Sunday, July 26, 2015

TUJIKUMBUSHE: KATIBA BORA AFRIKA NI ILE ITOKANAYO NA MAONI YA WANANCHI




Nianze kwa kuzurula

Unajua furaha ya ujana ni kuweza kufanya makosa, kueleweka, kusamehewa, na kupuuzwa kwa kigezo kwamba ni ujana unasumbua au unajua damu bado inachemka na sababu kadhaa wa kadhaa zinazofanana nazo. Sidhani kama vijana wenzangu wameling’amua hili, kwamba ni wakati wa ujana mtu huruhusiwa kwa kiasi fulani kukosea kama sehemu ya kujifunza. Ni kipindi hiki kijana anaweza akasema mambo mazito na yakachukuliwa kawaida kwa kile kile kigezo kwamba ujana huo, akikua ataacha. Namshukuru Mungu kwamba nimo kwenye rika la kujifunza na hasa na niseme kwa kiingereza “interest” yangu imekuwa kujifunza kuhusu nchi yetu, ikoje, inaongozwaje, changamoto zake, magumu ambayo viongozi wetu au kama wanavyojulikana wakubwa, wanayokabiliana nayo siku hadi siku katika uongozi na utumishi.

Nimeanza hivyo makusudi kwasababu naanza kuona kama katika Makala hii nitaongea mambo ambayo niombe samahani mapema na nitashukuru kama nitachukuliwa kama ni ujana tu unanisumbua na ni damu inachemka. Siku moja Mama Mwatum Jasmine Malale Mjumbe wa Tume ya Katiba aliniambia kitu ambacho mpaka leo huwa nikipata wasaa nawasimulia na vijana wenzangu. Alisema kuna tofauti kati ya kuwa na akili au uwezo wa kufanya mambo labda kwa haraka, kwa ustadi na kwa umahiri upande mmoja na kuwa na hekma au hekima, uwezo wa kuyatizama masuala kwa undani, kwa pande zote na hasa hasa ukizingatia uzoefu unaojengwa na wakati. Akaniambia unaweza kuwa na akili na ukakosa faida ya uzoefu unaokuja kwa wingi wa wakati. Mtu mwenye akili ni mwepesi kuhadaika lakini mtu asiye na werevu wa akili ya darasani au hii akili ya kileo ya kukurupuka ni vigumu sana na nikitumia lugha ya vijana “kuuingia mkenge” kwasababu ameshaona “mikenge mingi” katika maisha yake na hivyo kuikwepa si bahati ni hekma (hapa msisitizo ni wangu).

Sasa nauanza ujana, juzi juzi hapa nalipata kusikia kwamba Katiba Inayopendekezwa ni bora kuliko Katiba zote Afrika, nikasema hilo nalo neno na sikupenda linipite pasina kusema neno. Unaposema Katiba Bora unamaanisha nini? Na je umepima kwa vigezo vipi? Au tunarudi kule kule kwenye simulizi pasina ushahidi? Najua baadhi yetu sisi vijana wa leo tungepata fursa ya kupata kile kifaa cha kurudisha wakati nyuma labda miaka 30, huenda tungewapuuza wananchi katika mambo mengi sana. Kwa namna ambavyo naona baadhi yetu kipindi hicho tungeamua mambo sisi wenyewe, watu tungesema hawa wanapaswa kutengenezewa vitu na kupelekewa na wala hawana haja ya kuulizwa maana tungeamini kabisa wao (wananchi) ni wa kutawaliwa tu.

Yaani nawaona baadhi yetu tukitembea huku na huko tukijua sisi ndio tujuao kuliko wananchi na kwamba hata inapokuja masuala makubwa yawahusuyo wao wananchi basi, tutaambiana kama wakati mwingine ni lazima watu watuelewe, uongozi sio jambo dogo. Naona kama tumekaa kwenye viti katika mduara mdogo kwenye bustani nzuri na tunafurahi kwa vinywaji na tukipata mchapalo taratiibu na tukisema unajua kamaradi, uongozi hapa sio kama kilimo cha nyanya, uongozi sio kama ufundi gereji, uongozi ni kazi, na michapalo hiyo inakuwa ndio wigo wa kutuweka mbali na watu wetu. Hapo ni Miaka ya 80 tukiwa tumerudisha wakati kwa kutumia kile kifaa maalum “time machine”.

Lakini muda unafika na tunarudi tena katika ulimwengu wa leo, ulimwengu wa dijitali, karibu kila mtu anajua kitokeacho duniani katika viganja vya mikono yake. Ulimwengu ambao tofauti na ule wa miaka ya 80, siku hizi ukisema uongo watu wanabaki na sauti yako au video yako ukisema uongo, ukiwa holela hata mambo ya kusitiriwa yanawekwa bayana Astakafilulah ni sheedah! Naona ulimwengu wa leo watu hasa vijana hawapokei tu eti tu kwasababu amesema mkubwa, hapa, wanapenda kuhoji kwanza, wanapenda waelezwe misingi kabla ya kuunga mkono hoja, na kadhalika.

Katiba Bora ikoje?

Katiba huwa ndio sheria mama, huwa ndio msingi mkuu wa sheria katika nchi au taasisi. Katiba kwa kawaida na kidesturi hutungwa na wenye kuitumia, bado haijawa mifano mizuri kwa baadhi ya katiba kutungwa na watu wachache na zikawa nzuri na kutumiwa na watu wengi kwa muda mrefu. Katiba Bora siku hizi ni ile ambayo imeandikwa kwa kuzingatia uwakilishi mpana, na tukumbuke dhana ya uwakilishi mpana si nyepesi, na tunaposema uwakilishi mpana tunakwenda mbali zaidi kusema ni kwa kiasi gani kila mtu anayeshiriki, mchango wake unaheshimiwa na sio ule mchezo wa hadaa wa wengi wape wachache wasikilizwe, la hasha.

