Saturday, April 18, 2015

KUHUSU MAADILI YA VIONGOZI, KATIBA INAYOPENDEKEZWA IMEPUUZA KILIO CHA WENGI JUU YA UADILIFU WA VIONGOZI

Mhe. Rais na Makamu wa Rais wakipata picha ya pamoja na wajumbe wapya wa Tume ya Maadili
Kudhoofisha maadili ya uongozi ni sawasawa na madaraka pasina udhibiti

Maadili na uwajibikaji wa viongozi wa Umma

Tanzania, kama ilivyo nchi nyingine za Kiafrika, ina changomto za kiuwajibikaji na wananchi wametoa mawazo yao wakati wa mchakato kukusanya maoni kuhusu Katiba mpya. Wananchi walizungumzia changamoto za uwajibikaji kwa viongozi wa umma na wakatoa sababu na mantiki ya kuunda mfumo thabiti wa uwajibikaji.

Uwajibikaji ni dhana pana, inahusu utaratibu endelevu wa udhibiti na uwekaji wa mipaka katika matumizi ya madaraka. Vilevile, ina maana ya kuwepo utaratibu wa kuwalazimisha wenye madaraka kufanya wanayotakiwa kuyafanya na kuacha kufanya wasiyotakiwa kuyafanya na ya kujibu maswali au hoja zinazohusiana na matumizi ya madaraka aliyopewa. Kwa mantiki hii, uwajibikaji unamaanisha pia kipengele cha adhabu kwa wale wanaotumia madaraka ya umma vibaya. Kwa hiyo, dhana ya uwajibikaji inahusu masuala yafuatayo: kwanza, uwepo wa mfumo wa udhibiti wa madaraka; pili, uwepo wa utaratibu wa kuwalazimisha wale walio na madaraka kutekeleza wajibu wao na kuwazuia kukiuka wajibu wao; na tatu, kuwepo utaratibu wa kuwaadhibu wenye madaraka pale wanapokosea.

Kwa upande mwingine, maadili maana yake ni kanuni au misingi inayoelekeza ni kitu gani kibaya au kisichofaa au kizuri au kinachofaa. Misingi hii inaweza kujengwa katika utamaduni wa jamii husika. Vilevile, misingi hiyo inaweza kuandikwa na kwa kanuni ya maadili. Kwa maneno mengine na hasa kwa hali ilivyo katika nchi yetu sasa na hata kwa vizazi vijavyo kuna umuhimu mkubwa wa kuweka masharti mahususi ya maadili ya viongozi katika Katiba kama sehemu ya kujenga utamaduni wa kikatiba wa kuendelea kudhibiti matumizi ya madaraka.

Kuna aina nyingi za uandishi wa Katiba, moja ni ile ambayo kitaalamu huitwa “instrumentalist approach” Katiba hizi huwa hazijipambanui sana, kwa asili yake huwa zinaweka misingi na kujenga taasisi, huwa fupi na maeneo mengi huja kufanyiwa kazi na sheria zitakazotungwa na Bunge. Aina ya pili ni ile inayoitwa “Programmatic approach” ambayo huwezesha uandishi wa Katiba za mfano wa Katiba ya uhuru wa Taifa la Ireland. Ni Katiba ambayo huweka bayana ndoto, malengo makuu na misingi ya mwelekeo wa shughuli za serikali na sera za kitaifa ambazo kwa ujumla wake katika Katiba hutanabaisha dira ya nchi.

Katiba ambazo ni programmatic huweka ndani yake pia masharti mahususi juu ya misingi ya Taifa, misingi juu ya maadili ya Taifa, misingi ya maadili ya viongozi sambamba na utaratibu wa uwajibikaji kwa viongozi wa umma. Moja ya changamoto kubwa katika taifa lolote lile ni namna gani Taifa linaweza kuwa na mfumo wa kikatiba ambao unawazuia viongozi wa Serikali kuyatumia madaraka ya umma vibaya.

