Saturday, June 6, 2015

WATANGAZA NIA WAJIPIME KWANZA KWA HAYA MACHACHE: TUJIREKEBISHE

Kuonesha kila mtu anaweza kutangaza nia ya Urais kwa watu wazima ni kumkosea heshima aliyeko madarakani

Wiki ijayo nitaendelea kujadili hasa kwenye runinga, redioni na kwenye hadhara mbalimbali juu ya mchakato wa ndani ya Chama cha Mapinduzi wa kumpata mtu atakayepewa dhamana na chama ya kuwa mgombea katika uchaguzi mkuu wa mwezi Oktoba mwaka huu.

Ninaendelea kusisitiza kwamba, CCM inapasa kuonesha mfano kwa vyama vingine, CCM inatakiwa kutoka katika mchakato wake wa ndani kwa ushindi. Ninaposema ushindi ninamaanisha, mbele ya macho ya watu na kwa wingi wa wale ambao ninaonana nao. CCM haijajijengea taswira nzuri mbele ya watu na hasa vijana wadogo na kwa maneno mengine hii ni fursa adimu na adhimu ya kuuthibitishia umma wa watanzania kwamba imani yao kwa CCM haijawekwa rehani.

Lakini kabla sijaainisha mambo machache ambayo wana CCM wanatakiwa kujipima kwayo ninabudi ya kueleza pia kwamba, licha ya chama kutoa uhuru mpana kwa watu kutangana nia ya uombea Urais, lakini pia jambo hilo linaleta taswira yenye ukakasi kidogo. Inawezekana tuna wana CCM wengi wenye uwezo mkubwa wa hata kupewa utawala wa nchi lakini inabidi kujichunguza na kutafakari ndani ya chama je kuwa na wagombea karibia 20 ni sifa yenye tija au ni sifa za kijinga mbele ya macho ya watu?

Kila kona watu wanasema hata huyu, hata yule? Inaonekana kana kwamba ni mchezo wa gombania goli, maadamu unaweza kubutua mpira mbele basi karibu uwanjani, la hasha. Najua CCM inajua fika na kwa uzoefu kwamba Urais ndio taasisi kubwa kabisa katika Taifa letu. Taasisi ya Urais na kiongozi wake ambaye ni Rais mwenyewe, ni nafasi na wadhifa nyeti kabisa. Taasisi ya Urais na nafasi ya Urais si pahala pa kukimbilia kana kwamba ni mchezo wa “chandimu” au “gombania goli”.

Nimepata kusema hapo awali uongozi wa nchi na hasa uongozi wa juu kabisa wa nchi yetu ni kama cheo cha kiongozi wa dini, ni kama kuhani ni kama nabii, nafasi hiyo ni takatifu. Kwa wale wenye imani ni vema mkajua kwamba hata Mungu anapolitazama Taifa letu ili kulibariki na kutufungulia neema, huzipitisha Baraka na neema hizo kwa yule Kiongozi wetu mmoja ambaye ndiye taswira ya Umoja wetu, huyo ndiye Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Mkichagua mtu ambaye kwa sifa za kibinadamu na kwa muonekano wa haraka haraka wa kibinadamu ni mzuri, Taifa letu litakosa Baraka za Mungu kwa miaka mitano inayokuja.

Nafasi kama hii ya Urais kwa asili yake mtu hutafutwa, huombwa na hata kulazimishwa na wale ambao huwa wameonekana kutoka miongoni mwetu kuenea katika nafasi hiyo aghalabu hukubali kwa kuumia moyo kwasababu wanajua jukumu lilopo mbele yao ni gumu, zito na lenye changamoto nyingi.

Na hapa niwaase viongozi wa dini kwamba wao ndio mabalozi wa Mungu hapa duniani, wawe makini sana hasa kipindi hiki kwasababu iwapo watamwakilisha Mungu sehemu ambazo Mungu asingependa kuwakilishwa itakuwa ni kujichumia dhambi kubwa.

Unajua katika utendaji wa majukumu ya nchi balozi ndiye mwakilishi wa nchi na mwakilishi wa Rais, sasa nikupe mfano, mwaka 1977 tulikuwa na mgogoro na Nduli Idi Amini Kiongozi wa Uganda wakati huo, sasa kama ingetokea balozi wetu kila kukicha yuko kwa Idi Amini anakula na kunywa naye kama marafiki tena kwa utashi wake mwenyewe wala sio kwa maelekezo ya kimkakati kutoka makao makuu kwa maana ya hapa nyumbani. Je balozi kama huyu tungemtendea vipi? Katika kipindi kile cha vita, huyu angekuwa mhaini moja kwa moja na adhabu yake ni kifo. Sasa na ninyi viongozi wa dini ambao mnamwakilisha Mungu katika maeneo ambayo mnajua kabisa asingependa kuwepo, mjue, na ninawaambia leo kwamba mbele za Mungu adhabu zenu zitakuwa zile zimstahilizo anayemuasi Mungu, kibinadamu huwa tunaita mhaini. Kuweni macho!

Na niwaase pia wana CCM watakao kuwa na dhamana ya kupitisha mgombea wao kwamba, msianze kuhukumu watu kwa muonekano wao, msije nanyi mkahukumiwa, hatumpimi mtu kwa habari za kusikia, la hasha, maana najua wako katika watangaza nia ambao wamefanikiwa kuficha ubaya wao, lakini hawana tofauti na wale muwaonao wabaya sasa, watendeeni haki na Mungu atawaheshimu.

Baada ya kusema maneno ya utangulizi sasa naomba kwa sehemu nieleze baadhi ya matarajio ya Tanzania na watanzania kwa Rais wa Awamu ya Tano. Matarajio haya yamejikita katika namna ambavyo Rais wa awamu ya Tano ataweza kwa uwezo na ufanisi mkubwa kushughulika na masuala ambayo kwa muda mrefu sasa yametuvuruga kama Taifa na yametuacha katika sintofahamu juu ya mustakabali wetu kama Taifa sasa na baadaye.

Kusimamia Utawala Katiba na Sheria

Rais wa awamu ya Tano anapaswa kujua kwamba kwa muda mrefu tumekwenda kinyume na Katiba au kwa lugha kali tumekuwa tukivunja Katiba muda mrefu hata tukazoea tabia hiyo na kuifanya mazoea, tabia na utamaduni. Rais wa awamu ya Tano anapaswa kuwa mtu mwenye uhalali wa jamii “social legitimacy” na ambaye kwa uhalali huu atakuwa na mamlaka ya uadilifu yaani “moral authority” ya kuondoa kabisa mazoea, tabia na utamaduni wa kuvunja Katiba na kuenenda kinyume cha sheria za nchi.

CCM wakitupatia mtu ambaye hana uhalali wa jamii yaani “social legitimacy” na ambaye hana mamlaka ya uadilifu yaani “moral authority” kwa uwazi tumwonavyo sasa na kwa kificho tusivyomjua sasa, mtu huyo kamwe hatoweza kusimamia utawala wa Katiba na Sheria, mtu huyo ataendeleza mazoea yale yale yasiyofaa. Mtu huyo ataendelea kulinda maslahi ya wale wanufaikao na mazoea, tabia na utamaduni wa kuvunja sheria za nchi, mtu huyo hatakuwa Rais wa watanzania na vivyo hivyo watanzania wasitegemee miujiza kutoka kwake.

Suala la Muungano wetu

Matarajio ya watanzania kwa Rais wa awamu ya Tano ni pamoja na kushughulikia na kumaliza kabisa Changamoto za msingi zinazokabili Muungano wetu. Kila mtu anajua kwa tuna manung’uniko kutoka kila upande wa Muungano kwa maana ya Tanzania Bara na Tanzania Visiwani. Tunataka mtu ambaye ana uhalali, ana mamlaka na anaheshimika na viongozi wastaafu na walioko madarakani kwamba anaweza kuwaitisha na kuwaambia “watanzania wanatatizwa na Changamoto za Muungano wetu na kwa pamoja tunakwenda kuziondoa”. Awe mtu ambaye viongozi wa upinzani na viongozi wa CCM wakimtizama wanasema mtu huyu ninamheshimu na nina imani naye kwamba anaweza kufanya kazi hii.

Naomba niwaume sikio kidogo, tunataka mtu ambaye ataimarisha heshima na nidhamu ya madaraka ya Rais, leo hii wengi wa viongozi wetu hawaheshimiani, hawapendani, hawazungumzi na ukiongea na huyu anamlaumu yule, ukiongea na yule anajifanya kama halioni tatizo vile, na hawakai kwa ujumla wao wakazungumza na kuondoa tofauti zao. Hii inakwenda kwa viongozi wa wastaafu na walioko madarakani, kila mtu anamwonea kinyongo mwenzake. Tunamtaka mtu ambaye ana uhalali wa kuwaita wote na wakaitikia wito. Leo hii tuna nchi mbili na serikali mbili, hili ni baa maana hata ukisoma ibara ya kwanza ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano inasema tofauti.