Ushiriki huanzia kwenye sheria inayo ongoza mchakato, kisha katika ushiriki wa watu, wanapotoa maoni na hapa nyumbani walipokaa kwenye mabaraza na hatimaye walipokaa kwenye Bunge Maalum. Hivi nikuulize baba, na naomba unijibu kweli na kweli tupu ile ya kutoka ndani ya moyo wako, hivi wananchi tuliwaacha huru wakati wa kutoa maoni?

Hebu ngoja nikusimulie kitu kidogo, si unajua karibu kila mtu ana kadi ya chama chake? Sasa kipindi kile kule Tume wako waliokuwa wanajulikana itikadi zao na vyama vyao na wapo wale waliokuwa wana vyama lakini kwa asili ya kazi zao, utambulisho wa vyama vyao ulibaki uhusiano wa ndani kati yao na vyama vyao. Mimi ni mmoja wapo, sasa kuna mzee wangu mmoja, alijaribu sana kunipa kadi ya chama chake, masikini hakujua na mimi ni mwanachama tayari wa chama kingine, nikamkwepa kwepa sana. Lakini leo nikiri kwa mara ya kwanza nilishikwa na uchungu mkubwa sana baada ya kuona namna vyama vilivyokuwa vikilazimisha wananchi kutotoa maoni yao na wakati mwingine wakiwatisha kabisa watoa maoni wale. Nakumbuka nilichukia vyama vya siasa, mpaka ndani ya moyo wangu, nikajiambia inakuwaje vyama kuwa magenge ya maharamia wawatishao watu ili wasiseme Tanzania yao wangependa iweje.

Kuna wakati na ujana wangu ilipasa niwe mkali kila nilipo ona vitisho vinaongezeka, kuna siku ilikuwa katika Baraza la Katiba la Wilaya mojawapo kusini mwa Tanzania, na mtoa maoni alikuwa Mkuu wa Wilaya Mstaafu, huyu alisema wazi kwamba yeye amekataa kupokea maelekezo na atatumia fursa ile kusema yake. Wakati akiongea wengine walijaribu kumzonga zonga, nimeumia sana kwa matukio yale na nimeendelea kuumia. Sasa “baba” unasema kwa mazingira yale ya Bunge Maalum na namna ambavyo vyama viliuteka mchakato bila simile, je hii ni Katiba ya Wananchi na Bora Afrika au ni yale yale ya safari yangu iliyonipeleka miaka ya 80 kipindi mimi na wenzangu tukiwapuuza wananchi. Tena nikumbushe kipindi kile niko miaka ya 80 tulikuwa tukiambiana kabisa wananchi wanapaswa kupigwa propaganda na watakaa sawa. Nauliza, hizo ndio zama za leo?

Kauli ya Mheshimiwa Rais

Mhe. Rais wakati alipokabidhiwa Katiba Inayopendekezwa alisema wakati mwingine mambo mazuri yapasa yasubiri wakati upite, haya, tujadili, unakumbuka msingi wa kwanini alisema yasubiri wakati upite? Alisema baadhi yetu tuna hofu, anhaa, sasa nauliza hivi dawa ya hofu ipo au itakuja kulingana na muda unavyokwenda?

Je Hofu ya Mapendekezo makubwa ya Tume ya Jaji Warioba, ni ya kusubiri miaka 10, 20, 30 ijayo au ni suala la kueleweshana kwa taarifa na maarifa sahihi? Najiuliza. Maana siku hizi kila mtu ameshika lake tu, ooo Rais amesema tusubiri, narudia kusema tuache kumtafsiri Rais ili kukidhi matakwa yetu.

Nimalizie kwa kusema “ee baba” Katiba Inayopendekezwa sio bora hata kidogo na kimsingi inatugawa watanzania, inalinda maslahi ya wachache na imetupilia mbali maoni ambayo wananchi walitaka yawemo.

Rai kwa wagombea Urais na Ubunge

Nendeni mkawaambie wananchi kwamba mtajitahidi kushughulikia suala la Katiba ili tuwe na uelewa wa pamoja, tujenge muafaka wa kitaifa na tufanye maridhiano inapobidi, huo ndio uongozi. Hatuwezi kamwe kuwa na kura ya maoni tukiwa tumegawika kiitikadi na kimsimamo kama vyama vya siasa, mgawanyiko huu utashuka kwa wananchi na hii sio afya kwa Taifa letu.

Sunday, July 19, 2015

UKAWA, NI AMA MPITE KATIKA TANURU NA KUTOKA KAMA DHAHABU SAFI AMA OMBENI RADHI WATANZANIA



Siasa safi na si siasa ya uadui

Kila siku huwa ninapozungumzia ujenzi wa demokrasia katika nchi yetu, baadhi ya watu huwa hawanielewi ninaposema kwamba CCM imara ni lazima iambatane na upinzani makini. Na kwamba kwa mazingira yalivyo sasa pasina kuwa na upinzani makini CCM itayumba, na kuyumba huku sio lazima kuiangushe CCM leo, lakini sote tunakubali kwamba kuwa katika safari ambamo gari linayumba yumba huwa si dalili njema. Nadhani wengine wanaendelea kutonielewa, mantiki ya uwepo wa vyama vya siasa katika ulimwengu wa leo ni kuibua hoja, kujenga hoja, kuleta mawazo ya kustawisha maisha ya watu na raia wa Taifa letu.

Kama chama kimojawapo kipo madarakani na kinatekeleza mawazo yake ya kustawisha maisha ya Wananchi, kazi ya vyama ambavyo haviko madarakani ni kuibua hoja na kujenga hoja ya namna mawazo hayo ama yanafanikiwa au la na kuhakikisha chochote kinachofanyika kweli kina mguso chanya kwa Wananchi. Aidha vyama vile ambavyo havipo madarakani vina kazi kubwa pia ya ama kuboresha mawazo ya chama kilichopo madarakani au wanaweza kuja na mawazo mbadala kabisa, ilhali lengo likiendelea kuwa kustawisha maisha ya watu na raia wa Taifa letu.

Sijui niseme hivi karibuni au tangu kitambo, kumejengeka dhana mbaya kwamba mkiwa katika vyama tofauti basi ninyi ni mahasimu, ninyi ni maadui na wengine huenda mbali na kujinasib wao ni wa utawala wa nuru na wengine ni wa utawala wa giza. Mimi nakubali kabisa vyama kama Taasisi ni watu na watu hukosea na tukubaliane kwamba watu wanapokosea wanapaswa kuwajibika kwa mujibu wa taratibu  tulizojiwekea, Katiba na sheria zetu ikiwa ni mojawapo. Kwahiyo watu wakikosea, wawajibishwe, hata kama watu hao wanatoka chama chako, na si ustaarabu iwapo unashabikia watu kuwajibika kutoka vyama vingine wakati katika chama chako kuna matatizo.

Unapokuwa sio msafi unapoteza mamlaka ya kimaadili “moral authority” ya kukemea wengine wasio wasafi. Hata katika vitabu vya dini imeandikwa “ufalme mmoja hauwezi kuinuka juu ya ufalme uleule bali ufalme mwingine”, tafsiri yangu ya ufalme hapa yaweza kuwa watu wasio wasafi hawawezi kamwe kuwawajibisha watu wachafu na halkadharika watu safi hawana sababu ya kuwawajibisha watu walio safi, hiyo ni asili. Tunataka watu wasafi zaidi kama mtu mmoja mmoja katika mifumo yetu na mamlaka zetu za nchi ili watu hawa wasafi sio tu waende kuhakikisha mifumo na Taasisi zetu zinafanya kazi kwa uadilifu ili kutoa haki na hukumu kwa kila anayestahili bali wakajenge pia utamaduni wa watu wasafi tu kushika mamlaka. Imeandikwa katika vitabu vya dini watu wenye haki wakishika mamlaka Wananchi hufurahi na kunufaika.

Katika mazingira ya leo na nikizungumzia namna ya kuenenda katika siasa safi na uongozi bora, ni dhambi kwa mtu wa CCM kufanya hila ila kudhoofisha vyama vyenye mawazo mbadala na vivyo hivyo ni dhambi kubwa kwa vyama vyenye mawazo mbadala kutumia hila kuhujumu utekelezaji wa mawazo ya yule aliye madarakani.

Fitina na hujuma haziwezi kutujengea misingi ya demokrasia ambapo washiriki wa demokrasia wakiwemo wanasiasa na wengi wengineo, wanaheshimia, wanapendana wana aminiana na wana uelewa mmoja kuhusu nini watanzania wanataka kama nchi na Taifa. Hivi karibuni tumeona mtindo kwa kila chama kuwa na vikundi vyake vya usalama, hili si jambo la kufurahia hata kidogo, hii si dalili njema kwa ustawi wa demokrasia katika Taifa letu. Ukiona baadhi ya vyama vinapoteza imani na polisi wakati vyama vingine vinaonekana kuwa na amani na polisi, ujue kuna tatizo hapo, kama viongozi tunapaswa kujadili hilo na kulipatia ufumbuzi ili lisikue kuwa sehemu ya uvunjifu wa amani.

Mchakato wa Ukawa na sintofahamu

Nimefuatilia kwa karibu sana mchakato wa UKAWA kupata mgombea Urais pamoja na namna watajiratibu kwa nafasi za ubunge, udiwani na baada ya uchaguzi. Nikiri kwamba njia waliyoichagua UKAWA si rahisi hata kidogo, ni njia ngumu, ina Changamoto nyingi na ina makwazo mengi. Pasina hekima za hali ya juu, busara ya tofauti, pasina kuwatia moyo na kuwapa maneno ya kuwajenga ili wajiamini kwamba njia wanayoipitia ni sehemu muhimu ya “kuzaliwa upya” kidemokrasia, itakuwa vigumu kwao na kwa akili za kibinadamu kufanikiwa.

Nimeongea na mzee wangu na rafiki yangu Profesa Baregu kwamba katika hali waliyonayo akumbuke hali ngumu ilivyokuwa katika Tume ya Mabadiliko ya Katiba (TMK). Kuna wakati lazima ukubali kupoteza ili kupata, na nilazima wadau wa UKAWA wakafahamu kwamba kupata haimaanishi kupata kila kitu. Lakini moyo wa upole na uelewa unahusika sana, mkumbuke kuna baadhi ya vyama kwa fanikio lolote la UKAWA katika hatua hii ya awali inaweza kuonekana kama jaribio la kujitoa mhanga ambalo mara nyingi matokeo yake huwa kifo. Hivyo wale wakubwa wawafikirie wadogo, sio tu kwa nafasi zinazohesabika kwa idadi ya wabunge na madiwani bali katika kujitoa kwao na kukubali kwao kuwa sifuri kwa wakati ili nyote muweze kuwa nambari inayohesabika na yenye maana “significant”.

Katika mchakato wa UKAWA sasa ni lazima mjue mkubwa anapaswa kumhakikishia mdogo kuwa kinachoendelea ni mapenzi ya dhati na mdogo alione hilo. Na kama miongoni mwa UKAWA kuna wanaolingana kimo kwa sehemu ni vema wakaa pembeni ili wengine wakasaidia kutoa uongozi, kwa kufanya hivyo imani itaongezeka. Mlipofika ni imani tu itawavusha, kazi ni kuondoa kila alama ya kuteteresha imani. Muungano huu una wakubwa na wadogo na wadogo sana, alama moja ya kujenga imani ni kuhakikisha wakubwa hawahodhi madaraka makubwa kabisa. Unajua kwanini Tume ya Katiba ilipendekeza Serikali 3 ni kwasababu ilibidi na mdogo aonekane, na mkubwa akubali hilo na kuwekwa kwenye nafasi sawa na mdogo, ni imani tu hata kama mkubwa ataendelea kuwa mkubwa na mdogo vivyo hivyo.

Kubwa kabisa, mkishindwa kuafikiana na kutoka kama washindi, mtakuwa mmewakwaza watanzania, mtakuwa mmerudisha nyuma zoezi adhimu la ujenzi endelevu wa demokrasia yetu. Mimi nitapata wakati mgumu kuwaelewa, mlishindwaje kujikana nafsi zenu ili UKAWA ndio utamalaki?

Hivi mnajua kwamba kama mngechukua msimamo mkubwa kabisa ambao nao usingekuwa na shida, ni mgumu lakini ungetuzalia taswira mpya ya demokrasia katika Taifa letu. Msimamo mkali kabisa “extreme position” ingekuwa vyama kukubali kufa na kubaki na kimoja lakini roho zote za vyama zikahamishwa katika kile chama kimoja, kisha lengo likawa kuutafuta ushindi na hatimaye kushika dola. Utaratibu wa nani atapata nini huo ni wa badaaye, kwa kiingereza ningesema “the details will be sorted later”. UKAWA bado kwa utaratibu wenu mnaweza kulifanikisha hili kuelekea uchaguzi mkuu.

Haya ni mapito, mkiwa pamoja na mkiondoa ubinafsi mtapita na ushindi utakuwa kwa watanzania, mkishindwa mtakuwa mmeimarisha zoezi la kuidhoofisha CCM na mtapoteza imani ya Wananchi. Na pindi Wananchi wakipoteza imani na upinzani, wanachama wabaya wa CCM wale ambao wanaamini CCM imara ni kubomoka kwa upinzani watashika hatamu, na hao kamwe hawanii kwa dhati kubadilisha maisha ya watanzania. Wana CCM wazuri wanapenda upinzani usio dhaifu na hawafanyi siasa za chuki na fitina ili kupata ushindi.

Ujumbe mdogo kwa Dkt. Magufuli

Hongera sana kwa ushindi ndani ya CCM uliokupa dhamana ya kupeperusha bendera ya CCM katika uchaguzi mkuu. Nimesema hapo awali, rai yangu kwako, ukawe ile nguvu ya kutuunganisha katika chama. Ukumbuke kuna mawazo ya Wananchi na baadhi ya wana CCM hayakubaliki CCM, lakini mawazo hayo yanakubalika hata na Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA), maadamu unatafuta kura, zingatia mawazo yao.

Nimekusikia pia ukijibu hoja ya mchakato wa CCM na nafasi yako, nimekuelewa sana, Bob Marley aliwahi kuimba wimbo akisema tujikwamue kutoka utumwa wa kifikra “emancipate yourself from mental slavery...”, mimi nakuombea kwa Mungu utusaidie katika CCM kujikwamua kutoka siasa zisizofaa, kuondoa kiburi, kuondoa maslahi binafsi yayozidi sana maslahi ya umma wa watanzania. Wengi wameanza kusema oo sijui ushindi wako ni wa maridhiano, vijana wanasema wapotezee, waoneshe kwamba wewe ni wa tofauti, kwa mtindo huo nakuona ukiendelea kuandika historia yako katika ukuta wa dhahabu.

*Mwandishi ni Mwanachama wa Chama cha Mapinduzi anayeamini katika misingi ya kuanzishwa kwa chama cha Mapinduzi na Ahadi za Mwanachama wa CCM.

Saturday, July 11, 2015

NILIYASEMA HAYA KWAMBA TUWE WAANGALIFU NA SASA YAMETIMIA. CCM HATUPASWI KUSHEREHEKEA USHINDI BADO KUNA KAZI KUBWA


WATANZANIA CHUNGENI NCHI YENU, HIYO NDIO MALI YENU NA URITHI WA WATOTO WENU


KUJIANDIKISHA NA KUSHIRIKI KATIKA UCHAGUZI MKUU NI HATUA YA KWANZA SASA

Nimefuatilia kwa karibu sana mchakato wa kuelekea uchaguzi mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani, nimejifunza mengi na ninaendelea kujifunza sana. Nimefuatilia mchakato wa ndani ya vyama vya siasa kupitisha wagombea wa nafasi ya Urais na hasa hasa mchakato wa Chama cha Mapinduzi (CCM), nimetupia jicho pia, mashirikiano ya vyama vyenye mawazo mbadala chini ya mwamvuli wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA), huko nako nimejifunza.

Nikiri kwamba katika miaka 10 iliyopita ushiriki wangu katika siasa za maendeleo umenifunza mengi, nimeona namna ambavyo siasa za asasi za kiraia zilivyo na zinavyogubikwa ila ile dhana na uhalisia wa kutafuta madaraka au “struggle for power”. Kimsingi asasi hizi za kiraia ndio hasa sauti za wananchi, maana hata shule tunasoma kwamba asasi za kiraia ndio uwanja wa wananchi kudai na kutetea haki zao dhidi ya Dola (state), sekta binafsi (Private sector) na nguvu ya soko (Market forces). Nikang’amua nako kuna siasa kweli kweli, lakini kazi lazima iende, lazima tuendelee kusimamia maslahi ya raia na wananchi wa Taifa letu.

Rai yangu kwa asasi za kiraia ni kuweka mbele maslahi ya Wananchi na kujitahidi kuweka pembeni maslahi binafsi, tukumbuke asasi za kiraia imara ndio sauti ya Wananchi kwa serikali yao dhidi ya nguvu za soko pamoja na sekta binafsi.

Baada ya kushiriki mchakato wa Katiba, huko nako nikaona siasa za kutosha, huko ndio nikajua siasa za vyama vya siasa ambazo kimsingi zinalenga kulinda maslahi yake kwanza kuliko hata yale ya Taifa. Na ninapozungumzia vyama nazungumzia vyama vyote, kwa maana ya chama kilichopo madarakani na vyama vyenye mawazo mbadala. Hapo niliona namna gani ukijaribu kugusa maslahi ya watu na vyama vyama siasa, hasa yale ambayo yamejikita katika kujenga himaya za kisiasa, kukamata nafasi za madaraka na kuzishikilia ikiwezekana wakati wowote, utapata upinzani mkubwa. Ninaposema kugusa maslahi ya watu na ya vyama vya siasa namaanisha maslahi ambayo mara nyingi hujikita katika kunufaisha wachache katika gharama ya wengi.

Kwenye sekta binafsi ndio kuna matatizo makubwa, huko lengo kuu ni kuongeza faida kwa namna yoyote. Wengi wao wanalo pia lengo la kujitahidi kukwepa kodi ili mapato ambayo wanayakusanya kutoka kwa umma wa watanzania yasiguswe kwa namna yoyote. Huu unaitwa udhalimu, uporaji wa rasilimali za watanzania na wizi ambao hautendwi katika nchi ya mbali bali hapa hapa nchini kwetu. Ukitizama vizuri utagundua hawa jamaa ndio ambao wameshikilia hata uwezo wa serikali kufanya maamuzi lakini hawa huwa hawaonekani mbele ya hadhira, mara nyingi hukaa nyuma ya pazia na mara chache hujitokeza kutoa mtisho mkuu na kutokomea nyuma ya pazia baada ya kutufanya tuweweseke sisi raia na serikali yetu.

Sekta binafsi na wadau wake ni watu wenye nguvu kweli na ukitaka kujua nguvu yao jaribu kurejea mifano michache tu kama vile siku wenye mabasi ya abiria wakigomea nauli au kiwango cha mwendo kasi, itabidi waziri afanye mazungumzo mara moja. Licha ya kwamba tuna reli ya kati na ile ya TAZARA yenye uwezo mkubwa wa kubeba shehena za mizigo lakini siku wamiliki wa malori TATOA wakigoma kusogeza tu malori yao bandarini kwa kigezo kwamba uendeshaji wa mizani katika barabara zetu una tatizo vivyo hivyo serikali itakimbia mara moja na kutatua suala lao.

Hawa watu wa sekta binafsi na Taasisi zao huwa hawana mzaha na kazi zao, kama nilivyosema ni kutengeneza faida katika gharama yoyote. Katika nchi nyingine na wala haziko mbali nasi, sekta binafsi ndio hufadhili hata vita zinazoendelea ili mkiwa mnapigana wao wanachukua rasilimali zenu.

Tunamshukuru Mungu hapa kwetu tuko sawa, lakini haimaanishi tukiwa wazembe tutaendelea kuwa sawa, na uzembe namaanisha pale Wananchi tutakapoiacha nchi yetu mikononi mwa viongozi na watumishi wa umma pekee. Ni lazima tuwe mstari wa mbele kujua kila linaloendelea kwasababu faida ya usimamizi mzuri wa siasa zetu ambazo ndio huamua mustakabali wa matumizi ya rasilimali zetu huwa kwetu sote. Aidha, usimamizi mbovu wa siasa zetu na kwa uzembe tu kushindwa kushiriki katika shughuli za kiraia kama raia hutuzalishia viongozi wabovu, wabinafsi, wabadhirifu na wenye kujipenda wenyewe na si maendeleo na ustawi wa watu wetu.

Hapa nyumbani tumeshaanza kuona viashiria, unakumbuka Wananchi mlisema mikataba ya madini lazima iwe wazi kwa kila raia anayetaka kujua yaliyomo kwenye mikataba hiyo. Rasimu ya Warioba ilisema Bunge liwe linaridhia mikataba ya rasilimali kabla haijaanza kutumika katika Jamhuri yetu. Bunge Maalum lilifuta masharti hayo muhimu yaliyokuwa na lengo la kuweka uwazi katika matumizi ya rasilimali zetu na hatimaye Katiba Inayopendekezwa haina masharti haya muhimu yaliyotolewa na Wananchi.

Unakumbuka pia kipindi baada ya Bunge Maalum, katika vikao vya Bunge la Muungano ilizuka hoja ya kudai mikataba ya gesi na mafuta iletwe, lakini serikali ikakataa. Unakumbuka Kamati ya Mahesabu ya mashirika ya umma (PAC) nayo ikaomba kupewa mikataba, ikanyimwa, hata wakaenda mbali kwa hasira kuielekeza polisi kuwakamata watendaji wakuu wa Shirika la Taifa la Uendelezaji wa Sekta ya Mafuta (TPDC). Mwisho wa siku Bunge likashindwa, na mikataba bado ni siri, na utagundua hata wale walioshabikia kufutwa kwa masharti ya Rasimu ya Warioba ya uwazi wa mikataba baadaye walianza kujirudi kwamba lazima mikataba iwe wazi, kwa kiingereza tabia hii ningeita “too good too late” kwa maana ya ukifanya mazuri mwishoni ni kazibure.

Tafsiri ya kuwa raia makini na majukumu yako kwa Taifa

Hapa nataka nianze na imani zetu, nianze na uislamu, katika uislamu kuna mstari mwembamba sana kati ya imani ya muumin na masuala ya kiraia yakiwemo yahusuyo utawala wa nchi. Katika uislam, kimsingi imani inapasa kutoa hamasa kwa namna ulimwengu wa siasa unaenenda. Tafsiri yangu ni kwamba katika mazingira ya kawaida na hasa katika nchi kama yetu ya Tanzania ambapo tuna mfumo unaotenganisha utendaji wa shughuli za dini/imani na mamlaka ya nchi, jukumu pekee nilionalo kwa watanzania waumin wa kiislam ni kuhakikisha wanafuata maagizo ya vitabu vya dini. Muumin mzuri wa dini ya kiislamu ameelekezwa kwamba imani (ya uislamu) lazima itoe hamasa ya namna mamlaka ya nchi inaenenda. Ili utoe hamasa ni lazima ushiriki katika shughuli za kiraia na za kisiasa ili matendo yako mema kama muumin tukayaone katika utendaji wa mamlaka za nchi.

Tafsiri inaendelea, hivyo kama wewe ni muumin wa dini ya kiislamu hufuatilii namna nchi yako inaongozwa kwa kigezo kwamba unawaachia viongozi pekee na huhudhurii vikao vya maendeleo katika eneo lako na hujajiandikisha na hutakwenda kusikiliza wagombea wakijinadi katika kampeni na hutapiga kura katika siku ya uchaguzi ujue unakwenda kinyume na Quran Tukufu na katika siku ya kiyama jehanum inakusubiri, yaani ule moto wa milele ni halali yako.

Kwa waumini wa dini ya kikristo, wao Biblia Takatifu imeeleza kabisa kwamba katika Warumi 13:1-7 “1 Kila mtu anapaswa kuwatii wenye mamlaka katika serikali; maana mamlaka yote hutoka kwa Mungu; nao wenye mamlaka wamewekwa na Mungu. 2 Anayepinga mamlaka ya viongozi anapinga agizo la Mungu; nao wafanyao hivyo wanajiletea hukumu wenyewe, 3 Maana, watawala hawasababishi hofu kwa watu wema, ila kwa watu wabaya. Basi, wataka usimwogope mtu mwenye mamlaka? Fanya mema naye atakusifu; 4 maana yeye ni mtumishi wa Mungu anayefanya kazi kwa faida yako. Lakini ukifanya mabaya, basi, huna budi kumwogopa, maana anao kweli uwezo wa kutoa adhabu. Yeye ni mtumishi wa Mungu na huitekeleza ghadhabu ya Mungu kwao watendao maovu. 5 Kwa hiyo ni lazima kuwatii wenye mamlaka, si tu kwa sababu ya kuogopa ghadhabu ya Mungu, bali pia kwa sababu dhamiri inadai hivyo. 6 Kwa sababu hiyohiyo ninyi hulipa kodi; maana viongozi hao humtumikia Mungu ikiwa wanatimiza wajibu wao. 7 Mpeni kila mtu haki yake; mtu wa ushuru, ushuru; wa kodi, kodi; na astahiliye heshima, heshima.”

Nikitafsiri maandiko hayo, ni dhahiri kwamba kwa waumini wa dini ya kikristo Mamlaka ya nchi imeletwa na Mungu, na kama mjuavyo yote yaletwayo na Mungu huwa ni maelekezo na amri. Kama Serikali, Bunge na Mahakama zimeletwa na Mungu, je sisi waumini tunapaswa kujiepusha nazo? Je kujiepusha na mambo yaliyoletwa na Mungu katika imani ya kikristo tafsiri yake ni nini? Na ninapozungumzia kujiepusha kimsingi nazungumzia kwamba mamlaka ya nchi hutolewa na Wananchi kikatiba kwa kupiga kura na kushiriki katika shughuli za umma. Kwahiyo mkristo ambaye hafuatilii namna nchi yako inaongozwa kwa kigezo kwamba unawaachia viongozi pekee na huhudhurii vikao vya maendeleo katika eneo lako eti kisa umeenda katika “fellowship” kanisani wakati wote na hujajiandikisha na hutakwenda kusikiliza wagombea wakijinadi katika kampeni na hutapiga kura katika siku ya uchaguzi ujue unakwenda kinyume na Maelekezo ya Mungu wa Mbinguni na katika siku ya hukumu utaelekezwa katika ziwa la moto wa milele, na milele ukisaga meno.

