Sunday, June 14, 2015

HALI HALISI YA NCHI NA RAIS TUNAYE MTAKA: TANZANIA NJIAPANDA, TAIFA LIFANYE NINI?



Kinyang’anyiro cha Urais-Tanzania iko njia panda

Wengi mtakubaliana name kwamba kinyang’anyiro cha kumtafuta mgombea urais kupitia Chama cha Mapinduzi kimekwenda kwenye kiwango kingine kabi
sa, na hasa ukizingatia mpaka sasa huenda kuna makada zaidi ya 30 ambao wameonesha nia ya kuomba ridhaa ya chama.

Wengi wamekuwa na maswali ya kiuchokozi hapa na pale kwamba unadhani wimbi hili kubwa la wagombea tafsiri yake ni nini? Nimejitahidi mara zote kusema kuna tafsiri zaidi ya moja, mosi ni uhalisia kwamba wana CCM wako huru kuweka mawazo yao hadharani, pili, demokrasia iko pana katika chama kwamba yeyote ambaye anaona anaenea katika nafasi basi anayo fursa ya kujitokeza na kutangaza nia na hatimaye kuomba kukubalika na chama.

Tatu, ni kwamba huenda watu hawajui maana hali ya tafsiri ya urais kama taasisi na Rais kama kiongozi Mkuu wa nchi na majukumu yake, huenda watu wanauona urais kwa maana ya kusafiri kila pahala, kufungua miradi, kutoa hotuba, kutoa maelekezo, kupita kwenye msafara wakati wengine tunasubiri foleni, kutuma watu wakafanye kazi kana kwamba watu hawajui wanalopaswa kutenda.

Wengine wanadhani pia ukiwa Rais kazi ya kuwashughulikia wauza dawa za kulevya, kushughulikia wala rushwa na ufisadi ndio hasa itakuwa kazi yao, hawa nawaona wakitembea na pingu, bakora za mibungo na magereza yanayotembea ili kila watakaye mbaini basi watamfunga papo hapo, wapo watangaza nia ambao nikienda kwenye vichwa vya kwa kutafakari nawaona wakiwaza hivi.

Nne, ni kwamba huenda kuna watu wahuni pia, watu wasio na mapenzi mema na taifa hili, watu ambao wamegeuza nafasi ya urais bidhaa ya mnadani. Hawa wako pale kuhakikisha wanakuwa Rais, haijalishi sote tunajua Urais mtu hupewa kama dhamana na wananchi, lakini wapo ambao tayari wameshajiona marais, hii ni kuwakosea wapiga kura, na zaidi kukikosea heshima Chama cha Mapinduzi. Hawa watu wa namna hii wao hawajali demokrasia kwa maana ya utawala wa watu kwa watu na watu wenyewe yaani kiingereza “democracy”, watu hawa ni genge la wajanja wachache ambao wanataka kushika madaraka ya nchi, maslahi yao ya msingi ni wao wenyewe kiingereza mtindo huu tunaita “mobocracy”.

Kisiasa- Tanzania iko Njiapanda

Wengi wanahoji dira ya Taifa hili ni ipi? Taifa halina dira, ninaposema hivi wengi mtasema kwamba mbona tunayo ile inaitwa “vision 2025”, ni kweli lakini ile ni dira ya Tanzania Bara pekee, na Tanzania Bara si Taifa, utaniambia pia “vision 2020” nakubali lakini hiyo inahusu Zanzibar pekee, sasa na mimi nitakuuliza je iko vision moja ambayo inazungumzia Taifa la Tanzania?

Kwanza nikitizama vision 2020 na 2025 utagundua bado hazina sifa ya kuwa Dira. Dira ni waraka ambao, Taifa kwa mwafaka limesema huko ndiko tunakotaka kwenda. Ukisoma vizuri hizi nyaraka mbili kila moja iko huru, nikimaanisha Ukisoma vision 2025 inazungumza kana kwamba Tanzania Bara ndio Jamhuri na Muungano na vivyo hivyo ukisoma vision 2020 unaona Zanzibar inajizungumza yenyewe kana kwamba ni huru. Kwangu mimi kitendo cha nchi moja kuwa na dira mbili na zisizosomana ni sawasawa kabisa na kuwa na ndege moja yenye marubani wawili wasio na uelewa wa pamoja wa wanakwenda wapi. Juzi juzi hapa kule nchini Ujerumani kitendo cha kuwa na marubani wawili wasio na uelewa wa pamoja ndege inapaswa kwenda wapi kilipelekea ajali mbaya kabisa, rubani mmoja anajua tunatakiwa kuwafikisha salama abiria wakati rubani mwingine ana mipango ya kutoa uhai wa abiria na yeye mwenyewe kwa kuigongesha kwa makusudi ndege kwenye milima.

Mzee Warioba alijaribu kututengenezea dira katika Rasimu ya Katiba Toleo la Pili, lakini Katiba Inayopendekezwa ikasema hata serikali isipofanya chochote katika utekelezaji wake isihojiwe kokote hata mahakamani na mtu yeyote asiwe na mamlaka ya kuhoji juu ya utekelezwaji wa dira hiyo, sasa hapo ni dira au kiini macho?

Taasisi za Mamlaka ya nchi hasa Bunge ni dhaifu, unakumbuka wakati wa Bunge Maalum wengi ya wabunge walitaka mikataba isipelekwe Bungeni, baada ya Bunge maalum wakazinduka wakataka mikataba ya TPDC, wakanyimwa, roho ikawauma sana hata wakatenda kinyume na mamlaka yao na kuelekeza Polisi iwakamate viongozi wa shirika la mafuta, walitenda kwa hasira, kiko wapi leo? Kitendo kile kikawafanya watake mikataba ipitie bungeni kupata ukubalifu, hawa ni wale wale ambao wengi wao walifuta masharti ya rasimu ya Warioba yaliyosema mikataba ya madini iridhiwe na bunge.

Wakati Bunge likiwa na mtanziko wa kimamlaka, hali iko dhahiri shahiri kwamba kuna upungufu wa utamaduni wa kidemokrasia (democratic culture), tumeacha kuwa watu wa majadiliano (dialogue), hatujengi hoja bali tunapiga makelele na kushutumiana wakati wote, Mwalimu Nyerere alipata kusema “argue, don’t shout”. Hatujengi muafaka, hatufanyi maridhiano, hatuna uelewa wa pamoja katika masuala ya msingi, hatuna uhimilivu (tolerance) lakini inaonekana tuna uhimilivu kwa mambo kama rushwa, ufisadi, mauaji ya albino na vikongwe n.k.

Tumeanza kushuhudia roho mbaya ya utengano (negative devisive force), ukabila, ukanda, udini, ubara na uzanzibari n.k. Umeshuhudia hata watangaza nia tayari wameanza kujipanga kikanda hii ni hatari kwa ustawi wa umoja wa kitaifa. Inaanza kuonekana Uongozi si dhamana tena bali mali ya watu fulani. Utumishi wa umma unafanya kazi kwa woga. Maadili ya Taifa, binafsi na ya viongozi ni tatizo kubwa, hata pale sekretarieti ya Maadili ya viongozi inapowafuatilia wale wanaokiuka miiko ya uongozi utagundua nguvu zake zina ukomo mkubwa.

Kuongezeka kwa vitendo vya Rushwa, ufisadi na mmomonyoko wa maadili, angalia namna ambavyo watangaza nia wanatumia fedha nyingi, swali la kujiuliza ni fedha zao binafsi? Na kama si zao waliowapa wana maslahi gani na nafasi ambayo watangaza nia hawa wanaitafuta? Muungano wetu bado una changamoto nyingi, Serikali 2 hazieleweki, sio tu kwenye Katiba ya 1977 bali hata kwenye Katiba Inayopendekezwa. Watu wa Tanzania Bara wanauona Muungano kama mzigo na watu wa Tanzania Zanzibar wanauona Muungano kama Kero. Kuvurugwa kwa mchakato wa kupata Katiba Mpya ni huzuni nyingine inayoongeza njia panda ya kisiasa

Kiuchumi- Tanzania Njiapanda

Umma wa watanzania hauna mali za pamoja, tulibinafsisha kila kitu na mashirika ya umma yaliyosalia ni hohehahe, mfano ni shirika la ndege la Taifa “Air Tanzania”, shirika la reli (TRL) ni shida nyingine kubwa licha ya kwamba tuna ubia na watu wengine. Tuna shirika la nyumba (NHC), hili linakimbia kwa kasi baada ya maboresho makubwa ya kiutendaji, lakini nawapa indhari kwamba uchumi wa Marekani ulianguka kwa uwekezaji usiotabirika katika makazi na nyumba, tuwe macho.

