Tuesday, March 10, 2015

SABABU 15 WIKI HII ZA KUSEMA HAPANA KWA KATIBA INAYOPENDEKEZWA

SABABU 15 WIKI HII ZA KUSEMA HAPANA KWA KATIBA INAYOPENDEKEZWA

Katiba Mpya inapaswa kuwa Mpya kweli kweli na si vinginevyo

1.    Uhuru wa Mkuu wa Jeshi la Polisi

Rasimu ya Warioba ilipendekeza Mkuu wa Jeshi la Polisi atekeleze kazi zake kwa uhuru, bila woga, upendeleo wala chuki na kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii na sheria za nchi. Masharti haya yamefutwa na Katiba Inayopendekezwa

2.    Tume ya Utumishi wa Jeshi la Wananchi

Tume ya Warioba ilipendekeza kuwepo kwa Tume ya Utumishi ya Jeshi la Ulinzi la
Wananchi wa Tanzania itakayokuwa na jukumu la kusimamia masuala yote ya utumishi katika Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania. Katiba Inayopendekezwa imefuta masharti haya licha ya wapiganaji wetu kupendekeza utaratibu wa kusimamia maslahi yao Kikatiba.

3.    Tume ya Utumishi wa Jeshi la Polisi

Kutakuwa na Tume ya Utumishi wa Jeshi la Polisi itakayokuwa na jukumu la kusimamia utumishi wa Jeshi la Polisi. Katika uajiri wa askari wa Jeshi la Polisi, Tume ya Utumishi wa Jeshi la Polisi itazingatia kanuni na misingi ya utumishi iliyoainishwa katika Katiba hii

4.    Misingi ya utendaji wa Jeshi la Polisi

Rasimu ya Warioba ilipendekeza kwamba katika utekelezaji wa majukumu yake, Jeshi la Polisi la Jamhuri ya Muungano litazingatia (a) viwango vya juu vya kitaaluma na nidhamu miongoni mwa wafanyakazi wake; (b) ulinzi na ukuzaji wa haki za binadamu; (c) kanuni za uwazi na uwajibikaji; na (d) kukuza mahusiano na jamii. Warioba akaendelea kusema, Jeshi la Polisi, katika kutekeleza majukumu yake, litashirikiana na vyombo vinavyohusika na kupambana na uhalifu vya Nchi Washirika katika kufanya uchunguzi na kushughulikia makosa ya rushwa na ufisadi.
Misingi hii yote imefutwa na Katiba Inayopendekezwa

5.    Kuhusu Sifa ya Kielimu kwa Mbunge

Rasimu ya Warioba ilipendekeza sifa mojawapo ya kuwa mbunge ni kuwa na elimu isiyopungua kidato cha nne na ajue kusoma na kuandika lugha ya Kiswahili au kiingereza. Baadhi ya sababu za kuunga mkono pendekezo hili ni pamoja na maendeleo ya sayansi na teknolojia pamoja na Changamoto zilizoko katika sekta za uchumi, elimu na utandawazi ipo haja ya Mbunge kuwa na elimu ya kutosha kuweza kukabiliana na Changamoto zinazosababishwa na mabadiliko haya.

Katiba Inayopendekezwa inapendekeza sifa mojawapo ya kuwa Mbunge ni kujua na kusoma lugha ya Kiswahili au kiingereza. Pendekezo hili liko mbali kabisa na chini ya kiwango cha maoni ya watumishi wa Ofisi ya Rais Tume ya Utumishi wa Umma.

6.    Nafasi za Makatibu Wakuu na Naibu Makatibu Wakuu Kikatiba

Rasimu ya Warioba ilipendekeza kuweko na nafasi kikatiba za Makatibu Wakuu watakaoteuliwa na Rais kutoka miongoni mwa watumishi waandamizi katika utumishi wa umma kama watakavyopendekezwa na Tume ya Utumishi wa Umma.  Kila Katibu Mkuu atakuwa kiongozi na Mtendaji Mkuu wa Wizara ya Serikali aliyopangiwa na Rais na atashika nafasi ya madaraka ya Katibu Mkuu na kutekeleza majukumu yake kama itakavyoainishwa katika sheria za nchi. 

