Sunday, September 17, 2017

HATUTARUDI NYUMA KATIKA JITIHADA ZETU ZA KUPINGA UDHALIMU NCHINI


HATUTARUDI NYUMA KATIKA JITIHADA ZETU ZA KUPINGA UDHALIMU NCHINI

Uhuru wetu wa kisiasa ni kazi bure pasina kuumiliki na kuudhibiti uhuru wetu wa kiuchumi

Mageuzi Makubwa ya Chama na Serikali

Tunapitia kipindi cha tofauti katika historia ya Taifa letu, kipindi ambacho naweza kukiita kipindi cha mpito, hiki ni kipindi ambacho tunatoka katika hali moja na tunapaswa kwenda kwenye hali nyingine ambayo ni bora zaidi.

Kipindi hiki cha mpito kinaongozwa na kauli mbiu ya CCM Mpya Tanzania Mpya. Ni kipindi ambacho Chama Cha Mapinduzi (CCM) kimeamua kujitizama kitofauti, kimeamua kujitafakari na kujihoji, maswali yafuatayo na kwa ufupi, tumetoka wapi, tuko wapi na tunataka kwenda wapi.

Chama Cha Mapinduzi (CCM) kimejitizama mwenendo wake, matendo yake, itikadi yake, siasa yake, dhamira yake, malengo yake na Imani yake. Kisha Chama kikaenda mbele kikatizama viongozi wake, nidhamu yao kwa Chama, tabia zao, mienendo yao, matendo yao, na kuoanisha hayo yote na ahadi tisa za mwanachama wa CCM.

Chama kikachukua muda zaidi kuangalia sauti za wanachama wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) ambazo mara zote zimeendelea kuelekeza nini mwelekeo sahihi wa CCM chama ambacho si tu ni Chama kilichopo madarakani lakini ni Chama kikubwa Tanzania na Afrika.

Tafakuri hii ndefu ya CCM ndiyo iliyopelekea kuandikwa kwa waraka wa Chama uliopewa jina la “Umuhimu wa kufanya Mageuzi ndani ya Chama”.

Katika waraka huu wa Mageuzi inafafanuliwa kwamba kabla ya awamu ya tano, suala la rushwa (ufisadi) limekuwa ni mzigo mkubwa ambao Chama chetu kimebebeshwa. Pamoja na juhudi kubwa ambazo serikali ya awamu ya nne ilifanya katika kupambana na rushwa ikiwa pamoja na kutunga sheria mpya wakati huo, kuiunda na kuiimarisha taasisi yetu ya kupambana na rushwa na kutunga sheria ya kudhibiti Matumizi ya Fedha za Uchaguzi wananchi bado waliona Chama chetu kilikumbatia wala rushwa.

Chama baada ya tafakuri jadidi na shirikishi kikaamua kwa kauli na sauti moja kufanya Mageuzi makubwa yatakayokitoa Chama Cha Mapinduzi (CCM) katika mwonekano huu hasi mbele ya umma wa wanachama na wananchi na kuwa Chama ambacho kinamaanisha kwa maneno na matendo chuki yake dhidi ya rushwa na wala rushwa.

Mageuzi Makubwa yanalengwa katika Chama chenyewe (CCM) na katika Serikali.

Mwelekeo ni kukifanyia Chama Mageuzi makubwa katika mawanda ya Kiuongozi, Kimuundo na Kiutendaji. Mageuzi haya katika mawanda haya matatu yataongeza tija, ufanisi, uwajibikaji, faida, itapunguza gharama za uendeshaji wa Chama na huduma za wanachama zitaboreka zaidi.

Mageuzi haya katika Chama msingi wake ni kukirejesha Chama chetu kwa Wanachama na kuimarisha msingi wa kuwa chama kinachoshughulika na shida za watu.

Mojawapo ya sababu za hamasa ya Mageuzi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) tunaipata kutoka kwa Mwalimu Nyerere katika kitabu cha Binadamu na Maendeleo katika ukurasa wake wa 18 na 19, Mwalimu anasema “ Kazi ya Chama Cha Siasa kilicho imara ni kuwa kama daraja la kuwaunganisha watu na serikali waliyoichagua, na kuiunganisha serikali na watu inayotaka kuwahudumia...”

Mwalimu Nyerere anaendelea kusema katika kitabu hiki “…Ni wajibu wa Chama kuwasaidia watu kuelewa serikali yao inafanya nini na kwa nini; ni wajibu wake kusaidia watu kushirikiana na serikali yao kwa juhudi ya pamoja ili kuundosha umasikini ambao umetulemea. Na ni wajibu wa Chama pia kuhakikisha kwamba serikali inaendelea kuyajua sana maoni, shida na matakwa ya watu…”

Aidha Mwalimu Nyerere anatukumbusha katika kitabu hiki “…Ni wajibu wake (CCM) kuwasemea watu. Pia ni wajibu wake kuwaelimisha watu na kuwasaidia kuona shughuli za serikali zina maana gani kuhusu usalama wao wenyewe wa siku zijazo na fursa zao wenyewe za siku zijazo”

Tangu Uongozi wa Awamu ya Tano uingie madarakani mwaka 2015 kupitia tiketi ya CCM chini ya Ndugu yetu John Pombe Joseph Magufuli Mageuzi Makubwa yanaendelea kufanyika katika Serikali na taasisi zake katika maeneo ya utolewaji wa huduma, nidhamu ya ukusanyaji wa mapato na matumizi ya fedha za serikali, kuimarisha zaidi mapambano dhidi ya rushwa hasa ufisadi na uhujumu uchumi, kupambana na biashara haramu ya dawa za kulevya, kukabiliana na kudhibiti mtawanyiko haramu wa silaha za moto, kuwakabili na kuwachukulia hatua kali wakwepa kodi, walanguzi, watakatisha fedha na kushughulika na wote wale ambao kwa matendo yao uchumi wa nchi na ustawi wa watu wake unawekwa rehani.

Mageuzi haya makubwa hayaji katika sahani ya fedha mezani, ni kazi ngumu, napenda nikiri ina upinzani mkubwa, iko bayana kwamba kwa watu wasio wema na wasio na mapenzi mema na maendeleo ya nchi hawafurahishwi na Mageuzi makubwa yanayofanyika ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) na katika Serikali.




Tafsiri ya Mageuzi ya CCM

Baada ya tafakuri kubwa na kusikiliza sauti za wananchi, CCM imenia na inatenda kwa uhalisia kukirejesha Chama kwa wanachama. Kuna wakati Chama kilionekana ni pango la maharamia, kila mkwepa kodi alikuwa na uhusiano na CCM, hili lilichafua sana taswira ya CCM. Taswira hii mbaya imechafua heshima ya Chama chetu na kukifanya kinuke, lakini idadi ya kutosha ya wachafuzi wa Chama chetu wamekuwamo ndani ya CCM yenyewe. Baadhi ya wachafuzi hawa wa taswira na heshima ya Chama chetu ni viongozi katika Chama chetu katika ngazi mbalimbali.

Kwa msingi huu, Mageuzi Makubwa katika Chama yanatizama eneo la Uongozi; Chama kinataka aina ya viongozi ambao watanzania wanawataka. Viongozi wachapa kazi, waaminifu, waadilifu, wanyenyekevu, wanaochukizwa na rushwa, wanaochukizwa na ubadhirifu wa mali za Chama na Mali za Serikali, viongozi wasio wabinafsi bali wanaowaweka wanachama kwanza, viongozi wapole lakini wakali kwa mambo ya hovyo, viongozi wanaoziishi imani za Chama Cha Mapinduzi (CCM), Viongozi wanaoziishi ahadi za mwana CCM, viongozi wasioukamia Uongozi, hawa ni viongozi ambao watakubalika si kwa fedha bali kwa mienendo yao mema na maono yao ya kiuongozi kwa Chama chetu katika ngazi husika na kwa umma wa watanzania hata wale ambao sio wana CCM.

Ukiwa na aina hii ya viongozi CCM inaamini chama chetu kitakuwa imara na madhubuti zaidi na kitasimamia haki za wanachama na wananchi kwa ujumla. Tukiwa na viongozi wa aina ambayo nimeieleza kwa uchache hapo juu, hawa ndio wataisimamia serikali kutoka ngazi za msingi katika Serikali za Mitaa na Vijiji, Serikali za ngazi ya Kata, Serikali katika ngazi ya Wilaya na Halmashauri mpaka katika Mikoa, Miji na Majiji ya Nchi yetu.

Viongozi wa aina hii, hawahongeki, hawapokei wala kutoa rushwa, ni wakali sana kwa wote wanaofanya ubadhirifu wa mali za Chama na Mali za Umma. Viongozi hawa ambao Chama Cha Mapinduzi (CCM) kinaendelea kuwapata katika uchaguzi wake wa ndani mwaka huu wa 2017 wanapenda HAKI na wanaheshimu wanachama wa CCM na wananchi wa Tanzania.