Mwanafalsafa wa Uskochi David Hume katika Karne ya 18, alipata kunena haya, “tunapotengeneza mfumo wa Serikali katika Katiba na kuweka udhibiti na urari wa madaraka ni vizuri kuzingatia kuwa kila mtu siyo mwaminifu na kwamba binadamu yeyote katika matendo yake mengi huwa hana malengo mengine isipokuwa kutafuta manufaa binafsi. Hume anaendelea kusema ni lazima kuweka utaratibu wa kuyadhibiti madaraka hayo ili mtu huyo aweze kutoa ushirikiano wake katika masuala ya umma. Anaonya kuwa tusipofanya hivyo tutajisifu kuwa tuna katiba lakini kumbe hatuna usalama wa mali na uhuru wetu isipokuwa tu kwa matakwa ya watawala au viongozi wetu, na jambo linapotolewa kwa utashi wa viongozi na hasa katika mambo ya msingi kama hatutakuwa na usalama kabisa. Kwa ujumla, mwanafalsafa huyu anaeleza kuwa madaraka wanayopewa viongozi ni lazima yadhibitiwe kikatiba; haifai kumwamini mtu kwa sababu ni vizuri kila mtu achukuliwe siyo mwaminifu au kwa kimombo anasema “every man ought to be supposed a knave”.

Maadili katika Rasimu ya Warioba ukilinganisha na Katiba Inayopendekezwa

Rasimu ya Katiba Toleo la Pili ilijaribu kwa mara ya kwanza baada ya marekebisho makubwa yaliyofanyika mwaka 1984 kwa Katiba ya Mwaka 1977 yaliyoigeuza kwa sehemu Katiba ya Mwaka 1977 kuwa “programmatic”. Licha ya marekebisho hayo bado Katiba ya mwaka 1977 haikuwa imejipambanua ipasavyo ili kuendana na mahitaji ya wakati, yaliyohitaji misingi ya maadili na uwajibikaji pamoja na uanzishwaji wa taasisi huru za kusimamia maadili na uwajibikaji wa viongozi wa umma.

Wengi wenu mtakuwa mlishuhudia kile kilichokuja kuwa maarufa miongoni wa mitandao ya kijamii kama sinema ya Baraza la Maadili. Iliitwa sinema kwasababu watuhumiwa waliopata kuhojiwa katika baraza letu la Maadili chini ya Jaji Msumi hawakuonekana kuitetemekea Mamlaka ile ambayo ndio ina dhamana ya kuwawajibisha viongozi wanaokwenda kinyume na maadili ya uongozi. Hata pale waandishi walipomhoji mwenyekiti wa Baraza juu ya hatima ya viongozi wale, aliishia kusema wakimaliza kazi watapeleka taarifa kwa mamlaka za juu. Swali ambalo wananchi wamekuwa wakijiuliza ni vipi pale ambapo wanaohojiwa ni viongozi na watumishi kutoka mamlaka ya juu? Je utekelezwaji wa mapendekezo ya Baraza utazingatiwaje katika mazingira hayo?, haya si maneno yangu ninayasikia huku na huko.

Tunaposema kwamba Katiba Inayopendekezwa imetupilia mbali masharti mahususi kuhusu maadili ya uongozi, hebu tutizame mfano huu;- Ibara ya 15 ya Warioba ilisema “Kiongozi wa umma wakati anapotekeleza shughuli zakiserikali, akipewa zawadi, zawadi hiyo itakuwa ni mali ya Jamhuriya Muungano na ataiwasilisha kwa Katibu Mkuu Kiongozi kupitiakwa Katibu Mkuu wa Wizara au kiongozi wa taasisi ya Serikaliinayohusika, akiainisha: (a) aina ya zawadi; (b) thamani ya zawadi; (c) sababu ya kupewa zawadi; na
(d) mtu au mamlaka iliyotoa zawadi hiyo”. Kifungu cha pili cha Ibara hii kinasema “Neno “zawadi” kama lilivyotumika katika Ibara hii linajumuisha kitu chochote chenye thamani atakachopewa Kiongoziwa umma katika utekelezaji wa shughuli za umma. (3) Bunge litatunga sheria itakayosimamia, pamoja na
mambomengine, thamani, kiwango, aina na uhifadhi wa zawadi kwa Jamhuri ya Muungano.

Katiba Inayopendekezwa imeiboresha Ibara hii na kuandika Ibara ya 29(2)(a) ambayo kwa jumla inasema “Kwa madhumuni ya Katiba hii, Bunge litatunga sheria itakayoweka, pamoja na mambo mengine: (a) tafsiri ya neno zawadi, aina, thamani, kiwango na uhifadhi wa zawadi ambayo kiongozi anapokea wakati akitekeleza
majukumu yake.