Muungano umejeruhiwa zaidi miaka mitano iliyopita na hatujaweza kuponya majeraha yake hata kidogo isipokuwa kutoa dawa za kupunguza maumivu, dawa za kupunguza maumivu ndio kushughulika na zinazoitwa “kero za Muungano”. Sasa ufike wakati tumpate mtu ambaye tunaamini ataweza kutoa dawa ya kuponya na kumaliza ugonjwa kabisa ili Muungano wetu uwe na afya ya kudumu miaka 100 ijayo.

Ujenzi wa Amani, Umoja na utulivu (stability) wa kisiasa

Tunamtaka Rais ambaye anajua kwamba amani na Umoja wa Taifa letu msingi wake ni haki na usawa kwa watu na Wananchi wetu. Anapaswa kujua amani ni tokeo la ujenzi endelevu wa amani pamoja jitihada endelevu za kulileta Taifa kuwa kitu kimoja licha ya mtawanyiko mkubwa wa makabila na dini za watu na Wananchi wetu. Matarajio ya watanzania kwa Rais wa awamu ya Tano, ni kuona haki za watu na binadamu raia wa nchi yetu zinaheshimiwa, zinatolewa kwa wakati, zinalindwa na kuhifadhiwa.

Aidha Rais huyu ajaye anategemewa kutoa hamasa na kuwa mfano wa kulinda na kuzitoa haki hizi ili watu na raia wa Taifa letu waweze kunufaika na kufurahia matokeo kuheshimu haki za binadamu. Ili haki itolewe ni lazima usawa uzingatiwe kwa gharama yoyote ile. Haki bila usawa ni kazi bure, Amani bila usawa ni kazi bure kabisa. Rais ajaye anatakiwa kujua tumecheza cheza na haki za raia wetu na kwamba hatujafanya kazi nzuri ya kuzitoa haki hizi kwa usawa kwa watu wetu katika maeneo yote ya nchi na kati ya masikini na matajiri.

Ukicheza na haki za binadamu na watu, kisha ukaondoa usawa kwa kupendelea wachache, jua tunakaribia ukingoni, muda si mrefu, watu na raia wetu watakwenda kuchukua haki zao kwa mikono yao, kwa vigezo vya maeneo ya kijiografia, dini, masikini dhidi ya matajiri na kadharika. Tukifika huko, amani yetu tutakuwa tumeiweka rehani na Umoja wetu mashakani. Leo hii viashiria vyote kwa amani yetu inatetereka viko bayana, tunamtaka mtu ambaye akisimama tu imani zetu za nafsi juu ya Taifa letu zinaanza kukua mara moja, mtu huyo akisimama hata imani ya uchumi inaanza kuimarika na utashangaa kabla ya kuanza kutenda kiuchumi thamani ya shilingi ya Tanzania itaimarika.

Nafasi ya Vyombo vya Ulinzi na Usalama

Tendeni haki, shaurini viongozi wetu, msijiingize kwenye siasa na kamwe msishiriki kufanya uamuzi wa kisiasa, kazi yenu ni ushauri na ni ushauri tu. Kama mpo wenye tabia mbaya na isiyo na heshima ya kutisha viongozi wetu ninawaasa acheni mara moja. Rais wa nchi hupatikana kwa ridhaa ya Wananchi na si vinginevyo, katika utumishi uliotukuka wa vyombo vya ulinzi na usalama, mnajua ni dhambi na ni kinyume na weledi wenu kujaribu kutengeneza Rais kwa namna na hali yoyote ile.

Najua dhamira njema hutenda haki, na ninyi mmeapa hata kwa kufa ili nchi hii iishi, msiruhusu wachache na wabaya na wenye dhamira mbaya miongoni mwenu kuvuruga zoezi takatifu la kupata Kiongozi wa nchi hii. Wale ambao mtasimamia maadili ya kazi yenu, histoa itasimama kueleza utumishi wenu uliotukuka na wale ambao tama imewazonga, ni suala la muda tu na aibu kuu itawazonga na hatutawadhihaki bali tutahuzunika kwamba tulifanya uamuzi mbaya kuwa nanyi katika vyombo vyetu vya ulinzi na usalama.

Maswali kwa watangaza nia wiki hii


Walikuwa wapi kusimamia waziwazi maslahi ya Wananchi katika mchakato wa Katiba?

No comments:

Post a Comment