Rais anaweza, kwa mapendekezo ya Tume ya Utumishi wa Umma, kumteua mtumishi mwandamizi katika Utumishi wa Umma kuwa Naibu Katibu Mkuu.  Kila Katibu Mkuu atakuwa mshauri wa mwisho kwa Waziri kwa masuala yote ya utendaji na atatoa ushauri kwa Baraza la Mawaziri katika vikao na Kamati zitakazoitishwa na Katibu wa Baraza la Mawaziri. Katibu Mkuu au Naibu Katibu Mkuu hatashika madaraka yake hadi awe ameapa mbele ya Rais kiapo cha utii na uaminifu au kiapo kingine chochote kinachohusu utendaji wa kazi zake kitakachowekwa kwa mujibu wa sheria za nchi. Katiba Inayopendekezwa imefuta masharti haya na kudhoofisha ujenzi wa utumishi wa umma kikatiba.

7.    Kamati Maalum ya Makatibu Wakuu

Rasimu ya Warioba ilipendekeza kuwepo kikatiba kwa Kamati Maalum ya Makatibu Wakuu itakayoongozwa na Katibu Mkuu Kiongozi ambayo itakuwa na majukumu ya kuchambua na kulishauri Baraza la Mawaziri juu ya masuala mbalimbali kabla ya kuwasilishwa na kufanyiwa uamuzi na Baraza hilo na itatekeleza majukumu mengine kama itakavyopangiwa na Baraza la Mawaziri.

Katiba Inayopendekezwa imefuta msharti hayo yote mahususi licha ya kwamba huu ulikuwa wakati muafaka wa kuiimarisha sekta ya utumishi wa umma Kikatiba ili iendelee kutuhudumia wananchi ikiwa na ari, kujiamini na kutenda kwa weledi pasina ya kuvurugwa na mara kadhaa na wanasiasa wabaya.

8.    Uhuru wa Habari na vyombo vya Habari

Katiba Inayopendekezwa imeweka masharti “pokonyezi” (claw-back clauses) kwenye ibara ya Uhuru wa Habari na vyombo vya Habari. Rasimu ya Warioba inatoa wajibu kusambaza habari na taarifa kwa wananchi. Katiba Inayopendekezwa inatoa wajibu wa kusambaza habari na taarifa sahihi na za ukweli kwa wananchi.

Kuweka maneno taarifa sahihi na za ukweli ni kuminya haki hii, Katiba inapasa kuweka msingi na sheria ingetoa ufafanuzi. Kuwekwa hapa masharti haya kutapelekea kutumika ndivyo sivyo. kuzingatia miiko ya taaluma ya uandishi na utangazaji wa habari ni suala la sheria na kanuni, na ikumbukwe ulimwengu wa leo hautegemei pekee wanataaluma wa habari kutoa habari, kifungu hiki kitaminya haki hii. Kwa kuweka maneno haya katika masharti ya ibara hii, Uhuru wa Habari na vyombo vya Habari uko mashakani kabisa

9.    Haki ya Elimu na Kujifunza

Wananchi walipendekeza kutolewa kwa elimu bora ya msingi bure na bila vikwazo ikiwemo kupata elimu bora inayotolewa nje ya utaratibu wa umma kwa gharama nafuu.

Masharti yafuatayo yamefutwa na Katiba Inayopendekezwa:-
Kila mtu ana haki ya:
§  kupata fursa ya kupata elimu bora bila ya vikwazo;
§  kupata elimu bora ya msingi bila ya malipo nainayomtayarisha kikamilifu mwanafunzi ama kuendelea naelimu ya ngazi inayofuatia au kuweka msingi wa kuanzakujitegemea;
§  kupata elimu bora inayotolewa nje ya utaratibu wa ummakwa gharama nafuu; na

10. Haki ya Mtoto

Wananchi walipendekeza kutolewa ulinzi zaidi kwa haki za mtoto na Rasimu ya Katiba Mpya Toleo la Pili iliweka masharti yaliyoelekeza Mamlaka ya Nchi kuweka utaratibu wa Kisheria utakaowezesha utekelezaji na usimamizi wa haki za mtoto kwa kufuata msingi wa kutoakipaumbele kwa maslahi na manufaa ya mtoto. Masharti haya yamefutwa na Katiba Inayopendekezwa na kufanya haki zilizowekwa katika Ibara hii kuwa kiini macho.

11. Haki za watu wenye Ulemavu

Wananchi na hasa watu wenye ulemavu walipendekeza mamlaka ya nchi kuweka utaratibu wa sheria utakaowezesha watu wenye ulemavu kushiriki kwenye nafasi za uwakilishi.

Katiba inayopendekezwa imeondoa jukumu hili na tafsiri yake ni kwamba wawakilishi wa watu wenye ulemavu wataendelea kuteuliwa pasina ya kuwa na msingi wa kikatiba na kisheria kuhakikisha watu wenye ulemavu wanawachagua wawakilishi wao tofauti na sasa.

12. Haki za Wanawake

Wananchi waliotoa maoni hasa wanawake na wanaume walipendekeza kwa sauti moja kuona haki za wanawake zinalindwa, zinahifadhiwa, zinatolewa na kutekelezwa kwa wakati na mamlaka za nchi. Wananchi walipendekeza kuona wanawake wanalindwa dhidi ya unyonyaji na ukatili. Katiba Inayopendekezwa sio tu imefuta kifungu kinachomlinda mwanamke dhidi ya unyonyaji bali pia imefuta masharti elekezi yaliyokuwamo katika Rasimu ya Warioba ambayo yalikuwa yanazielekeza Mamlaka za nchi kuweka utaratibu wa kisheria utakaosimamia masuala yanayohusu utekelezaji wa masharti ya Ibara hii ikiwa ni pamoja na kukuza utu, heshima, usalama na fursa za wanawakewakiwemo wajane.

13. Kamati ya Uteuzi wa Tume Huru ya Uchaguzi

Rasimu ya Warioba ilipendekeza katika kifungu cha 191 kwamba Asasi za Kiraia zinaweza kupendekeza kwa Kamati ya Uteuzi majina ya watu wanaofaa kuwa Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti na wajumbe wa Tume Huru ya Uchaguzi. Katiba Inayopendekezwa katika Ibara yake ya 218 imefuta masharti yaliyotoa fursa kwa asasi za kiraia na asasi zisizokuwa za kiserikali kupendekeza watu watakaofaa kuhudumu katika Tume Huru ya Uchaguzi. Kila mtu ataelewa nafasi muhimu kabisa ya Asasi za Kiraia katika maendeleo ya Taifa letu hasa ukizingatia ni asasi hizi ndizo zinashirikiana na serikali katika kujenga uwajibikaji na kuimarisha utawala bora nchini.

14. Ujumbe wa Tume na Kanuni za Maadili ya Viongozi wa Umma

Rasimu ya Warioba katika Ibara yake ya 192(4) ilipendekeza kwamba “Mjumbe wa Tume Huru ya Uchaguzi ambaye atakiukamasharti ya kanuni za maadili atapoteza sifa za kuendelea kuwa mjumbe”. Masharti haya yaliwekwa kuhakikisha kwamba wajumbe wanayaishi maadili, miiko na kanuni za utumishi wa umma hasa ukizingatia uadilifu wa Tume Huru ya Uchaguzi ni kigezo kikubwa cha ujenzi wa demokrasia imara na makini kwa Taifa letu. Katiba Inayopendekezwa katika Ibara ya 219 imeyafifisha na kuondoa masharti ya moja kwa moja kama yalivyokuwa katika rasimu ya Warioba.

15. Wajibu wa Tume Huru ya Uchaguzi


Rasimu ya Warioba katika ibara 193(3)(b) ilieleza bayana kwamba mojawapo ya majukumu ya Tume Huru ya Uchaguzi ni pamoja na kuhakikisha kuna ya uwakilishi unaozingatia jinsi. Masharti haya yanapaswa kusomwa sambamba na masharti yaliyomo katika Rasimu ya Warioba Ibara ya 113 juu ya uwakilishi wa 50 kwa 50 kati ya Wanawake na Wanaume ambao msingi wake ulikuwa katika ngazi ya jimbo. Ili ujue Katiba Inayopendekezwa na walioshiriki kuiandika ama kwa kujua au kwa kutokujua na kwa hila wamefuta masharti ya usawa kati ya wanawake na wanaume ni pale walipofuta jukumu la Tume kusimamia usawa wa jinsi, ukisoma Katiba Inayopendekezwa ibara ya 220(3) utagundua masharti hayo hayapo.

KUMBUKA UKISEMA HAPANA MUDA UKIFIKA, NA KWA MUJIBU WA KIFUNGU CHA 35 CHA SHERIA YA KURA YA MAONI, BUNGE MAALUM LITAITISHWA TENA KWENDA KUREKEBISHA MAPUNGUFU HAYA NA KUZINGATIA MAONI YA WANANCHI. MJULISHE MWINGINE HARAKA

NA USIKOSE KUSOMA GAZETI LA RAI ALHAMISI NA MWANANCHI JUMAPILI KWA MAELEZO MAPANA ZAIDI.

No comments:

Post a Comment