Kama nilivyotangulia kusema viongozi wa aina hii huzongwa sana, hufanyiwa fitina na hufanyiwa kila aina ya hila. Chama kimejipanga ipasavyo kuhakikisha ya kwamba haki itasimamiwa ipasavyo, na majizi, na wote ambao wamekuwa wakijinufaisha na mali za Chama kwa faida yao kinyume na Ahadi ya Mwana CCM hawatopewa nafasi ya kuwa viongozi katika Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Chama Cha Mapinduzi (CCM) kinaongozwa kwa Katiba, Kanuni mbalimbali, desturi njema na dhamira na utashi mwema wa viongozi wetu, chini ya Uenyekiti wa Komredi Dkt. John Pombe Joseph Magufuli.


Msingi wa kutokurudi nyuma

Kipindi hiki tunapofanya Mageuzi haya Makubwa napenda ifahamike wako baadhi yetu ambao watashindwa kwenda na mwendokasi wa Mageuzi haya makubwa.

Baadhi ya wanaoshindwa kwenda na mwendokasi wa Mageuzi Makubwa ya CCM ni wale ambao walizoea kuishi kwa mazoea, kula visivyo vyao, kudhulumu haki za wananchi hasa wanyonge, walizoea kujimilikisha mali za CCM na kuzifuja watakavyo, walizoea kuwa miungu watu na kuwadharau wanachama.

Katika historia ya Chama chetu watu hawa wamekuwapo katika awamu zote, na ni mapambano kuwaondoa, wanachama wanawajua, dhamira njema ya CCM Mpya inawajua, na hakika Uongozi wa CCM na Vikao vya Chama vitahakikisha watu hawa wenye inda hawapati Uongozi katika Chama chetu.

Watu waovu wana mitandao yao ya uovu, tuwakatae, na Chama chetu kimekuwa na desturi nzuri ya kuwakataa, kipindi hiki tutawakataa tena na kwa sauti kuu. Mitandao imedhoofisha sana Chama chetu, mitandao ya watu wabinafsi na wanaotaka kukitumia Chama chetu kama kitega uchumi, mitandao ya kidhalimu haina nafasi kwa Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Wakati mwingine hata watu ambao wamepata kuhudumu katika nyadhifa za Uongozi wanahusika kuhujumu Chama na nchi yetu, wanatengeneza mitandao na kushirikia na madhalimu, tunawajua, hata utu una kikomo, hatutawaruhusu kuvuruga Chama chetu.

Shime wanachama msikubali hata kidogo madhalimu wa kisiasa wakajaribu tena kuteka Chama chetu, walishindwa, wameshindwa na wataendelea kushindwa. Rai yangu hapa, watu wabaya huwa hawagombani, maslahi yao ya kidhalimu ni ya kudumu, wanaweza kuonekana hawako pamoja lakini wanaunganishwa na maslahi yao ya kudumu ya kidhalimu. Hata kwenye Chama chetu walikuwepo, wameondoka, wamebaki, kazi yetu ni kuwadhibiti ipasavyo, wameanza kuzungumza, tuwe macho kulinda misingi ya Chama chetu.

Kila mwana CCM asimame kidete, akisemee Chama, aisemee Serikali ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), ni wajibu wetu kuujuza umma wa wananchi nini Serikali inafanya na kwa nini.

Tunaupinga udhalimu katika Chama chetu na tunaupinga udhalimu katika Serikali, sio kazi rahisi lakini tutashinda kwasababu dhamira yetu ni njema na inasimamia maslahi mapana ya Taifa la Tanzania na watu wake.

Hata mabwana wakubwa wa dunia tumewaonesha kwa vitendo kwamba tunamaanisha tunaposema tumechoka kuonewa, tumechoka kuibiwa kwa makusudi au kwa kuhadaiwa. Nchi yetu ni ya kipekee sana na Mungu ametubariki na kila aina ya utajiri wa asili na watu wenye mshikamano.

Kijiografia nchi yetu iko katika eneo la kimkakati katika uso wa dunia. Katika bara la Afrika ni nchi mbili tu ndio zinatengeneza nyonga ya bara la Afrika nazo ni Tanzania na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo. Hizi ndizo nchi pekee ambazo zinalikata bara la Afrika katikati na nchi ambazo zina mipaka ya bahari kuu zinazozunguka bara la Afrika kwa maana ya Bahari ya Hindi upande wa Mashariki inayopakana na Tanzania na Bahari ya Atlantiki upande wa Magharibi inayopakana na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo.

Ukizungumzia nguvu za siasa za kidunia (geo-political forces) Majabali (Mataifa makubwa) ya kidunia na hasa yanayoongozwa na mrengo wa siasa za kiliberali na yenye uchumi uliononeshwa na matunda za udhalimu wa kibepari, utagundua wanatamani sana nchi hizi mbili zisitawalike.

Majabali haya yanatamani nchi hizi zisitawalike ili wapate nafasi ya kudhibiti eneo hili la kimkakati. Lakini zaidi ya yote ifahamike kwamba katika eneo hili ndiko hazina ya rasilimali madini ya dunia iliko, kwa uchache na kwa kutaja, hapa yako madini yenye thamani ambayo hata duniani hakuna, ndio maana hata Tanzanite ikapewa jina hilo. Ili Majabali wawe na uhuru wa kuchukua hapa watakacho lazima hapa pasiwe na mwenyewe, watapandikiza chuki kwa makundi, watajaribu kutuvuruga kwa tofauti za kiimani na watajaribu pia kupitia vyama vya siasa.

Majabali ya dunia yamefanikiwa kuiangusha Congo ama niseme yamefanikiwa kuifanya Congo isitawalike na wamepafanya pawe pahala ambapo wanaingia na kutoka na chochote bila kuulizwa maswali wala kulazimika kutoa majibu.

Mwenyekiti wa CCM Ndg. Magufuli na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania amebadilisha utamaduni mbaya na desturi zisizofaa. Amewakatia mirija madhalimu wakubwa na wadogo walioko ndani ya nchi na walioko nje ya nchi. Imewauma sana sana, na wale walioko ndani wanatafuta kila njia ya kumhujumu asifanikiwe, uzuri wanajulikana, ni wanaume wavaao baibui, baadhi yao ni watoto wa masikini na wamenufaika kwa fedha za masikini ila wamechagua maisha ya kufuru na ufedhuli, kwao vikao hukutania Dubai. Tunawajua.

Wako wachache katika Chama chetu cha Mapinduzi (CCM), wana CCM na vikao vyake tusaidieni kuwakataa, na pale wanapotumia hila kujipenyeza wafichueni. Hakuna Chama makini kama CCM, ndio Chama ambacho kwa imani yake kina amini katika Ujamaa na kujitegemea, ndio Chama pekee ambacho kinaamini binadamu wote ni sawa na ndio Chama pekee ambacho kwa imani kinaamini utu wa binadamu unastahili kuheshimiwa. Kule nje hakuna vyama, kuna vikundi maslahi, ni kama bidhaa sokoni, akifika mwenye bei anachukua bidhaa, na ninyi ushahidi mmeuona Mwaka 2015.

Nakomea hapa, wiki ijayo nitazungumza namna ambavyo ndoto ya kujenga uchumi imara na madhubuti ambayo Mwalimu Nyerere alikuwa nayo na hakuishi kuiona imeanza kudhihirika katika awamu ya Tano.

Ombi langu kwenu, hivi ni vita vya mwili na roho, ni vita ya haki dhidi ya udhalimu, vita ya mwili tunaimudu na tutaishinda hakika, tusaidieni Maombi maana vita ya roho yapaswa ipiganwe na wengi wema na waishio maisha ya kujikana nafsi na wenye hofu ya Mungu.

Makala hii imeandikwa na Humphrey Polepole, Katibu wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) mwenye dhamana ya Itikadi na Uenezi


4 comments:

  1. SIASA NI UCHUMI

    kidumu chama cha mapinduzi, kidumu chama tawala CCM

    ReplyDelete
  2. Katibu wetu Mungu akubariki sana! Huu ujumbe unagusa sana kwa Mtanzania yeyote mwenye Uzalendo wa kweli na mwenye kumcha Mungu! Nakutakia moyo huohuo, endelea hivyohivyo na kazi yako, usirudi nyuma na Mungu azidi kukulinda kila wakati, kila mahali na kila iitwapo leo. Amina.

    Tunasubiri kwa hamu hiyo makala ya pili juu ya ndoto aliyokuwa nayo mwl. Nyerere katika kujenga uchumi imara na madhubuti! Mungu Ibariki Tanzania, Mungu ibariki Afrika, Mungu akubariki!

    ReplyDelete
  3. FOR SURE NAJIVUNIA CHAMA CHA MAPINDUZI...HIKI NDO CHAMA SASA.

    ReplyDelete