Monday, July 6, 2015

TUJIKUMBUSHE MAPENDEKEZO YA KAMATI ZA BUNGE MAALUM YATAKAYOVUNJA MUUNGANO, HII IWE CHANGAMOTO KWA RAIS AJAYE


















MASLAHI ZAIDI KWA ZANZIBAR NI SUTI KAMILI YA MUUNGANO KWA TANGANYIKA


Ni kweli kwamba Bunge Maalum lilitumia muda mwingi baada ya kumaliza kanuni kujadili sura ya kwanza na sura ya sita na kujiridhisha kumaliza suala la muundo wa muungano. Uhalisia ni mbali kabisa na ukweli huu, ili kuujadili muundo wa muungano kama msingi  ilipasa sura ya kwanza, sita na kumi na tano kusomwa na kujadiliwa kwa pamoja (in tandem). Rai yangu kwa wajumbe wa Bunge Maalum ni kuhakikisha wanasoma ibara na sura zinazoendana kwa pamoja ili kupata mantinki na kutoa maboresho stahiki.

Kumekuwapo hoja kwamba ufike wakati suala la muungano maadamu limeleta ubishani mkubwa na sintofahamu nyingi basi tuliweke kando na tujadili masuala mengineyo katika rasimu. Hoja hii yaweza kuwa ina nia njema, lakini kwa hakika haitaarifiwi na uhalisia. Taifa letu ni Muungano wa zilizokuwa nchi mbili huru kabla ya mwaka 1964. Nchi hizi zilipoungana ziliundwa mamlaka tatu tofauti kikatiba, kwa maana ya Mamlaka inayohusika na Mambo ya Muungano, Mamlaka inayohusika na mambo yasiyo ya Muungano ya Zanzibar na Mamlaka inayohusika na Mambo yasiyo ya Muungano ya Tanzania Bara. Unapo andika Katiba ya Mamlaka ya Jamhuri ya Muungano ni lazima uzingatie masuala ambayo kiasili ni ya Muungano na huwa ni majukumu ya kidola (sovereign functions).

Hoja ninayojaribu kuijenga hapa ni kwamba kwa asili ya Nchi yetu, suala la muungano huwezi kulikwepa unapozungumzia Katiba Mpya. Kabla hatujafahamu suala la maji, barabara, kilimo, elimu, afya na masuala mengine ya kimaendeleo, lazima tumalize suala la Muundo wa Muungano. Ni muundo wa Muungano ndio utatupatia msingi wa kuenenda (framework) katika masuala ya muungano (majukumu ya kidola) na masuala yasiyo ya muungano (yote yahusuyo ustawi na maendeleo ya watu).

Tofauti kubwa kati ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba na Bunge Maalum ni kwamba Tume ilipoanza kazi haikuwa na hoja mfukoni bali ilipaswa kisheria kupokea maoni kutoka kwa wananchi. Bunge Maalum kisheria linapaswa kupokea hoja kutoka Tume ya Katiba, kisha kuijadili na kuipitisha. Tume ya Katiba ilipata fursa ya kusikiliza na kupokea maoni ya wananchi katika hoja mbalimbali na hata ilipofika wakati wa uchambuzi na majadiliano ndani ya Tume, wajumbe wake walijiwekea utaratibu wa kujadili masuala mengineyo na kisha kulitizama suala la muungano. Ni wazi kwamba Bunge Maalum halina fursa hiyo, Sheria ya Mabadiliko ya Katiba inalielekeza Bunge Maalum kupokea hoja kutoka kwa wananchi kupitia Tume ya Katiba. Sheria inaendelea kulielekeza Bunge Maalum katika kifungu cha 25(2) kwamba msingi wa majadiliano ya Bunge Maalum ni Rasimu ambayo imewasilishwa na Tume ya Katiba.

Vyombo vya utendaji vya Jamhuri ya Muungano

Kamati namba tatu chini ya uenyekiti wa Dkt. Francis Michael katika Taarifa yake ukurasa wa 13 inatoa pendekezo la kuendelea kuwa na serikali mbili na shughuli za Mamlaka ya nchi kusimamiwa na kutekelezwa na vyombo viwili vya utendaji, vyombo viwili vya kutunga sheria na vyombo viwili vyenye dhamana ya kutoa haki. Pendekezo hili kama lilivyo halina tofauti na hali ilivyo katika Katiba inayotumika sasa ya mwaka 1977 toleo la 2005.

Katika pendekezo hili najiuliza kama kamati imejiridhisha na uzoefu wa zaidi ya miaka 40 katika muundo wa serikali mbili na kuzingatia changamoto ambazo zimejitokeza kabla ya kupendekeza kuwepo kwa serikali mbili. Nachelea kusema kwamba kamati imegubikwa na ile dhana ya ukinzani wa mabadiliko kutokana na mazoea.

Kamati namba tatu inaendelea kujenga hoja katika ukurasa wa 14 kwa kusema kwa maoni ya wajumbe walio wengi zipo baadhi ya Changamoto katika mfumo wa Serikali mbili ila kinachohitajika ni kuzitafutia ufumbuzi, kama kazi hiyo inavyoendelea na sio kuwa na mfumo wa Shirikisho ambao utakuwa na matatizo makubwa zaidi kuliko tuliyonayo hivi sasa. Hoja ya uchache wa changamoto haina ukweli na ni upotoshwaji, naomba turejee Taarifa ya utafiti kutoka Tume ya Katiba katika suala la muungano katika ukurasa wake wa 32-34, yameainishwa maeneo zaidi ya 40 yenye changamoto katika Muungano. Mambo haya sio mageni yako na yanajulikana, kujiaminisha kwamba ziko changamoto chache ni ishara ya ama kutokuelewa uhalisia (ambao uko vitabuni) au ni kuonesha dalili za kutokuwa na dhamira ya dhati ya kuzifanyia kazi changamoto hizo.

Nieleze kwa ufupi sifa na tabia za miundo mbalimbali pamoja na namna ya kuenenda na mambo ya muungano na yale yasiyo ya muungano. Muundo wa serikali moja huwa na sifa ya kushughulikia mambo yote na tabia mojawapo ni uratibu, usimamizi na ufuatiliaji wa jumla kutoka Mamlaka Kuu (Supreme Authority). Muundo wa shirikisho huwa na sifa ya kuwa na mambo machache ya muungano pamoja na ngazi mbili za usimamizi, uratibu na ufuatiliaji. Ngazi ya kwanza ni serikali ya muungano au shirikisho kwa mambo machache yenye asili ya majukumu ya kidola na ngazi ya pili ni serikali za washirika kwa mambo yanayosalia ambao huwa na asili ya kimaendeleo zaidi.

Bado katika Muundo wa shirikisho unaweza kuwekwa utaratibu ambao unahakikisha kwamba serikali ya muungano inakuwa na mfumo mahususi wa kuratibu, kusimamia na kufuatilia ustawi wa masuala ya maendeleo hata katika ngazi za nchi washirika, mfano ni pendekezo la Rasimu ya Katiba Mpya juu ya uwepo wa Tume ya Uhusiano na Uratibu ambayo kimsingi inakazi hiyo, ibara ya 111(1)(b) inasema Tume ya Uhusiano na Uratibu ndio chombo maalum cha Jamhuri ya Muungano chenye dhamana ya kusimamia, kuratibu na kuhakikisha kwamba kuna kuwiana kwa sera na sheria za nchi washirika katika mambo yasiyo ya muungano.

Muundo wa Mkataba huwezesha mahusiano katika maeneo fulani yanayokubaliwa na nchi zinazoingia katika mkataba. Sifa ya Muungano wa Mkataba huwa ni lazima uingiwe na mataifa mawili au zaidi yaliyo huru (sovereign states). Kwa mazingira ya hapa kwetu ni kurudi nyuma ya mwaka 1964. Kwa mtizamo wangu huko hatuko na binafsi sidhani kama tunapaswa hata kufikiri kwenda huko.

Sifa kubwa mojawapo ya muundo wa serikali mbili ni kuwapo kwa mambo mengi ya muungano kama ilivyo kwenye Katiba ya 1977 au zaidi. Sifa nyingine ni nafasi ya Rais wa Jamhuri ya Muungano kuwa na mamlaka na madaraka ya usimamizi na ufuatiliaji wa ufanisi kwa masuala yasiyo ya muungano upande wa Zanzibar sambamba na Tanganyika ili awe na uhusiano wa moja kwa moja na raia wa Tanzania waishio Zanzibar kama ilivyo kwa wale wa Tanganyika. Jambo hili linabishaniwa vikali na serikali zetu mbili hasa kutoka upande wa Zanzibar, huu ndio ukarabati usiwezekana.

Mambo ya Muungano

Kamati namba tatu katika taarifa yake ukurasa wa 21 inakubaliana na pendekezo la rasimu kwamba mambo ya muungano yabaki saba, pendekezo hili linapaswa lisomwe pamoja na pendekezo la serikali mbili katika ukurasa wa 13 wa taarifa ya kamati. Kwa mtu yeyote anayejua masuala ya muungano lazima aone tatizo la msingi hapa. Huwezi kutaka serikali mbili halafu ukapunguza mambo ya muungano. Kitendo cha kupunguza mambo ya muungano kinakuleta katika muundo wa shirikisho ambao mambo machache yanabaki kwa serikali ya shirikisho (kama kwenye rasimu) na yanayobaki yanakuwa kwa washirika.

Unapokuwa na mambo machache ya muungano ndani ya muundo wa serikali mbili ambapo serikali ya muungano inashughulikia mambo ya muungano na yasiyo ya muungano ya Tanzania Bara au Tanganyika tafsiri yake ni kwamba; Jamhuri ya Muungano ndio itakuwa Tanganyika na Zanzibar itakuwa imepachikwa tu katika muungano huu. Kwa maneno mengine tutakuwa tumeweka uhusiano kati ya Zanzibar na Jamhuri ya Muungano katika masuala ya ulinzi na usalama kwa kiasi kikubwa pekee.


Kwa mapendekezo haya ya kamati namba tatu, hayatatuacha tena na Nchi moja tena yenye uraia mmoja bali tutakuwa tumeigeuza Zanzibar kuwa Nchi kamili yenye mamlaka yote isipokuwa ulinzi na usalama ambalo litakuwa jukumu ya Jamhuri ya Muungano. Tukifika hapo tutakuwa tunafanana kabisa na uhusiano uliopo kati ya Nchi ya Italia na San Marino au uhusiano wa Nchi ya Ufaransa na Monako. Narudia huo utakuwa Muungano dhaifu kabisa wa serikali mbili ambao utaendeleza kero na kwa vile una mianya mingi ya udhaifu mwishowe utavunja muungano wetu wa kihistoria.