Sekta binafsi ni dhaifu, sekta binafsi imeingia katika huduma na si uzalishaji, tizama kampuni ambazo zinaonekana vinara ni makampuni ya simu. Haya hayazalishi, haya yanatoa huduma na yanachukua pesa za watanzania masikini zaidi kuliko hata faida ambayo tunanufaika nayo moja kwa moja kama wananchi masikini na wasio na ajira.

Angalia ongezeko kubwa la mabenki, unadhani wanufaikaji ni wakulima na wafanyabiashara ndogondogo ambao kwa kiasi kikubwa wanaangukia katika sifa za watu wasio kopesheka, Tuamke, benki ni nzuri lakini lazima tuwe na uchumi ambao unabeba watu wake.

Hakuna viwanda vya kutosha vya uzalishaji kunakopelekea tatizo la ajira na kupoteza fedha za kigeni (hakuna exports za kutosha), mchele wa mbeya na kwingineko tunao lakini tunaagiza, sukari ya kutoka Mtibwa, Kilombero na Kagera tunayo lakini tunaagiza, tunayo gesi lakini bado tunaagiza mafuta mazito. Halafu dola ya kimarekani ikifika zaidi ya shilingi 2000 tukiuliza tunaambiwa huko duniani dola imeimarika zaidi, kweli?

Sekta binafsi iliyo dhaifu haiwezi kusimamia demokrasia na kuhakikisha kwamba amani inaendelea kuwepo. Na hapa niwaseme kidogo Taasisi ya Sekta Binafsi (TPSF) kwamba wameona Bunge Maalum lilivyoendeshwa na namna ambavyo Katiba Inayopendekezwa imedhoofisha maadili ya viongozi na kuvuruga Dira ya Taifa kwa kuiwekea vikwazo, lakini kwani umesikia wakikemea au wakishauri kitaalamu madhara ya kubomoa misingi ya maadili na uwajibikaji katika Katiba? Nawapa changamoto, na wao wajitafakari.

Mkazo haujawekwa katika uchumi wa kujitegemea unaozingatia ukuaji wa kilimo kinachotoa malighafi kwa ajili ya viwanda ambavyo vinachakata malighafi kuwa bidhaa zilizochakatwa au bidhaa kamili ambazo ziko tayari kurudi na kutumika katia sekta nyinginezo ikiwemo kilimo

Kukosekana kwa uchumi imara unaojitegemea kunazalisha watu masikini wengi zaidi katika Taifa letu. Tuna walipakodi wachache na tuna walaji wengi katika Taifa lakini pia mianya ya wanaokula zaidi yaw engine kinyume cha sheria ni wengi zaidi na kusababisha chakula wanachokusanya wachache wetu ama kinaliwa na wachache wetu kinyume na sheria na matokeo yake hakitoshelezi mahitaji yetu kama Taifa. Tunalo pia Tatizo la kuwa na vyanzo mbadala mbali na hivi vya sasa vya mapato ya Taifa na Serikali, na bado tunalo tatizo la Makampuni ya madini kutokutoa kodi ya mapato kutoka faida zao.

Wengi wanasema wanatoa kodi lakini ni kodi wanazokatwa wafanyakazi wao na sio kodi inayokatwa kutokana na shughuli za ushalishaji wa makampuni. Kwenye gesi ni eneo linguine ambalo ukiachia kwamba limegubikwa na sintofahamu juu ya namna mikataba yake imefungwa hasa katika ngazi ya utafutwaji wa gesi ni kizungumkuti kingine kinachotuweka kwenye njiapanda kama Taifa.

Rais tunayemtaka Awamu ya Tano

Tunataka Rais ambaye anajua tuko njia panda, ana ana uwezo na mamlaka ya kukemea kwasababu na yeye ni mwadilifu “moral authority”. Tunataka kiongozi ambaye anakubalika na jamii na jamii inamwona kama sehemu ya majibu ya changamoto zao. Hatutaki watu wajitembeze kwetu, tunajua tunataka Rais ambaye atasimamia masilahi yetu.


Leo karibu kila mtia nia, nasikia huyu kapata pesa kule, huyu kapata pale, huyu hela za wizi, huyu kapokea hela chafu, huyu kachukua za watu wabaya na kadharika. Watanzania tuache ushabiki, tusimame na tuwe wamoja katika hili. Rais wetu akiletwa na watu maana yake si wetu ni wao. Tafakari

3 comments:

  1. Kijana upo vinzuri, naomba nipate namba yako ili ukipata mda tukuombe kundi letu la CHADEMA vs CCM lijifunze jambo toka kwako

    ReplyDelete
  2. 0786146700 Karibu

    ReplyDelete