mojawapo ya kazi za kikatiba kwa Rais ajaye na Serikali yake ni kuendelea na Mchakato wa Katiba, sio utashi bali ni takwa la kikatiba.

Fursa ya Mjadala

Kilichobaki sasa ni kuendelea kujadiliana kuhusu mchakato wa Katiba, Rasimu ya Warioba, Katiba Inayopendekezwa na tuulizane maswali na kupeana majibu. Kama ilivyo ada wikendi hii Taasisi ya Mwalimu Nyerere imeandaa Mdahalo wa Katiba huko Mbeya, ni sehemu ya kujadiliana. Na ninawasihi Taasisi ya Mwalimu Nyerere wasiishie hapo, waende na mikoa mingine mingi zaidi maana elimu hii inahitajika sana.

Tunapojiandaa kisaikolojia na Uchaguzi Mkuu

Tuipe Tume ya Taifa ya Uchaguzi ushirikiano wa kutosha wanapoendelea na zoezi la uandikishwaji wapiga kura. Tujitokeze kwa wingi kuandikishwa na kupata vitambulisho vya mpiga kura, bila kitambulisho cha mpiga kura hutaweza kutumia haki yako kufanya uamuzi wa ni nani na nani wapewe dhamana ya kukuongoza katika ngazi ya kata, jimbo na Jamhuri yetu.


Wito, kwa unyenyekevu niwasihi serikali msiwaingilie Tume wanapotenda kazi yao, wapeni uhuru wa kutosha kama ambavyo wanapaswa kuwa. Waacheni ili watanzania kwa muda huu uliobaki wapate huduma ya Tume bila matatizo. Rai yangu kwa vyama vya siasa, jipangeni, pigeni siasa safi, jengeni hoja, toeni sababu na onesheni ushahidi, watu watawaelewa tu, ila achene kuisakama Tume ya Uchaguzi bila sababu, maana hiyo ni tabia mbaya.

No comments:

Post a Comment