Nikitazama kwa kina maboresho hayo utagundua masharti ambayo wananchi walikuwa wanayapendekeza kuwa yawepo katika Katiba kama masharti mahususi, Katiba Inayopendekezwa imeyatupilia mbali na kuacha ombwe hilo kufanyiwa kazi na Sheria zitakazotungwa na Bunge. Ikumbukwe hata wabunge ni viongozi na masharti haya kikatiba yangewawajibisha hata wao na kama yasingefutwa basi wangelazimika kutunga sheria ambazo misingi yake imo katika Katiba tofauti na mtindo wa uandishi wa Katiba Inayopendekezwa ambao unawapa viongozi nguvu za kutumia utashi wao kutunga masharti ya kuwawajibisha na kuwadhibiti viongozi wao wenyewe. Kwa maneno mengine misingi ya kuwadhibiti viongozi wetu na namna wanatumia madaraka yao inapaswa iwekwe kwenye Katiba na wananchi na si viongozi waje kujitungia masharti ya kuwadhibiti wao wenyewe, hawatatenda.

Warioba alisema katiba Ibara ya 16 kwamba “Kiongozi wa umma - (a) hatafungua au kumiliki akaunti ya benki
nje ya Jamhuriya Muungano isipokuwa tu kwa namna ambayo sheria za nchi zinaruhusu; na (b) hataomba au kupokea mkopo au faida yoyote kwa namnaau mazingira ambayo yanashusha hadhi au heshima ya utumishi wa umma”.

Ukiitizama Katiba Inayopendekezwa namna ambavyo imeiboresha Ibara hii katika Ibara ya 29(2) inasomeka kama ifuatavyo “Kwa madhumuni ya Katiba hii, Bunge litatunga sheria itakayoweka, pamoja na mambo mengine: (b) masharti ya kufungua akaunti za nje kwa kiongozi wa umma.

Hivi kweli ukisoma Ibara za 15 na 16 za Rasimu ya Warioba, je uboreshwaje wake ni kama ulivyowekwa katika Ibara ya 29(2) ya Katiba Inayopendekezwa? Tafakarini kwa kina kabla ya kusema Katiba Inayopendekezwa ni Bora Afrika.

Warioba alisema katiba Ibara ya 21(3) kwamba “Kiongozi wa umma ambaye anatuhumiwa kwa makosaya: kimaadili; (b) udhalilishaji wa mtu au wa kijinsia; au (c) wizi au ubadhirifu wa mali za umma, atasimamishwa kazi hadi suala lake litakapoamuliwa kwa mujibu washeria za nchi au taratibu nyingine zinazowahusu viongozi waumma.

Katiba Inayopendekezwa imeyafuta kabisa masharti haya, kwa msingi huu tusishangae kiongozi anayetuhumiwa kwa masuala tajwa hapo juu akaendelea kutoa huduma kwa wananchi ilhali tukijua mzizi wa tatizo uko kwa kiongozi au mtumishi huyo wa umma.

Katiba Inayopendekezwa inapokuja katika suala la Maadili kwakweli haijawatendea haki watanzania, hasa katika kipindi hiki ambapo taifa letu limepitia katika kufichuka kwa tuhuma na kashfa za ufisadi mkubwa katika taasisi zetu za serikali tena karibu katika ngazi zote.

Labda kabla ya kuwaacha niwape mfano wa mwisho, Ukiangalia Tume ya Maadili na uwajibikaji utagundua kwa sababu ambazo hazieleweki masharti mengi na muhimu yaliyokuwa sehemu ya majukumu ya Tume ya Maadili kwa Rasimu ya Warioba yamefutiliwa mbali katika Katiba Inayopendekezwa. Rejea masharti ya ibara ya 203(2)(b), (e) hadi (o) ya Rasimu ya Tume, juu ya majukumu ya Tume ya maadali yauongozi.Ukisoma kifungu cha 231 cha Katiba Inayopendekezwa masharti hayo yamefutwa.

Hakika Katiba Inayopendekezwa itaturudi nyuma kabisa katika uandishi bora wa Katiba Barani Afrika, lakini fursa ya kuirekebisha kabla haijawa rasmi mpya iko pale pale ukirejea kifungu cha 35(3) na (4) cha Sheria ya Kura ya Maoni.

Karibu kutoa Maoni



1 comment: